“Ninaweza Kupata Wakati Wapi?”
1 Hilo ndilo lalamiko la wengi wetu, kwa kuwa maisha yetu yanajaa utendaji mbalimbali. Imesemwa kwamba wakati ndiyo mali yetu yenye thamani zaidi na yenye kupita haraka zaidi. Kwa hiyo, tunaweza kupata wakati wapi kwa ajili ya mambo yaliyo ya maana kwelikweli, kama vile kusoma na kujifunza Neno la Mungu?—Flp. 1:10.
2 Ufunguo si kutafuta kupata wakati zaidi, lakini kuamua mambo ya kufanya katika wakati tulio nao. Sisi sote tuna saa 168 kwa juma; huenda tukapitisha 100 ya saa hizo tukilala usingizi au tukifanya kazi. Hivyo, tunawezaje kutumia saa zile zenye kubaki kwa njia yenye kutufaidi zaidi? Andiko la Waefeso 5:15-17 linatushauri tutembee “si kama wasio na hekima bali kama watu wenye hekima, [tu]kijinunulia kabisa wakati unaofaa, [na] kufahamu mapenzi ya Yehova ni nini.” Hilo linaonyesha uhitaji wa kutumia kikamili kila nafasi inayojitokeza ili kufanya mambo ambayo Yehova anasema ni ya maana sana.
3 Yesu alilinganisha siku zetu na zile za Noa. (Luka 17:26, 27) Katika siku hizo, watu walijishughulisha na mambo ya kila siku ya maisha. Lakini, Noa alipata wakati wa kujenga safina kubwa na kuhubiri. (Ebr. 11:7; 2 Pet. 2:5) Namna gani? Kwa kutia mapenzi ya Mungu pa nafasi ya kwanza na kumtii yeye kwa kufanya mambo “sawasawa.”—Mwa. 6:22.
4 Ni Nini Kinachopaswa Kuchukua Nafasi ya Kwanza? Yesu alisema: “Binadamu lazima aishi, si kwa mkate pekee, bali kwa kila tamko linalokuja kupitia kinywa cha Yehova.” (Mt. 4:4) Kila juma, tunapokea ‘kipimo cha chakula cha kiroho kwenye wakati wenye kufaa.’ (Luka 12:42) Hilo linaomba programu ya kawaida na ya kibinafsi ya usomaji na funzo ili kuweka akilini chakula hicho chote na kufaidika kwelikweli. Tukiwa wenye shukrani kuhusu chakula cha kiroho, hatukioni kuwa chakula cha kuliwa haraka-haraka, cha kuchunguzwa kijuujuu kama vile mtu anavyoweza kula chakula cha kimwili haraka-haraka. Badala yake, uthamini wenye kufaa hutuchochea tuchukue wakati wa kujifunza na kufurahia mambo ya kiroho.
5 Kutwaa chakula cha kiroho kunaweza kuongoza kwenye uzima wa milele. (Yn. 17:3) Jambo hilo linastahili nafasi ya kwanza katika programu yetu ya kila siku. Je, tunaweza kupata wakati kwa ajili ya kusoma Biblia kila siku na kujitayarisha kwa ajili ya mikutano ya Kikristo? Ndiyo. Ikiwa tunafanya hivyo, tutapokea ‘thawabu nyingi’ inayotokana na kujua na kufanya mapenzi ya Mungu.—Zab. 19:7-11.