Tutavuna Kulingana na Jitihada Zetu Binafsi
1 Yehova Mungu ameonyesha upendo wake kuelekea wanadamu katika njia nyingi. Yesu alikazia upendo wa Mungu wenye kuzidi, akionyesha mkutano wa watu waliokusanyika kwamba Mungu “hufanya jua lake lichomoze juu ya watu waovu na wema na kufanya mvua inyeshe juu ya watu waadilifu na wasio waadilifu.” (Mt. 5:43-48) Kwenye pindi nyingine, Yesu alitambulisha wonyesho mkubwa zaidi wa upendo wa Baba yake—dhabihu ya Mwana wake mzaliwa-pekee, ambaye Mungu alitoa kwa ajili ya wokovu wetu. (Yn. 3:16) Yesu alitia wasikilizaji wake moyo waitikie kwa uthamini upendo wa Yehova. Je, sisi tunajitahidi kufanya hivyo?
2 Ili tuonyeshe uthamini kamili na kupata faida zenye kudumu kutokana na upendo wa Yehova, tunapaswa kumjua yeye. (Yn. 17:3) Tunahitaji shauri na mwongozo kuhusu jinsi tunavyoweza kumtumikia kwa njia yenye kukubalika. Yehova ameonyesha hangaiko lake lenye upendo kwa kututolea Neno lake lililopuliziwa, Biblia, na kwa kutokeza tengenezo lake zuri ajabu, ambalo kupitia hilo tunapokea shauri na maagizo. (Mt. 24:45-47; 2 Tim. 3:16, 17) Tukiwa watu wa Yehova waliojiweka wakfu, tumefundishwa katika njia zake. Lakini, je, tunaonyesha kupitia jitihada yetu binafsi kwamba tunathamini upendo wa Yehova? Je, tunasikiliza shauri lake ili kuwa wenye kumpendeza na kwa njia hiyo kujifaidi wenyewe? (Isa. 48:17; Yak. 1:22) Mtume Paulo aliandika kwenye 1 Wakorintho 3:8: “Basi yeye apandaye na yeye atiaye maji ni mmoja, lakini kila mtu atapokea thawabu yake mwenyewe kulingana na kazi yake mwenyewe yenye jasho.”
3 Ndiyo, tunapaswa kujitahidi kufanya yale ambayo Mungu anataka tufanye. Watu wote hawafanyi maendeleo ya kiroho kwa mwendo uleule. Kuna mambo mengi yanayoweza kuwa na uvutano juu ya maendeleo yetu, na lingekuwa jambo lisilo la hekima kufanya malinganisho yenye kuvunja moyo. Hata hivyo, jitihada tunayofanya kibinafsi ni ya maana sana. Tunaweza kufanya nini ili kukaribia zaidi tengenezo? Je, kuna sehemu ambazo tunaweza kufanyia maendeleo katika kukubali madaraka yetu binafsi tukiwa Wakristo? Ni jitihada gani itakayohitajiwa ili kutoa utegemezo bora zaidi kwa utendaji mbalimbali wa kutaniko? Je, kuna nukta tunazohitaji kutumikisha kuhusiana na maagizo tunayopewa na tengenezo?—1 Tim. 4:16.
4 Iga Wale Walio Waaminifu: Kwa makumi ya miaka, habari njema ya Ufalme imehubiriwa na akina ndugu na dada waaminifu. Waaminifu hao, kama vile Paulo, wanastahili kuigwa. (1 Kor. 11:1) Wameitikia upendo wa Mungu, nao wamepata faida nyingi kwa sababu ya kazi yao ngumu na jitihada zao binafsi za kufuata shauri la Biblia. Wanafanyiza kiini chenye nguvu cha wafanyakazi wenye kutenda katika kutaniko; hawaepi daraka lao binafsi. Tunaweza kuona matunda ya kazi za jasho za kila mmoja wao.—Rom. 1:13; 2 Kor. 3:1-3.
5 Sasa, mamia ya maelfu ya wapya wanamiminika kwenye tengenezo kila mwaka. (Isa. 60:8) Wao pia ni wenye kuchukua mambo kwa uzito kuhusu kufanya jitihada ili kuwa watu wa kiroho wenye kukomaa kabisa, na bidii yao katika huduma ya shambani inastahili sifa. Wanafaidika kwa kuona jinsi Yehova anavyobariki wale wanaofanya kazi sana katika utumishi wake. Mfano wa ndugu na dada wakomavu husaidia wapya waone kwamba huu si wakati wa kulegeza mikono au kusimamisha utumishi wetu kwa Mungu. Iwe kwamba sisi ni wapya au wahubiri wenye uzoefu, je, tunaendelea kukomaa kiroho, tukikubali madaraka yetu binafsi ya Kikristo na kufaidika na maandalizi yote ya kitheokrasi?
