Acheni sote tutukuze Yehova na Mwana wake
Jinsi wote wanaohudhuria ukumbusho mnamo aprili 8 wanavyoweza kufaidika kikamili zaidi
1 Ni nani wanaopewa utukufu leo? Wale ambao wametimiza mambo yenye kuheshimiwa sana na ulimwengu. Hata hivyo, katika hali zilizo nyingi, matendo yao husahauliwa upesi. Lakini namna gani kuhusu matendo ambayo yanafaidi kwelikweli wanadamu wote? Tutatoa uangalifu wa karibu zaidi kwa lililo kubwa zaidi la matendo hayo tutakapoadhimisha Chakula cha Jioni cha Bwana, mnamo Aprili 8, 2001, baada ya jua kutua.
2 Ni nani anayestahili utukufu wa juu zaidi? Biblia inajibu: “Wewe wastahili, Yehova, . . . kupokea utukufu na heshima na nguvu, kwa sababu uliumba vitu vyote.” (Ufu. 4:11) Akiwa Muumba, Yehova ndiye Mtawala Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu. Kustahili kwake utukufu hakutakwisha kamwe!—1 Tim. 1:17.
3 Yesu Kristo, Mwana wa Mungu, alifanya matendo yenye kustahili, ambayo yataletea wanadamu baraka zisizo na mwisho. Aliiga kikamilifu Baba yake. (Yn. 5:19) Utii wake usio na kasoro, na utumishi wake mwaminifu vilimfanya “astahili kupokea uwezo na utajiri na hekima na nguvu na heshima na utukufu na baraka.” (Ufu. 5:12) Baba yake alimtukuza kwa kumtawaza kuwa Mfalme. (Zab. 2:6-8) Kwa upande wetu, tutakuwa na nafasi ya kutukuza Baba na Mwana tutakapoadhimisha Chakula cha Jioni cha Bwana mnamo Aprili 8, 2001.
4 Jambo la kusikitisha ni kwamba watu wachache katika historia ya kibinadamu ndio wametoa kwa Yehova na kwa Mwana wake utukufu unaostahili. Nyakati nyingine, hata watu wa kale wa Mungu, Waisraeli, walitoa tu utumishi mdogo kwa Yehova. Huo ulikuwa ukosefu wa heshima wa waziwazi. (Mal. 1:6) Heshima yenye kufaa inaomba utii mwaminifu wenye msingi juu ya upendo na juu ya uthamini kuelekea yote ambayo Yehova na Mwana wake wamefanya kwa ajili yetu. Kutoa utukufu na heshima kama hiyo kunamaanisha kwamba tunaonyesha woga wa kimungu na ustahifu, tukifikiria Yehova na Yesu katika njia zetu zote. Kutaniko la Kikristo linajitahidi kufundisha na kusaidia wengine wafanye hivyohivyo.
5 Wakati wa pekee wa kutoa utukufu: Mwadhimisho wa Ukumbusho ndio mkutano wa maana zaidi wa watu wa Yehova kila mwaka. Kila mtu aliye na tamaa ya kutumikia Yehova na kumtukuza anapaswa kuwapo. (Luka 22:19) Tunatazamia kwamba, zaidi ya ile milioni 6 ya Mashahidi wenye kutenda, wale wenye kupendezwa wataongeza hudhurio kufikia zaidi ya milioni 14. Ni nafasi nzuri kama nini ya kumtukuza Baba yetu wa mbinguni! Ingawa mwadhimisho huo unatia mkazo juu ya Yesu, utukufu na heshima vinavyoonyeshwa kwa sababu ya yale aliyotimiza humtukuza Baba aliyemtuma.—Yn. 5:23.
6 Tunaweza kufanya nini ili kutegemeza tukio hilo la pekee? Tunaweza kusaidia wale waliopendezwa karibuni wafaidike kikamili. Wahimize wahudhurie, na mahali ambapo inahitajiwa, toa msaada kwa wema ili kuwasaidia wafike mahali hapo. Eleza kusudi la hotuba. Watambulishe kwa wengine. Yale wanayoona na kusikia yanaweza kuwachochea watafute kujiunga nasi katika kumtukuza Yehova.
7 Msidharau uvutano ambao programu hiyo inaweza kuwa nao. Mwanafunzi mmoja wa chuo kikuu aliitikia ifuatavyo: “Nimehudhuria mara nyingi Upokeaji wa Ukaristia katika kanisa langu, lakini huu ni tofauti kabisa. Ninaona kwamba huu ni kama vile tu Biblia inavyosema, na ninafikiri nyinyi mnayo kweli.” Akaanza kuhudhuria mikutano kikawaida, naye akabatizwa upesi.
8 Saidieni wapya wafanye maendeleo: Iweni waangalifu kuhusu wapya wanaohudhuria Ukumbusho, na mwatembelee upesi ili kuchunguza pamoja nao mambo yenye kuburudisha waliyojifunza na kuona. Wajulisheni kuhusu mikutano mingine, ambako wanaweza kuongeza ujuzi wao wa Biblia. Kuchunguza sura ya 17 ya kitabu Ujuzi, “Pata Usalama Miongoni mwa Watu wa Mungu,” kutawaonyesha aina mbalimbali za maandalizi ya kiroho yanayotolewa na kutaniko, maandalizi ambayo yanapatikana kwao kwa utayari. Chukueni mipango ili watazame vidio Our Whole Association of Brothers [Toute la communauté de nos frères] kusudi waone na macho yao wenyewe umoja, shangwe, na bidii ya watu wa Yehova!
9 Ni jambo la maana kwamba wale wenye kupendezwa wajifunze jinsi wanavyoweza kibinafsi kuonyesha heshima na utukufu kwa Yehova. Eleza kwamba sala yenye kutoka moyoni inampendeza Yehova na kwamba hiyo ni chanzo cha kila wakati cha burudisho la kiroho. (1 Yn. 5:14) Kwa kutumia masomo ya 8 mpaka 12 katika broshua Anataka, eleza aina ya mwenendo inayomtukuza Yehova. Kwa kuzungumzia yale yanayosemwa katika broshua Mashahidi wa Yehova, kurasa za 30-1, tieni wapya moyo wafikiri kuhusu uwezekano wa kumtukuza Yehova kwa kushiriki kibinafsi katika kazi ya kuhubiri.
10 Uthamini kuelekea dhabihu ya Yesu na kuelekea pendeleo letu la kutumikia tukiwa wanafunzi wake humtukuza Baba, nao huleta baraka kwa wengine. Yesu aliahidi: “Ikiwa yeyote angenihudumia mimi, Baba atamheshimu yeye.”—Yn. 12:26.