Wazazi—Toeni mfano mzuri kwa watoto wenu
1 Neno la Mungu linatuambia kwamba ‘baba [na mama] wa mwenye haki watashangilia.’ (Mez. 23:24, 25) Ni baraka kama nini kwa wazazi ambao wametoa mfano mzuri kwa watoto wao! Mshiriki mmoja wa Halmashauri ya Tawi alisema kuhusu wazazi wake: “Ile kweli ilikuwa maisha yao yote, nami nilitaka kuifanya iwe maisha yangu yote pia.” Watoto wangepaswa kuona nini katika wazazi wao?
2 Mazoea mazuri na heshima yenye kina kirefu: Ni daraka la wazazi kuingiza tabia nzuri katika watoto wao. Watoto hujifunza mazoea mazuri, si kupitia maagizo ya mdomo tu, bali kupitia kutazama na kuiga. Kwa hiyo, ni mazoea gani unayoyaonyesha? Je! watoto wako wanakusikia ukisema “unisamehe,” “tafadhali,” na “aksanti”? Katika familia yako, je! mnatendeana kwa heshima yenye kina kirefu? Je! wewe unasikiliza kwa uangalifu wakati wengine wanaposema? Je! unasikiliza wakati watoto wako wanaposema nawe? Je! tabia hizo nzuri zinaonyeshwa kwenye Jumba la Ufalme na katika faragha nyumbani?
3 Hali ya kiroho yenye nguvu na utendaji wenye bidii: Ndugu mmoja ambaye amepitisha zaidi ya miaka 50 katika utumishi wa wakati wote anakumbuka: “Mama yangu na baba yangu walikuwa mfano wa ajabu katika kuthamini kwao mikutano na katika bidii yao katika huduma.” Unaonyeshaje watoto wako kwamba unahangaikia kudumisha hali ya kiroho ya watu wa nyumbani mwako? Je! nyinyi huchunguza andiko la siku pamoja? Je! nyinyi huwa na funzo la familia la kawaida? Je! watoto wako wanakuona ukisoma Biblia na vichapo vya Sosaiti? Wao husikia nini wakati unaposali kwa ajili ya familia? Je! wewe unashiriki maongezi yenye kujenga pamoja na watoto wako, ukizungumzia mambo yenye kufaa kuhusu kweli na kutaniko? Je! nyinyi ni wenye hamu ya kuhudhuria mikutano yote na kushiriki katika huduma ya shambani mkiwa familia?
4 Wazazi, fikirini juu ya mfano mnaotoa kwa watoto wenu. Fanyeni huo uwe mfano bora, nao watauthamini katika maisha yao yote. Mke wa mwangalizi msafiri mmoja, ambaye sasa ni mwenye umri wa zaidi ya miaka 70, alisema: “Ningali nikifaidika kutokana na kielelezo chema cha wazazi wangu Wakristo. Na sala yangu ya bidii ni kwamba nitathibitisha uthamini wangu kamili kwa ajili ya urithi huu kwa kuutumia ifaavyo katika enzi zote zijazo.”