6 Tutumikishe Yale Tunayojifunza: Muda mrefu kabla ya Yakobo kuandika kwamba tunapaswa kuwa ‘watendaji wa kazi,’ Musa aliambia Wayahudi: ‘Mnapaswa kutumikisha maneno haya.’ (Yak. 1:25; Kum. 11:18, NW) Kwa hiyo, ujuzi peke yake haukutosha. Wayahudi walihitaji kutii Yehova kwa kutumikisha maneno ya Sheria. Kanuni hiyo ya msingi inabaki isiyobadilika. Yesu, Mwana wa Mungu, bila shaka alijua umaana wa utii. (Yn. 8:28) Alisema kwenye Mathayo 7:24: “Kila mtu asikiaye semi zangu hizi na kuzifanya atafananishwa na mtu mwenye busara.”
7 Je, tunatumikisha yale tunayojifunza kwenye makusanyiko ya mzunguko? Je, tunafahamu kwa nini ni jambo la maana sana wakati huu kubaki macho na kulinda akili zetu? Je, tuko macho ili kutambua mashambulio ya ujanja na mitego ya Ibilisi? Je, tunathamini shauri na maonyo ambayo tengenezo linatutolea kwa kurudilia-rudilia kuhusu uhitaji wa kuwa safi kiadili na kiroho katika kutaniko? Ni kwa kiasi gani sisi binafsi tunatumikisha yale tunayosikia?—Yak. 1:23-25.
8 Kichwa cha programu ya kusanyiko la pekee la siku moja mnamo mwaka mpya wa utumishi kina msingi wa Kimaandiko wenye nguvu: “Jitiisheni Wenyewe kwa Mungu—Mpingeni Ibilisi.” (Yak. 4:7) Huo ni mwongozo wenye kufaa nyakati hizi ngumu! Kutii kwetu amri za Mungu kunatufanya tupambane moja kwa moja na Shetani. Programu hiyo itatufundisha jinsi ya kupinga mipango miovu ya Ibilisi yenye kuharibu imani. (Ebr. 2:1) Tunapofanya hivyo, tutavuna baraka kulingana na jitihada zetu binafsi.
9 Faidika na Funzo la Kibinafsi: Funzo la kibinafsi hutusaidia kujenga imani yenye nguvu, nalo hufanya uthamini wetu kuelekea kweli uwe wenye kina kirefu zaidi. Hilo hutupatia uhakika na hututayarisha ili kusema kwa mamlaka. Linatutolea utambuzi na ufahamu wenye kina kirefu, nalo linatusaidia kuvaa utu mpya. (Kol. 1:9-11) Lakini, funzo lenye kuzaa matunda huomba wakati na jitihada, na hakuna njia fupi zaidi ya kupata ujuzi sahihi na kina cha kiroho. Faida tutakazopata kutokana na funzo hutegemea wakati na jitihada tulizofanya kwa kusudi hilo.—2 Kor. 9:6, 7; Gal. 6:7.
10 Je, tunapanga wakati wa kutosha kila juma ili kutayarisha mikutano ya kutaniko? Hiyo ni njia moja ambayo kwa hiyo tunaweza kuonyesha kwamba tunathamini chakula cha kiroho ambacho Yehova hutoa kupitia mtumwa mwaminifu na mwenye busara. Kutayarisha mikutano ifaavyo hutusaidia tushikamane na programu ya usomaji na ya funzo la Neno la Mungu. Je, kila juma tunapanga wakati wa kufanya usomaji wetu wa Biblia kama unavyopangwa katika programu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi? Inaomba dakika chache tu kila siku ili kusoma na kutafakari juu ya habari hiyo. Mkutano wa Utumishi hutusaidia tuendelee kuwa macho ili kutambua njia ambazo katika hizo tunaweza kufanya huduma yetu ya peupe iwe yenye matokeo. Je, tunajitayarisha, tukifikiria kipekee jinsi tunavyoweza kutumia habari hiyo katika huduma? Na je, tunafanya jitihada ya kuitumia papo hapo? Mipango kamili inapaswa kuchukuliwa ili kutayarisha Funzo la Mnara wa Mlinzi na Funzo la Kitabu. Je, tunafanya hivyo?
11 Shiriki Katika Mikutano: Tunaweza kufaidika zaidi na mikutano wakati tunapoishiriki. Kutayarisha mikutano na baadaye kujitahidi kushiriki kunatufanya tuendelee kuwa waangalifu wakati wa mikutano hiyo na kunafanya iwe vyepesi zaidi kwetu kufaidika na maelezo ya wengine. Wengi wangali wakikumbuka jitihada waliyofanya ili kutoa maelezo yao ya kwanza kwenye mkutano au hotuba yao ya kwanza ya mwanafunzi kwenye Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Ingawa wasiwasi inapaswa kuwa imepunguka kwa kiasi kikubwa, je, tunaendelea kujitahidi ili kufanya maendeleo yetu yawe wazi kwa wote? (1 Tim. 4:15) Maelezo yetu hufaidi na hutia wengine moyo. Ikiwa tumejitayarisha vema kwa kujifunza habari itakayozungumziwa kwenye mikutano, kushiriki kwetu mikutano kwa njia yenye maana kutachochea wengine kwenye upendo na kazi zilizo bora.—Ebr. 10:23-25.
