“Lihubiri neno . . . kwa hima”
1 Ikiwa unapokea furushi fulani lenye maandishi “LA HIMA,” wewe utalionaje? Fungu la maneno “–a hima” lamaanisha “-enye kuomba uangalifu wa mara moja.” Kwa sababu nzuri, mtume Paulo aliagiza kwamba tungepaswa “[ku]hubiri neno . . . kwa hima.” (2 Tim. 4:2) Je, wewe unaitikia kwa kutolea kazi hiyo uangalifu wako wa mara moja?
2 Huenda Paulo alipata ripoti kwamba wengine kati ya ndugu zake walikuwa wakionyesha mwelekeo wa ‘kucheza-cheza katika shughuli zao’ wakiwa Wakristo. (Rom. 12:11) Hilo lilipunguza matokeo ya kazi yao na pia shangwe ambayo wangeweza kupata kutokana na kusaidia wengine.
3 Maoni ya Yesu kuhusu huduma: Yesu alipendezwa kama nini na kutimiza huduma yake! Alisema: “Chakula changu ni kwamba mimi nifanye mapenzi yake aliyenituma na kumaliza kazi yake.” Kielelezo cha Yesu kilichochea wanafunzi wake, ambao alitia moyo kwa kuwaambia kwamba ‘mashamba ni meupe kwa ajili ya mavuno.’ (Yn. 4:34, 35) Hisi ya uharaka aliyoonyesha katika huduma yake yote ilikuwa wazi wakati alipoambia wanafunzi wake ‘waombe Bwana-mkubwa wa mavuno atume wafanyakazi katika mavuno yake.’ (Mt. 9:38) Yesu alifahamu kwamba utume wake ulikuwa kuhubiri, naye aliazimia kutoacha kitu chochote kimzuie kufanya hivyo.
4 Namna gani sisi? Kusonga mbele katika kazi ya kuhubiri ni jambo lenye uharaka leo kuliko wakati mwingine wowote. Katika sehemu nyingi za dunia, mashamba ni yenye kukomea kwa ajili ya mavuno. Hata katika mabara ambako inaonekana kana kwamba ushahidi kamili umetolewa, maelfu ni wenye kubatizwa kila mwaka. Mwisho wa mfumo huu wa mambo ukiwa wenye kukaribia kwa haraka, kuna “mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.” (l Kor. 15:58) Sasa kuliko wakati mwingine wowote, ni jambo la maana sana kwamba tujitahidi kwa bidii kushiriki ujumbe wa Ufalme pamoja na wengine.
5 Acheni tujitoe kabisa katika kufikisha habari njema kwa wengine, tukienda kutoka nyumba hadi nyumba na mahali pengine popote watu wanapoweza kupatikana katika eneo. Kwa kushiriki kikamili iwezekanavyo katika kazi ya kuhubiri, tunaonyesha wazi kwamba tumetia Ufalme pa nafasi ya kwanza katika maisha yetu. (Mt. 6:33) Uaminifu wetu katika kuhubiri neno kwa hima utatuletea shangwe kubwa.