Watchtower—MAKTABA KU ENTERNETE
Watchtower
MAKTABA KU ENTERNETE
Kiswahili (Congo)
  • BIBLIA
  • VICHAPO
  • MIKUTANO
  • km 2/02 uku. 3-6
  • ‘Hubiri Neno la Mungu Kikamili’

Hakuna video juu ya habari yenye umechagua.

Pole, kulikuwa kosa fulani wakati video ilikuwa inajaribu kusoma.

  • ‘Hubiri Neno la Mungu Kikamili’
  • Huduma Yetu ya Ufalme—2002
  • Habari za Kufanana na Zile
  • ‘Toa Ushahidi Kamili Kuhusu Habari Njema’
    Huduma Yetu ya Ufalme—2008
  • Je! Tutafanya Hilo Tena?
    Huduma Yetu ya Ufalme—1998
  • Endeleeni Kutangaza Kazi za Ajabu za Yehova
    Huduma Yetu ya Ufalme—2004
  • Tutafute Mapainia Wasaidizi 100,000
    Huduma Yetu ya Ufalme—1997
Ona Habari Zaidi
Huduma Yetu ya Ufalme—2002
km 2/02 uku. 3-6

‘Hubiri Neno la Mungu Kikamili’

1 Unapothamini kwa unyofu kupokea kitu fulani kizuri, unaonyesha hilo kupitia mtazamo wako na matendo yako, sivyo? Bila shaka! Kuhusiana na wema na fadhili-upendo ambazo Yehova anaonyesha kwa wanadamu, ona jinsi mtume Paulo alivyoitikia. Alisema kwa mkazo: “Shukrani ziwe kwa Mungu kwa ajili ya zawadi yake ya bure isiyoelezeka”! Hiyo ‘zawadi ya bure’ inatia ndani nini? Jumla ya “fadhili isiyostahiliwa ya Mungu izidiyo” ambayo tumeonyeshwa. Wonyesho mkubwa zaidi wa fadhili hiyo isiyostahiliwa ni ile zawadi ya Mwana wake mwenyewe kuwa ukombozi kwa ajili ya dhambi zetu.​—2 Kor. 9:​14, 15; Yn. 3:​16.

2 Je, wonyesho wa shukrani wa Paulo ulikuwa wa maneno tu? Hata kidogo! Alionyesha uthamini wake wenye kina kirefu kwa njia nyingi. Alihangaikia sana hali njema ya kiroho ya Wakristo wenzake, naye alitaka kufanya aliyoweza ili kuwasaidia wafaidike kikamili na fadhili-upendo za Mungu. Kuhusu hao, Paulo alisema: “Tukiwa na shauku nyororo kwa ajili yenu, tulipendezwa vema kuwapa nyinyi, si habari njema ya Mungu tu, bali pia nafsi zetu wenyewe, kwa sababu mlipata kuwa wapendwa kwetu.” (1 Thes. 2:8) Zaidi ya kusaidia wale ambao tayari walikuwa sehemu ya kutaniko wapate wokovu, Paulo alihubiri habari njema bila kuchoka, akisafiri maelfu ya kilometa kwenye nchi kavu na kwenye bahari ili kupata wale “waliokuwa na mwelekeo ufaao kwa ajili ya uhai udumuo milele.” (Mdo. 13:​48) Uthamini wenye kina kirefu wa Paulo kuhusu yote ambayo Yehova alikuwa amefanya kwa ajili yake ulimchochea “kulihubiri neno la Mungu kikamili.”​—Kol. 1:​25.

3 Je, uthamini wetu kuhusu yote ambayo Yehova amefanya kwa ajili yetu hautuchochei tutoe msaada wa kiroho kwa wale wanaouhitaji katika kutaniko letu? (Gal. 6:​10) Na je, hatuchochewi kushiriki kikamili zaidi iwezekanavyo katika kuhubiri habari njema ya Ufalme kotekote katika eneo letu?​—Mt. 24:14.

