Kuvaa Utu Mpya
1 Wakristo hufurahi kwa kuwa wamejua kweli! Hiyo imetufundisha jinsi ya kuishi ili tuepuke mwendo wa watu wa ulimwengu. Kwa kuwa ‘wamefanywa wageni kwa uhai ambao ni wa Mungu,’ watu hao ‘wamo katika giza kiakili.’ (Efe. 4:18) Tumekuwa tukifundishwa kufanya upya akili zetu kutoka mafikiri ya ulimwengu kwa kuvua utu wa hapo zamani na kuvaa utu mpya.—Efe. 4:22-24.
2 Utu wa hapo zamani huongoza kwenye mwendo unaozidi wa kuharibika kwa adili ambao hutokeza uchafu na kifo. Kwa hiyo, tunasihi kwa moyo wale watakaosikiliza ujumbe wa Ufalme waweke mbali hasira yenye kisasi, hasira, ubaya, usemi wenye kuudhi, na maongezi yenye aibu. Wale wanaotaka kibali cha Mungu wanapaswa kuweka mbali utu wa hapo zamani kwa uthabiti na kikamili, katika njia ileile wanavyoweza kuvua nguo chafu.—Kol. 3:8, 9.
3 Kani Mpya Inayotendesha Akili: Kuvaa utu mpya kwatia ndani kufanywa upya katika kani inayotendesha akili zetu. (Efe. 4:23) Mtu hufanyaje upya kani hiyo, au mwelekeo wa akili, ili ielekezwe katika njia inayofaa? Hilo hufanywa kwa kujifunza kikawaida na kwa bidii Neno la Mungu na kutafakari maana yake. Ndipo, namna mpya ya kufikiri husitawi, na ndipo mtu huona mambo kama vile Mungu na Kristo wayaonavyo. Maisha ya mtu hubadilika kadiri anavyositawisha sifa nyingi zilizo kama zile za Kristo, kutia ndani shauku nyororo za huruma, fadhili, hali ya akili ya kujishusha, upole, ustahimilivu na upendo.—Kol. 3:10, 12-14.
4 Kwa kuvaa utu mpya, tunawekwa kando kutoka ulimwengu. Namna yetu ya maisha hutufanya tuwe tofauti. Tunasema kweli na tunatumia usemi ulio safi ili kujenga wengine. Tunazuia hasira yetu na tunafanya sifa zenye uadilifu na za kimungu zichukue nafasi ya uchungu, kupiga kelele, matukano na ubaya wote. Kwa kuwa wenye kusamehe, tunafanya zaidi ya yale tunayoombwa. Yote hayo hutayarishwa kutoka moyoni.—Efe. 4:25-32.
5 Usivue kamwe utu mpya. Bila huo, hatuwezi kumtumikia Yehova kwa njia yenye kukubaliwa. Acha huo uvute watu kwenye kweli, na acha huo umtukuze Yehova, Muumba wa utu wetu mpya wa Kikristo ulio wa ajabu.—Efe. 4:24.