Je! hatukusikia hilo hapo mbele?
1 Bila shaka tumelisikia! Yehova hurudilia mambo mengi katika Neno lake kwa ajili ya faida ya watu wake. Mara nyingi, Yesu alirudilia mafundisho yake kuhusu pande mbalimbali za Ufalme. Mara kwa mara, mitume wake walirudilia mambo ya kiroho pamoja na wale waliokuwa imara katika kweli.—Rom. 15:15; 2 Pet. 1:12, 13; 3:1, 2.
2 Katika wakati wetu, tengenezo la Yehova limepanga mambo kusudi habari za maana zirudiliwe tena na tena kwenye mikutano ya kutaniko. Vichapo fulani vimechunguzwa kwa kurudia-rudia. Ndiyo, ni jambo la maana kusikia mambo ambayo tulisikia hapo mbele!
3 Kurudilia hutimiza uhitaji wa maana sana: Vikumbusho vya Yehova hufanya uelewevu wetu uwe wenye kina kirefu, hupanua maoni yetu, na hutia nguvu azimio letu la kubaki katika mbio kiroho. (Zab. 119:129) Kurudilia viwango na kanuni za Mungu ni kama kuangalia katika kioo. Huko kunatusaidia kujichunguza wenyewe na kunazuia mwelekeo wa kuwa “msikiaji msahaulifu.”—Yak. 1:22-25.
4 Ikiwa hatuendelei kujikumbusha ile kweli, mambo mengine yatakuwa na uvutano juu ya moyo wetu. Vikumbusho vya Mungu hututia nguvu ili kuzuia uvutano wenye kuharibu wa ulimwengu wa Shetani. (Zab. 119:2, 3, 99, 133; Flp. 3:1) Vikumbusho vya kawaida tunavyopokea kuhusu utimizo wa makusudi ya Mungu hutuchochea ‘tufulize kulinda.’ (Mk. 13:32-37) Kurudilia kweli za Kimaandiko kunatusaidia tubaki kwenye njia iongozayo kwenye uhai udumuo milele.—Zab. 119:144.
5 Jinsi ya kufaidika binafsi: Tunapaswa ‘kuelekeza mioyo yetu kwa shuhuda za Mungu.’ (Zab. 119:36) Wakati habari ambayo tunajua inapaswa kuchunguzwa kwenye mkutano wa kutaniko, tungepaswa kujitayarisha kimbele, kutafuta maandiko yenye kutajwa, na kufikiri juu ya jinsi tunavyoweza kutumia habari hiyo. Acheni tusikose kutayarisha kujikumbusha kwa kuandika katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, tukifikiri kwamba kujikumbusha huko si kwa lazima. (Lk. 8:18) Hatungetaka kamwe kukosa uangalifu ati kwa sababu kweli za msingi hurudiliwa mara kwa mara kwenye mikutano yetu.—Ebr. 5:11.
6 Acheni tushiriki mtazamo wa mtunga-zaburi: “Nimefurahi kwa njia za shuhuda [vikumbusho, NW] zako, sawasawa kwa mali zote.” (Zab. 119:14) Ndiyo, tumesikia mambo hayo ya thamani hapo mbele, na inaelekea tutayasikia tena. Kwa nini? Kwa kuwa Yehova anajua kwamba tunahitaji kuyasikia!