4 Nafasi ya Kuonyesha Uthamini: Kila mwaka, Ukumbusho wa kifo cha Kristo unatutolea nafasi ya pekee ya kuonyesha uthamini kuhusu yale ambayo Yehova na Yesu wamefanya kwa ajili yetu. Huo si mkutano ulio tofauti tu au ukumbusho wa tukio fulani tu. Yesu alisema: “Fulizeni kufanya hili katika ukumbuko wangu.” (Luka 22:​19) Ukumbusho wa kifo cha Kristo ni wakati wa kutafakari juu ya utu wa Yesu. Ni wakati wa kutambua kwamba yeye yuko hai na ni mwenye kutenda leo, akiwa na utukufu na ufalme ambao amepewa kwa sababu ya maisha yake ya uaminifu na dhabihu yake. Mwadhimisho huo ni nafasi pia ya kuonyesha ujitiisho wetu kwa ukichwa wa Kristo kadiri anavyoelekeza mambo na utendaji mbalimbali wa kutaniko la Kikristo. (Kol. 1:​17-​20) Kwa heshima, watu wote wa Mungu wanapaswa kuwako ili kuadhimisha Ukumbusho wa kifo cha Kristo. Mwaka huu, Ukumbusho utafanywa Siku ya Nne, Machi 28, 2002, baada ya jua kutua.

5 Kwa sababu ya jitihada yenye bidii iliyofanywa kabla ya mwadhimisho wa Ukumbusho mwaka uliopita, tulipata hudhurio la juu zaidi kuliko wakati mwingine wowote​—watu 592,292 katika Congo-Kinshasa na 20,258 katika Congo-Brazzaville. Hudhurio litakuwa la watu wangapi mwaka huu? Mengi yatategemea “kufanya kazi kwa bidii na kujikakamua [kwetu] wenyewe” ili kusaidia wengi zaidi iwezekanavyo wahudhurie.​—1 Tim. 4:​10.

6 Zaidi ya kuhudhuria Chakula cha Jioni cha Bwana, huenda tukawa na uwezo wa kuongeza utendaji wetu katika utumishi wa shambani. Bila shaka, makumi ya maelfu ya ndugu na dada watakuwa mapainia wasaidizi mwezi mmoja au zaidi. Kila mwaka mnamo miaka mitano iliyopita, tumekuwa na wastani wa mapainia wasaidizi 14,458 katika majira ya Ukumbusho, kuanzia Machi mpaka Mei. Je, unaweza kupanga mambo yako ili kufurahia pendeleo la kuwa painia msaidizi mwaka huu? Hiyo itakuwa njia bora ya kuonyesha uthamini wako wenye unyofu kuhusu uandalizi wenye upendo wa dhabihu ya Kristo uliofanywa na Mungu. Unaweza kuwa hakika na baraka ya Yehova, kama vile mambo yafuatayo yaliyoonwa yanavyoonyesha.

7 Dada mmoja aliye na kazi ya kimwili ya wakati wote aliandika kuhusu jambo alilojionea alipokuwa painia msaidizi mnamo mwezi wa Machi uliopita: “Huduma Yetu ya Ufalme ya Februari 2001 ilitia moyo kila mtu ambaye hali zake ziliruhusu kuwa painia msaidizi katika majira ya Ukumbusho. Kwa kuwa mwezi wa Machi ulikuwa na Siku za Posho tano, jambo hilo lilipatana vema na programu yangu. Kwa hiyo, nikaamua kutoa ombi langu.” Alipoanza mwezi, alijiwekea mradi wa kujaribu kuanzisha funzo la Biblia la nyumbani. Je, alifanikiwa? Ndiyo, katika saa yake ya 52 ya kutoa ushahidi mwezi huo! Alikata maneno kwa kusema: “Kuna baraka nzuri ajabu wakati tunapofanya jitihada ya ziada.”

8 Kuna faida gani kwa familia inayopainia pamoja? Familia moja ya washiriki wanne waliopainia mnamo mwezi wa Aprili uliopita waliona huo kuwa mwezi watakaoukumbuka sikuzote. Mama alisema: “Ni mtazamo wenye furaha kama nini tuliokuwa nao kila siku, kwa kuwa tuliungana katika huduma! Mazungumzo kuhusu utendaji wetu wa siku katika utumishi yalifanya wakati wa mlo wa mchana uwe wenye kufurahisha.” Mwana alisema: “Nilifurahia kutumika na Baba katika utumishi wa shambani katika juma, wakati ambapo kwa kawaida yeye huwa mwenye kufanya kazi ya kimwili.” Baba aliongeza: “Nikiwa kichwa cha familia, nilijisikia mwenye kutosheka kwa kujua kwamba tulitumika pamoja katika kazi iliyo ya maana zaidi kwa wakati wetu.” Je, familia yako inaweza kupainia pamoja? Kwa nini msizungumze katika familia na kuona ikiwa inawezekana kwa nyumba yenu yote kuwa mapainia wasaidizi katika majira haya ya Ukumbusho?

