Tulinde Mahali Petu pa Ibada Katika Hali Nzuri
1 Ulimwenguni pote kuna zaidi ya makutaniko 94,000 ya Mashahidi wa Yehova. Makutaniko yaliyo mengi yanakusanyika kwa ajili ya funzo la Biblia na ushirikiano wa Kikristo kwenye Jumba la Ufalme, linalotumika kuwa kitovu cha ibada safi cha mahali linapopatikana.
2 Usafishaji Unaopangwa kwa Ukawaida: Kazi inayofanywa ili kutunza Jumba la Ufalme ni sehemu ya maana sana ya utumishi wetu mtakatifu. Kitabu Huduma Yetu kinasema hivi kwenye ukurasa wa 61: “Ndugu wamepaswa walione kuwa pendeleo si kutoa tu michango ya kulipia gharama za Jumba la Ufalme, bali pia kujitolea walitunze kuwa safi, lenye kupendeza na katika hali nzuri. Jumba la Ufalme limepasa liwe mfano unaofaa wa tengenezo la Yehova, ndani na nje.” Ikiwa Jumba la Ufalme linatumiwa mara nyingi kwa juma, kutakuwa na uhitaji wa kufanya usafi na utunzaji kwa ukawaida. Kwa kawaida mambo hayo hushughulikiwa na wajitoleaji kutoka kutaniko au makutaniko yanayokusanyika katika Jumba la Ufalme. Kama katika nyakati za Biblia, watumishi wa Yehova leo wanapaswa kuwa wenye bidii katika “kutengeneza na kufanya upya” mahali petu pa ibada.—2 Nya. 34:10.
3 Programu ya usafishaji wa kila juma wa Jumba la Ufalme inapaswa kuwekwa kwenye ubao wa matangazo. Vikundi vyote vya mafunzo ya kitabu vinapaswa kupeana zamu ya kusafisha jumba kila juma, vikifuata orodha ya mambo yanayopasa kufanywa. Wote walio na uwezo wanapaswa kushiriki pendeleo la kila juma la kulinda Jumba la Ufalme likiwa safi na lenye kupendeza. Chini ya usimamizi wa wazazi, watoto wanaweza kuhusishwa; kwa njia hiyo watafundishwa kuonyesha uthamini kuelekea pendeleo hilo. Hasa, makutaniko mengi yanapotumia Jumba la Ufalme, ushirikiano mzuri ni wa lazima ili kushughulikia sehemu hiyo ya maana ya ibada yetu kusilemee watu wachache tu.
4 Orodha ya mambo ya kufanya inapaswa kuwekwa, ikiwezekana, mahali ambapo vifaa vya kazi vinalindwa. Orodha hiyo inapaswa kufafanua kazi za kufanya kila juma, kutia ndani kuvuta vumbi, kuondoa tando za buibui, kusafisha madirisha au kupangusa vumbi juu ya matofali yenye matundu-matundu mahali ambapo hayo yanatumiwa badala ya madirisha, kuondoa vumbi juu ya meza za vichapo, kumwaga uchafu kutoka vikapu vya takataka, kusafisha sakafu na vioo. Kazi nyingine zinaweza kufanywa mara chache, kama vile kung’arisha vifaa vyovyote vya mbao na kusafisha kikamili viti, benchi, pazia, na vyombo vya kutundikia taa. Kemikali zote zinazotumiwa katika usafishaji zinapaswa kulindwa mbali na watoto, na zinapaswa kuwa na majina yenye kuandikwa waziwazi juu yazo. Maelezo machache kuhusu jinsi kila kemikali inavyopaswa kutumiwa yanapaswa kutolewa.
5 Usalama kwenye Jumba la Ufalme ni wa maana sana. (Kum. 22:8) Kuhusiana na jambo hilo, kisanduku kwenye ukurasa wa 4 kinaonyesha vitu fulani vinavyohitaji kufanyiwa uchunguzi mara kwa mara ili kuzuia misiba. Mapendekezo hayo yanapaswa kutumikishwa kuhusiana na chumba cha mlinzi wa jumba.
6 Tutunze Jumba Letu la Ufalme: Baraza la wazee lina daraka la kusimamia utunzaji wa Jumba la Ufalme. Kwa kawaida, mzee au mtumishi wa huduma mmoja huchaguliwa ili kusimamia kazi hiyo. Anapanga jinsi Jumba la Ufalme litakavyotumiwa kila siku, akihakikisha kwamba linalindwa likiwa safi na katika hali nzuri na kwamba kuna vifaa vya kutosha. Ni jambo la maana kuhakikisha kwamba hakuna hali zinazoweza kutokeza hatari katika jumba au kandokando. Wakati kutaniko moja au mawili yanatumia jumba lilelile, mabaraza ya wazee yanaweka rasmi halmashauri inayoendesha kazi ili kufanya mipango kwa ajili ya kutunza jengo na kiwanja. Halmashauri hiyo inafanya kazi chini ya uongozi wa mabaraza ya wazee.
