“Acheni Nuru Yenu Iangaze”
1. Tuna pendeleo la kufanya nini?
1 Tangu asubuhi mapema jua linapotoka kuchomoza na linapotaka kulala, uzuri wa nuru inayoonekana unamletea Yehova Mungu sifa. Lakini, Yesu aliwaomba wanafunzi wake wawe na nuru ya aina nyingine—“nuru ya uzima.” (Yoh. 8:12) Kuwa na nuru hiyo ya kiroho ni pendeleo la pekee linaloleta madaraka mazito. Yesu alisema: “Acheni nuru yenu iangaze mbele ya watu.” Kwa kufuata shauri hilo tutawafaidi wengine. (Mt. 5:16) Katika giza kubwa la kiroho leo, tunapaswa kuangazia wengine nuru hiyo, na leo watu wengi wana lazima ya nuru hiyo kuliko wakati mwingine wowote! Kama Kristo, namna gani tunaweza kuacha nuru yetu iangaze?
2. Namna gani Yesu alionyesha kwamba ni jambo la maana kuangazia wengine nuru ya kiroho?
2 Kwa Kuhubiria Wengine: Yesu alitumia kila njia, wakati wake, nguvu zake ili kuwaangazia watu nuru ya kweli nyumbani kwao, katika nafasi za watu wengi, kwenye milima—mahali popote ambapo walipatikana. Alijua kwamba kuangazia wengine nuru ya kiroho kutawaletea faida ya kudumu. (Yoh. 12:46) Ili nuru hiyo iwafikie watu wengi zaidi, Yesu alitayarisha wanafunzi wake ili wawe “nuru ya ulimwengu.” (Mt. 5:14) Waliacha nuru yao iangaze kwa kuwatendea mema majirani zao na kuwafundisha kweli za kiroho.
3. Namna gani tunaweza kuonyesha kwamba tunapendezwa kabisa na nuru ya kweli?
3 Watu wa Mungu wanachukua kwa uzito daraka la ‘kuendelea kutembea kama watoto wa nuru,’ na kwa hiyo wanahubiri mahali popote ambapo watu wanaweza kupatikana. (Efe. 5:8) Kusoma Biblia ao vichapo vingine vyenye kutegemea Biblia mahali ambapo watu wanatuona, tunapokuwa kwenye kazi ao wakati wa mapumziko kwenye masomo, kunaweza kututolea nafasi ili kuanzisha mazungumzo ya Biblia. Kwa kufanya hivyo, dada mmoja kijana alianzisha funzo la Biblia na mwanafunzi mwenzake na akatolea wanafunzi wengine vitabu 12!
4. Namna gani mwenendo wetu mzuri unaweza ‘kufanya nuru yetu iangaze’?
4 Kupitia Mwenendo Wetu Mzuri: Nuru yetu inaweza pia kuangaza kupitia mwenendo wetu mzuri kila siku. (Efe. 5:9) Kwenye kazi, kwenye masomo, na kwenye nafasi zingine za watu wote, mara nyingi watu wanatambua mwenendo wetu wa Kikristo na hilo linatutolea nafasi ili kuwajulisha kweli za Biblia. (1 Pet. 2:12) Kwa mfano, mwalimu mmoja wa kike alivutiwa na mwenendo mzuri wa mtoto mwanaume wa miaka 5, na jambo hilo lilimufanya awaite wazazi wa mtoto huyo. Mwalimu huyo alisema hivi: “Sijapata kuona mtoto kama huyu anayetambua waziwazi yaliyo mema na mabaya!” Bila shaka, kazi yetu ya kuhubiri na mwenendo wetu mzuri vinawavuta watu kwenye “nuru ya uzima” na kumletea Mungu wetu sifa.