12 Maelezo yetu hayapaswi kuwa marefu na magumu kueleweka. Kwa kawaida, ni vizuri zaidi kutoa maelezo mafupi yenye kujibu moja kwa moja maulizo yanayoulizwa au maelezo yenye kusaidia kufanya matumizi ya andiko yawe wazi. Ikiwa tumejitayarisha vema, tutakuwa na uwezo wa kutoa maelezo katika maneno yetu wenyewe. Tunapofanya hivyo, faida kwetu wenyewe na kwa wengine zitakuwa kubwa zaidi. Kwa nini? Kwa kuwa jambo hilo linaomba tufikiri juu ya yale tunayosema na kueleza nukta kadiri tunavyoisikia. Hilo linaweza kufanya iwe rahisi zaidi kwa wengine kusikia habari. Pia, litatusaidia tukumbuke habari hiyo ili kuitumia kwenye pindi nyingine.
13 Panda kwa Wingi Shambani: Huduma yetu ya Kikristo ni hazina ya utumishi. (2 Kor. 4:7) Je, wewe unaiona hivyo? Kupitia huduma, tunalo pendeleo la kuonyesha imani yetu kwa wengine. Yesu alisema kwamba katika wingi wa moyo kinywa husema. (Luka 6:45) Jitihada ya kibinafsi tunayofanya ili kushiriki kikamili katika huduma ya shambani hutuwezesha kuvuna faida nyingi. Uelewevu wetu kuhusu kweli hukomaa zaidi, nasi husitawisha uwezo mkubwa zaidi wa kutumia Biblia. Tunayo furaha ya kupeleka kweli kwa wengine na kuwasaidia wajifunze kuhusu Muumba wao Mtukufu. Tunasimama tukiwa mashahidi wanaotetea haki ya utawala wa Mungu na enzi yake kuu. Sisi ni wenye furaha kwa kuwa tunajua kwamba tunampendeza Yehova, tukiwa tumefanywa upya katika ufanani wake na tukifanya mapenzi yake.—Mt. 5:48.
14 Ikiwa tunaendelea kupima jitihada yetu binafsi, ibada yetu kwa Yehova haitakuwa kamwe utumishi wa juujuu tu. Hilo linamaanisha nini? Linamaanisha kwamba hatutakuwa na moyo usio kamili katika kujipatanisha na mapenzi ya Mungu, tukifanya tu ionekane kana kwamba tunatoa utumishi kwake au tukitoa kiasi kidogo zaidi bila ujitoaji na jitihada zenye kutoka moyoni. Utumishi wetu kwa Yehova unapaswa kutolewa kwa moyo wote. Tunao wajibu wa Kimaandiko wa kutoa yote tuliyo nayo katika utumishi wake. (Kol. 3:23, 24) Ni kweli kwamba hali zinatofautiana, na Yehova hatuombi zaidi ya kile tunachoweza kufanya. Hata hivyo, yale tunayoweza kufanya, yeye anatutazamia tuyafanye! (Mt. 22:37) Kwa kuwa hali ya kibinadamu isiyokamilika ina mwelekeo wa kutojitoa kikamili, ni vizuri tujichunguze wakati kwa wakati ili kuona mahali ambapo tunaweza kufanyia maendeleo katika utumishi wetu kwa Mungu. Je, tuna zoea la kufanya hivyo?
15 Tunapaswa kuwa waangalifu ikiwa hatutaki kuruhusu mambo ya kibinafsi tunayofuatia na tamaa zetu wenyewe zituzuie tusitoe kilicho bora tulicho nacho katika utumishi wa Yehova. Raha, shughuli za kujifurahisha, na utendaji wa kujiburudisha vinapaswa kulindwa mahali pavyo. Pia, tunapaswa kujilinda tusiwe na mwelekeo wa kushughulikia kazi za kimwili kupita kiasi. Tukifuata shauri la Yesu kwenye Mathayo 6:22, 23, bila shaka tutaweza kufanya jitihada zaidi katika kufuatia faida za kiroho na kuvuna kulingana na jitihada hiyo.
16 Tunapoendelea kujitahidi kuvaa utu mpya, tutakubali daraka letu wenyewe katika kutumikisha shauri na mapendekezo tunayopokea kwenye mikutano ya kutaniko, makusanyiko, mikusanyiko, na kupitia vichapo. Acheni kila mmoja wetu ajifunze kwa bidii, atende kwa kushiriki katika mikutano, na ashiriki katika kazi hii kubwa ya kufanya wanafunzi kulingana na jinsi hali zetu binafsi zitakavyoruhusu. Kwa kuitikia hivyo upendo wa Mungu kwa uthamini, tunaweza kuwa hakika kwamba tutavuna thawabu nyingi za kiroho sasa na kudumisha tumaini lenye nguvu la uzima wa milele katika ulimwengu mpya wa Yehova.