9 Je, Tunaweza Kufanya Machi Kuwa Mwezi Wetu Bora Zaidi? Mapema mnamo mwaka wa 2000, Huduma Yetu ya Ufalme iliuliza ulizo hili: “Je, Tunaweza Kufanya Aprili 2000 Kuwa Mwezi Wetu Bora Kuliko Yote?” Itikio lilikuwa nini? Vilele mbalimbali vilifikiwa. Kulikuwa kilele cha mwezi mmoja cha mapainia wasaidizi 7,964. Kwa kuongezea, tulipata vilele vipya vya saa, magazeti waliyoachiwa watu, na ziara za kurudia. Je, unakumbuka shauku iliyotokezwa na ule utendaji mwingi wa kiroho katika kutaniko lenu mnamo mwezi huo wa pekee? Je, tunaweza kutimiza mambo yenye kuwa sawa au hata yenye kupita mwaka huu? Kupitia jitihada za wote pamoja, Machi 2002 unaweza kuwa “Mwezi Wetu Ulio Bora Zaidi.” Kwa nini Machi?

10 Kuna sababu mbili zinazopaswa kufanya Machi uwe mwezi wa pekee wa utendaji. Kwanza, Ukumbusho utafanywa karibu na mwisho wa Machi, ukitutolea nafasi ya kutosha mapema katika mwezi ili kualika watu wengi zaidi iwezekanavyo wahudhurie. Pili, mwaka huu, mwezi wa Machi una miisho-juma mitano kamili, jambo linalofanya iwe vyepesi zaidi kuwa painia msaidizi kwa wale wanaofanya kazi ya kimwili au wanaoenda shuleni. Kwa nini usiketi sasa na kupanga programu inayoweza kutumika, ukitumia kalenda inayotolewa katika nyongeza hii? Upainia msaidizi unaweza kuwa mwepesi zaidi kuliko unavyofikiri. Kwa mfano, kwa kupanga saa 8 za utumishi wa shambani kila mmoja wa ile miisho-juma mitano, utahitaji kupanga tu saa 10 za ziada katika sehemu yenye kubaki ya mwezi ili kufikia zile saa 50 zinazoombwa.

11 Wazee wanaweza kufanya nini ili kusaidia wote katika kutaniko “kulihubiri neno la Mungu kikamili”? Sitawisheni shauku ya akina ndugu kupitia sehemu za mikutano na mazungumzo ya kibinafsi. Waangalizi wa Mafunzo ya Kitabu ya Kutaniko na wasaidizi wao wanaweza kuchukua hatua ili kuongea na kila mshiriki wa kikundi chao na kumtolea msaada wa kibinafsi. Maneno machache mema yenye kutia moyo au mashauri fulani tu yenye kufaa huenda yakatosha. (Mez. 25:​11) Wengi wataona kwamba kwa kufanya marekebisho madogo katika programu yao, wanaweza kufurahia pendeleo la kutumikia wakiwa mapainia wasaidizi. Katika makutaniko fulani, wazee na watumishi wa huduma wengi, ikiwa si wote, na wake zao walitoa mfano mzuri kwa kuwa mapainia wasaidizi pamoja mnamo majira ya Ukumbusho. Hilo lilitia moyo wahubiri wengi waungane nao. Kwa sababu ya vizuizi vya kimwili au hali nyinginezo, huenda wahubiri fulani wasiwe na uwezo wa kupainia, lakini wanaweza kutiwa moyo waonyeshe uthamini wao kwa kufanya yote wawezayo katika huduma pamoja na wengine katika kutaniko.

12 Mafanikio yanategemea kupanga mambo kwa uangalifu kwa upande wa wazee. Mikutano kwa ajili ya utumishi wa shambani inapaswa kupangwa pa wakati wenye kufaa katika juma lote. Ikiwa inawezekana, mwangalizi wa utumishi atatoa mgawo kimbele kwa akina ndugu wenye sifa ili waongoze mikutano yote kwa ajili ya utumishi. Matayarisho mema yatahitajiwa ili mikutano hiyo isizidi dakika 10 mpaka 15, kutia ndani kupanga vikundi, kugawa eneo, na kutoa sala. (Ona Kisanduku cha Maulizo katika Huduma Yetu ya Ufalme ya Septemba 2001.) Programu ya utendaji katika mwezi inapaswa kufafanuliwa waziwazi kwa kutaniko na kuwekwa kwenye ubao wa matangazo.

