Je! wewe unatumika ukiwa na kusudi?
1 Yehova ndiye Mungu mwenye kusudi. (Isa. 55:10, 11) Tunahimizwa kumwiga yeye. (Efe. 5:1) Hilo bila shaka lingepaswa kuonekana katika namna tunavyotimiza huduma yetu. Kwa hiyo, ulizo hili ni lenye kufaa: “Je! wewe unatumika ukiwa na kusudi?”
2 Kuhubiri kwako toka nyumba hadi nyumba, kutoa ushahidi wa vivi hivi, na ugawaji wa vichapo, yote hayo ni sehemu ya huduma yenye kusudi. Lakini, kumbuka kwamba utume wetu hautii ndani kuhubiri tu bali pia kufanya wanafunzi. (Mt. 28:19, 20) Baada ya kupanda mbegu ya kweli ya Ufalme, tunapaswa kurudia na kuzitia maji, na kutoa utunzaji wa kawaida huku tukitazamia Yehova atokeze ukuzi. (1 Kor. 3:6) Tunapaswa kusukumwa na dhamiri kuhusu kufanya ziara za kurudia na kuanzisha mafunzo ya Biblia.
3 Panua huduma yako: Utajisikia vizuri sikuzote wakati unapoweza kuangalia nyuma kuona kile ulichofanya katika utumishi na kujiambia mwenyewe: “Nimetimiza kile nilichokusudia kufanya.” Kama inavyoandikwa kwenye 2 Timotheo 4:5, Paulo alisihi: “Timiza kikamili huduma yako.” Hilo latia ndani kupanua jitihada zako za kufuatia kupendezwa kote kulikopatikana. Katika programu yako ya utumishi ya kila juma, panga wakati kamili ili kufanya ziara za kurudia. Jitahidi kutimiza mradi wa kuanzisha mafunzo ya Biblia pamoja na wale walio na mwelekeo wenye kufaa. Hilo ndilo lingepaswa kuwa kusudi lako wakati unaposhiriki katika huduma.
4 Uliza wahubiri jinsi walivyojisikia wakati walipoona wanafunzi wao wa Biblia wakibatizwa kwenye kusanyiko. Walishangilia, huenda hata kuliko wale waliobatizwa. Walikuwa wametimiza kusudi tukufu! Mfanya-wanafunzi mmoja alisema jambo hilo kwa maneno haya: “Kufanya wanafunzi kwamaanisha kuwa na wasifaji wengi zaidi wa Yehova. Kwamaanisha uhai kwa wale wanaokubali kweli. Mimi hupenda sana kufundisha wengine kweli—kwapendeza sana! . . . Wengi wa wale ambao wamekuja kumpenda Yehova wamekuwa marafiki niwapendao sana.”
5 Fikiria kuwa na uwezo wa kusaidia mtu kuwa mtumishi aliye wakfu wa Yehova! Ni jambo la kufurahisha kama nini! Tunda kama hilo hutokana na kutumika ukiwa na kusudi katika huduma.—Kol. 4:17.