7 Uchunguzi kamili wa Jumba la Ufalme unafanywa kila mwaka kwa kutumia fomu CN-14, inayoandaliwa na Ofisi ya Tawi Inayohusika na Ujenzi wa Majumba ya Ufalme. Wazee wana daraka la kufanya mipango ili kushughulikia kikamili mambo yoyote yanayohitaji uangalifu. Wahubiri wanaweza kuombwa wasaidie kufanya utunzaji unaohitajiwa. Wote wanapaswa kujitahidi kutengeneza hata mambo madogo-madogo na kufanya haraka katika kushughulikia mambo yanayohitaji uangalifu.
8 Ikiwa wazee wanahitaji shauri au msaada katika kushughulikia utunzaji wa Jumba la Ufalme, wanaweza kuwasiliana na Ofisi ya Tawi Inayohusika na Ujenzi wa Majumba ya Ufalme. Jambo hilo linaweza kuhusisha mambo kama vile kushughulikia kazi ya kupamba ukuta, kutengeneza vifaa vyenye kuning’inizwa kwenye dari ili kuleta baridi ikiwa hivyo vinatumiwa, kusuluhisha matatizo ya uashi na ya kuvuja kwa jengo.
9 Tutumie Fedha za Kutaniko kwa Hekima: Sehemu kubwa ya kazi kwenye Jumba la Ufalme na katika kiwanja inafanywa na wajitoleaji. Jitihada wanazofanya kwa kujinyima ni wonyesho bora wa upendo na zinasaidia sana katika kupunguza gharama. Ikiwa linakuwa jambo la lazima kuajiri fundi ili ashughulikie kazi fulani, kama vile kuua wadudu au kuondoa uchafu kutoka katika choo chenye kujaa, wazee watatafuta njia isiyoomba pesa nyingi sana ili kufanya kazi hizo. Watafanya hivyo kwa kutayarisha kwanza maelezo yenye mambo yote kuhusu kazi inayopaswa kufanywa na vifaa vyovyote vinavyopaswa kutolewa. Nakala ya orodha hiyo itatolewa kwa watoaji mbalimbali wa huduma au vifaa ili wote wakadirie bei wakiwa na uelewevu uleule wa mambo yanayotakiwa. Baada ya kupokea bei kutoka kwa wale wanaoweza kutoa huduma au vifaa, wazee wanaweza kuchagua toleo bora zaidi. Utaratibu huo unapaswa kufuatwa hata ikiwa ndugu fulani amependekeza kufanya kazi hiyo au kutoa vifaa vinavyohitajiwa kwa bei fulani.
10 Wazee wanachukua pia hatua zinazofaa ili kupata ruhusa ya kutolipa kodi ya uwanja na ya uuzaji, mahali ambapo hiyo inapatikana. Wakati Jumba la Ufalme linapotumiwa na zaidi ya kutaniko moja, halmashauri inayoendesha kazi italinda fedha tofauti-tofauti na kutoa kila mwezi ripoti ya fedha kwa kila halmashauri ya wazee; kwa njia hiyo wazee wataendelea kujua jinsi fedha zinavyotumiwa. Ni daraka la wazee kuhakikisha kwamba fedha za kutaniko zinatumiwa inavyofaa.
11 Utengenezaji na Urekebishaji Mkubwa: Inapotambua kwamba jambo fulani kubwa linahitajiwa kuhusiana na utendaji au utunzaji wa Jumba la Ufalme, halmashauri inayoendesha kazi inatoa habari hiyo kwa mabaraza ya wazee ili kupata mwongozo. Ikiwa inaonekana kwamba utengenezaji na urekebishaji mkubwa utahitajiwa au kwamba msaada utahitajiwa kutoka nje ya kutaniko au makutaniko yanayokutana kwenye Jumba hilo la Ufalme, wazee watawasiliana na Ofisi ya Tawi Inayohusika na Ujenzi wa Majumba ya Ufalme. Ndugu hao wenye sifa na wenye uzoefu watatoa mapendekezo yenye kufaa na usimamizi katika kuongoza kazi. Ikiwa gharama kubwa inahusika, litakuwa jambo la lazima kupata kadirio sahihi la gharama hiyo na kutayarisha azimio kwa ajili ya kuomba ukubali wa kutaniko.—Ona Majibu kwa Maulizo Yenu katika Huduma Yetu ya Ufalme ya Agosti 1994.