13 Eneo la kutosha linapaswa kutayarishwa. Mwangalizi wa utumishi anapaswa kukutana na ndugu anayeshughulikia maeneo ili kuchukua mipango kwa ajili ya kutumika maeneo yasiyotembelewa kwa ukawaida. Mkazo unapaswa kuwekwa juu ya kukutana na wale ambao hawakuwa nyumbani, kutoa ushahidi barabarani na duka kwa duka, na kutoa ushahidi jioni. Mahali inapofaa, wahubiri fulani wanaweza kusaidiwa ili kutoa ushahidi kwa njia ya simu.

14 Wasaidieni Wafanye kazi Tena: Je, katika eneo la kutaniko lenu kuna watu ambao hawatendi tena katika kuhubiri habari njema? Watu kama hao bado ni sehemu ya kutaniko, nao wanahitaji msaada. (Zab. 119:​176) Kwa kuwa mwisho wa ulimwengu huu wa kale unakaribia sana na kwamba ulimwengu mpya uko karibu-karibu, tuna sababu nzuri ya kufanya jitihada zetu zote ili kusaidia wale ambao wamekuwa wasiotenda. (Rom. 13:​11, 12) Katika miaka mitano iliyopita, watu wengi kila mwaka wameitikia msaada, nao wameanza kutenda tena. Tunaweza kufanya nini ili kusaidia wengine wengi wawashe tena upendo na uhakika waliokuwa nao mwanzoni?​—Ebr. 3:​12-​14.

15 Baraza la wazee litataka kuzungumzia jinsi wanavyoweza kusaidia wale ambao wamekuwa wasiotenda katika miaka mitano iliyopita. (Mt. 18:​12-​14) Mwandishi anapaswa kuchunguza kadi za utendaji za wahubiri wa kutaniko na kuandika wale wote ambao wamekuwa wasiotenda. Jitihada ya pekee inapaswa kufanywa kupitia mpango wa ziara za uchungaji ili kutoa msaada. Huenda mzee akataka kutembelea mhubiri fulani kwa kuwa walijuana na walishirikiana na mhubiri huyo hapo mbele, au huenda wahubiri wengine wakaombwa kusaidia. Labda wahubiri hao walijifunza na yule ambaye sasa ni asiyetenda na kwamba wangekubali kuchukua nafasi hiyo ya kutoa msaada wa pekee wakati huu wa uhitaji. Kuna tumaini kwamba wengi wa wale ambao wamekuwa wasiotenda watachochewa waanze kuhubiri tena neno la Mungu. Ikiwa wanastahili, hakuna wakati ulio bora zaidi kwao kuanza kuliko katika majira ya Ukumbusho!​— Kwa ajili ya habari zaidi, ona Kisanduku cha Maulizo katika Huduma Yetu ya Ufalme ya Novemba 2000.

16 Je, Wengine Wanastahili Kuhubiri? Yehova anaendelea kubariki watu wake kwa kuleta “vitu vya kupendeza vya mataifa yote.” (Hag. 2:7) Kila mwaka maelfu hutimiza sifa za kustahili kuwa wahubiri wasiobatizwa. Hao ni nani? Watoto wa Mashahidi wa Yehova na pia wanafunzi wa Biblia wanaofanya maendeleo. Tunajuaje ikiwa wanastahili kuwa wahubiri wa habari njema?

17 Watoto wa Mashahidi wa Yehova: Watoto wengi wamekuwa wakiambatana na wazazi wao nyumba kwa nyumba kwa miaka mingi, ingawa hawajaanza kutumikia wakiwa wahubiri wasiobatizwa. Mwezi wa Machi unaweza kuwa wakati mzuri ili kuwasaidia waanze. Mtajuaje ikiwa mtoto wenu anastahili? Ukurasa wa 100 katika kitabu Tumefanywa Tengenezo Tutimize Huduma Yetu unasema kwamba ni wakati “mtoto anapokuwa mfano mzuri katika mwenendo wake na anapoweza kueleza binafsi imani yake kwa kuwaambia wengine juu ya habari njema, akiongozwa kutoka moyoni afanye hivyo.” Ikiwa unafikiri kwamba mtoto wako anastahili, ongea na mmoja wa wazee wanaofanyiza Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko.

