Tumia Sawasawa Neno la Mungu
1 Alipotoa ushahidi kwa ofisa mmoja, “Filipo akafungua kinywa chake na, akianza na Andiko [fulani], akamtangazia habari njema juu ya Yesu.” (Mdo. 8:35) Filipo alikuwa ‘akilitumia sawasawa neno la ile kweli.’ (2 Tim. 2:15) Lakini leo, waangalizi wasafiri wametambua kwamba wahubiri wengi hutumia Biblia mara chache wanapotoa ushahidi. Je, unatumia Biblia katika huduma yako?
2 Neno la Mungu ndicho chanzo cha kila jambo tunaloamini na kufundisha. (2 Tim. 3:16, 17) Hilo ndilo huvuta watu kwa Yehova na kuwafundisha ili wapate uzima. Kwa sababu hiyo, ni jambo la maana tutumie Biblia katika huduma yetu badala ya kuzungumza tu kuhusu habari zinazotupendeza sisi. (Ebr. 4:12) Kwa kuwa watu wengi hawajui mengi kuhusu Biblia, tunapaswa kusoma kutoka katika hiyo ili kuwaonyesha mwongozo wenye kufaa ambao inatoa na wakati ujao ambao inatolea wanadamu.
3 Soma Moja kwa Moja Kutoka Katika Biblia: Unaweza kujaribu kwenda kuhubiri bila mfuko wa vitabu. Unaweza kutia vichapo unavyotaka kutolea watu katika jalada nyepesi na kuchukua Biblia mkononi au katika mfuko wa vazi. Kisha, unapohusisha mtu fulani katika mazungumzo, unaweza kutoa Biblia kutoka mfukoni bila kufanya mtu huyo afikiri kwamba unajaribu kumtolea hotuba. Jiweke mahali ambapo patawezesha msikilizaji wako afuate usomaji katika Biblia yako. Labda mwombe asome andiko fulani kwa sauti kubwa. Msikilizaji atavutwa kwa kina kirefu zaidi wakati anapoweza kuona yale ambayo Biblia inasema badala ya kusikia tu mambo hayo kutoka kwako. Bila shaka, ili kumsaidia aelewe jambo linalozungumziwa katika andiko, kazia maneno yenye kutoa mawazo makuu.
4 Utoaji Wenye Kukazia Andiko Moja: Baada ya kujitambulisha, unaweza kusema: “Watu huendea vyanzo vingi ili kupata mwelekezo katika maisha yao. Ni nini unalofikiri kuwa chanzo bora zaidi cha uongozi wenye kufaa? [Acha mtu ajibu.] Unafikiri nini kuhusu maneno haya? [Soma Mezali 2:6, 7, na uache mtu ajibu.] Hekima ya kibinadamu imeonekana kwa njia yenye kusikitisha kuwa yenye kupungukiwa, ikiongoza watu wengi kwenye kukata tumaini. Lakini, hekima ya Mungu imeonekana sikuzote kuwa yenye kutegemeka na yenye mafaa.” Kisha, onyesha kichapo unachokipendekeza, na ukazie kutoka kichapo hicho mfano mmoja wa hekima ya Mungu yenye kufaa.
5 Yesu alitumia Maandiko ili kusaidia watu wenye mioyo minyofu. (Luka 24:32) Paulo alihakikisha Kimaandiko mambo aliyofundisha. (Mdo. 17:2, 3) Uhakika wetu na furaha yetu katika huduma vitaongezeka kadiri tunavyokuwa mafundi zaidi na zaidi katika kutumia sawasawa Neno la Mungu.