“Acheni nuru yenu ing’ae”
1 Ulimwengu unaotuzunguka uko katika giza kiadili na kiroho. Nuru ya kweli inafichua “kazi zisizozaa matunda” za giza kusudi vikwazo hivyo vyenye kuleta kifo viweze kuepukwa. Kwa sababu hiyo, mtume Paulo alisihi Wakristo: “Endeleeni kutembea kama watoto wa nuru.”—Efe. 5:8, 11.
2 “Matunda ya nuru” ni tofauti kabisa na giza ya ulimwengu. (Efe. 5:9) Kuzaa matunda hayo kunaomba tuwe mifano yenye kutokeza katika maisha ya Kikristo, aina ya watu ambao Yesu anakubali. Tunapaswa pia kuonyesha sifa kama vile kuwa na moyo kamili, unyofu, na shauku kuelekea kweli. Matunda hayo yanapaswa kuonyeshwa katika maisha yetu ya kila siku na katika huduma yetu.
3 Tuwe wenye kung’aa kila wakati: Yesu aliambia wanafunzi wake: “Acheni nuru yenu ing’ae mbele ya watu wote.” (Mt. 5:16) Tunamwiga Yesu katika kuonyesha nuru ya Yehova kwa kuhubiri kuhusu Ufalme wa Mungu na makusudi yake. Tunang’aa kama wamulikaji wakati tunapotembelea nyumba za watu na wakati tunapoeneza kweli kazini, shuleni, kati ya majirani zetu, na mahali pengine popote tunapopata nafasi.—Flp. 2:15.
4 Yesu alisema kwamba wengine wangechukia nuru. (Yn. 3:20) Kwa hiyo, hatuvunjwi moyo wakati watu walio wengi wanapokataa kuacha “nuru ya Habari Njema ya utukufu wa Kristo” ing’ae kupitia wao. (2 Kor. 4:4, ZSB) Yehova husoma mioyo ya wanadamu, naye hataki wale wanaojizoeza ukosefu wa uadilifu kati ya watu wake.
5 Wakati tunapofuata njia za Yehova na kufurahia nuru ya kiroho, tunaweza kuonyesha nuru hiyo kwa wengine. Ikiwa wanatambua kupitia mwenendo wetu kwamba sisi ‘tuna nuru ya uhai,’ ndipo wao pia wanaweza kuchochewa kufanya mabadiliko yanayohitajiwa ili kuwa wachukuaji wa nuru.—Yn. 8:12.
6 Kwa kuacha nuru yetu ing’ae, tunaleta sifa kwa Muumba wetu na tunasaidia watu wenye unyofu wamjue yeye na kupata tumaini la uzima wa milele. (1 Pet. 2:12) Kwa kuwa sisi tuna nuru, acheni tutumie nuru hiyo ili kuongoza wengine waone njia ya kutoka katika giza la kiroho na kufanya kazi zilizo za nuru.