12 Tunathamini kama nini pendeleo letu la kukutana pamoja katika Jumba la Ufalme! Hatutataka kamwe kupuuza mikutano yetu wala kuiona kuwa isiyo na thamani nyingi. Sote tunaweza kuchangia mafanikio ya uandalizi huo unaotutia moyo kwa kushiriki kikamili katika kutunza Jumba letu la Ufalme. Jambo hilo linatukuza ibada safi na kuletea jina la Yehova heshima. Acheni tuazimie kulinda mahali petu pa ibada katika hali nzuri.
[Study Questions]
1. Ni nini lililo kusudi la Jumba la Ufalme?
2. Kwa nini ni jambo la maana kulinda Jumba la Ufalme likiwa safi na lenye kupendeza?
3. Usafishaji wa Jumba la Ufalme unapangwaje, na ni nani anayeweza kushiriki pendeleo hilo?
4. Ni nini kinachopaswa kufanywa ili kutaniko lijue la kufanya wakati wa kusafisha Jumba la Ufalme?
5. Usalama ni wa maana kadiri gani, na ni mambo gani yanayopaswa kufanyiwa uchunguzi mara kwa mara? (Ona kisanduku kwenye ukurasa wa 4.)
6. Kazi ya kutunza Jumba la Ufalme inasimamiwaje?
7. (a) Ni nini kinachofanywa kila mwaka ili kuhakikisha kwamba Jumba la Ufalme linalindwa katika hali nzuri? (b) Ni mambo gani yanayotaka uangalifu wa mara kwa mara? (Ona kisanduku kwenye ukurasa wa 5.)
8. Ni wakati gani wazee wanaweza kuwasiliana na Ofisi ya Tawi Inayohusika na Ujenzi wa Majumba ya Ufalme kuhusu mambo ya utunzaji?
9. Ni utaratibu gani unaopaswa kufuatwa ikiwa kuna uhitaji wa kuajiri fundi?
10. Ni nini kinachofanywa ili kuhakikisha kwamba fedha za kutaniko zinatumiwa inavyofaa?
11. Ni nini kinachopaswa kufanywa ikiwa utengenezaji au urekebishaji mkubwa unahitajiwa?
12. Tunawezaje kuonyesha kwamba tunathamini pendeleo letu la kuhudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme?
[Picha kwenye ukurasa wa 4]
Orodha ya Mambo ya Kuchunguza Kuhusu Usalama
◻ Vyombo vya kuzima moto vinapaswa kuwa karibu-karibu na kufanyiwa utunzaji kila mwaka.
◻ Milango ya kutokea na ngazi zinapaswa kuonyeshwa wazi, kuwa na mwangaza wa kutosha, na kuwa bila vizuizi; mahali pa kukamatia ili kupanda au kushuka ngazi panapaswa kuwa salama.
◻ Vyumba vya kuwekea vifaa, na vyoo vinapaswa kuwa safi, vyenye utaratibu, na bila vifaa vinavyoweza kushika moto haraka sana, vifaa vya kibinafsi wala takataka.
◻ Paa na mifereji ya kushusha maji toka kwenye paa inapaswa kufanyiwa uchunguzi na kusafishwa kwa ukawaida.
◻ Vijia na mahali pa kuegeshea magari panapaswa kuwa bila hali zinazoweza kutokeza kuteleza au kuanguka.
◻ Mifumo ya umeme na ya baridi inapaswa kuchunguzwa na kurekebishwa inavyofaa.
◻ Mahali popote panapovuja panapaswa kutengenezwa haraka ili kuepuka kuvu.
◻ Chumba cha mlinzi kinapaswa sikuzote kuwa safi, chenye kupangwa vizuri; takataka na vitu vya kuwaka moto havipaswi kupatikana ndani.
◻ Jengo linapaswa kufungwa kwa kufuli wakati hakuna mtu katika kiwanja.
[Kisanduku kwenye ukurasa wa 5]
Utunzaji wa Jengo na wa Kiwanja
◻ Nje: Je, paa, sehemu ya ukuta inayoonekana nje, rangi, madirisha, na kibao chenye alama “Jumba la Ufalme” vinatunzwa vizuri?
◻ Uwanja: Je, uwanja unatunzwa vizuri? Je, vijia, ua, na mahali pa kuegeshea magari pako katika hali nzuri?
◻ Ndani: Je, pazia, viti na benchi, vifaa vya umeme, rangi kwenye kuta na makabati ya vichapo ni ya kupendeza?
◻ Vifaa: Je, mifumo ya mwangaza, ya sauti, na ya kupitisha hewa ya baridi inatumika inavyofaa?
◻ Vyoo: Je, ni safi na vyenye kutumika inavyofaa?
◻ Hati za kutaniko: Je, mnazo nakala za hati halali za kiwanja kwa ajili ya faili zenu (Kwa mfano, Certificat d’enregistrement, Contrat de location, Acte de vente)? Je, fomu za kuomba ruhusa ya kutolipa kodi ya kiwanja zinajazwa kila mwaka mahali ambako zinahitajiwa?