18 Wanafunzi wa Biblia Wanaostahili: Baada ya mwanafunzi wa Biblia kutwaa ujuzi na kuhudhuria mikutano kwa wakati fulani, huenda akataka kuwa mhubiri wa Ufalme. Ikiwa unaongoza funzo pamoja na mwanafunzi kama huyo, fikiria maulizo haya: Je, anafanya maendeleo kulingana na umri na uwezo wake? Je, ameanza kushiriki imani yake na wengine kwa namna ya vivi hivi? Je, ni mwenye kuvaa “utu mpya”? (Kol. 3:​10) Je, anatimiza sifa zinazotakiwa kwa wahubiri wasiobatizwa, kama zinavyoonyeshwa kwenye ukurasa wa 97-9 katika kitabu Huduma Yetu? Ikiwa ndiyo, unapaswa kukutana na Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko kusudi mipango ichukuliwe ili wazee wawili wakutane nawe na mwanafunzi huyo. Ikiwa anastahili, wale wazee wawili watamjulisha kwamba anaweza kuanza kushiriki katika huduma ya peupe.

19 Namna Gani Kuhusu Aprili na Mei? Hiyo pia itakuwa miezi ya pekee kwa ajili ya utendaji wenye kuongezeka katika huduma ya shambani. Wengi watakaokuwa mapainia wasaidizi mnamo Machi huenda wakawa na uwezo wa kufanya hivyo tena mnamo Aprili na/au Mei. Jambo tutakalotanguliza mnamo Aprili na Mei ni kutoa magazeti Mnara wa Mlinzi na Amkeni! katika huduma. Magazeti hayo yamekuwa na matokeo yenye mafaa kama nini juu ya maisha ya wale walioyasoma! Yametimiza fungu kubwa katika kufikia lile ongezeko zuri ajabu ambalo tumepata ulimwenguni pote. Jitihada ya pekee itafanywa mnamo Aprili na Mei ili kutoa magazeti kwa watu wengi zaidi iwezekanavyo. Panga sasa kushiriki kikamili.

20 Kwa kuwa utendaji wa kuhubiri wenye kuongezeka unapangwa, je, unahitaji kuongeza hesabu ya magazeti unayopata kupitia kutaniko? Katika mwaka wote wa utumishi, tunatoa Mnara wa Mlinzi na Amkeni! kila Siku ya Posho, ambayo ni siku yetu iliyochaguliwa kuwa Siku ya Magazeti. Hata hivyo, kwa kuwa wengi watakuwa wakishiriki utumishi wa painia msaidizi na kwamba sisi sote tutakuwa tukitoa magazeti kwa miezi miwili kamili, huenda likawa jambo la lazima kuongeza ombi lako la magazeti katika kutaniko. Ikiwa ni hivyo, tafadhali julisha mara moja ndugu anayeshughulika na magazeti katika kutaniko lenu. Wakati huohuo, ndugu anayeshughulika na vichapo anapaswa kuwa hakika kwamba kuna kiasi cha kutosha cha trakti Je, Ungependa Kujua Mengi Zaidi Kuhusu Biblia? kwa ajili ya matumizi ya wote.

21 Wengi wameonyesha shukrani kuhusu makala ya Huduma Yetu ya Ufalme yenye kichwa “Tuseme Nini Kuhusu Magazeti.” Je, umefaidika na uandalizi huo kwa kujifunza utoaji mbalimbali wa mfano kuhusu magazeti? Kwa nini msitumie sehemu ya wakati wa funzo lenu la Biblia katika familia ili kujizoeza utoaji huo mbalimbali?

22 Faidika Kikamili na Majira Haya ya Ukumbusho: Kama vile mtume Paulo, acheni tuonyeshe Yehova kwamba tunathamini sana “zawadi yake ya bure isiyoelezeka” kwa kushiriki kikamili katika utendaji mbalimbali wa kiroho unaopangwa kwa ajili ya majira haya ya Ukumbusho. Utendaji huo mbalimbali unatia ndani (1) kuhudhuria lile tukio la maana zaidi la mwaka, ni kusema mwadhimisho wa Chakula cha Jioni cha Bwana Siku ya Nne, Machi 28, 2002; (2) kusaidia wale ambao wamekuwa wasiotenda wawashe tena ‘upendo waliokuwa nao hapo kwanza’ (Ufu. 2:4; Rom. 12:11); (3) kusaidia watoto wetu na wanafunzi wa Biblia wowote wanaostahili wawe wahubiri wasiobatizwa; na (4) kuhusika kikamili zaidi iwezekanavyo katika kazi ya kueneza evanjeli, hata kuwa painia msaidizi mnamo Machi na baadaye.​—2 Tim. 4:5.

23 Sala yetu yenye bidii ni kwamba sote tushiriki kikamili katika kuhubiri habari njema ya Ufalme katika majira haya ya Ukumbusho, tukionyesha hivyo kwamba tunathamini sana yote ambayo Yehova amefanya kwa ajili yetu. 

[Picture on page 6]

For chart, see the printed material

    Vichapo vya Swahili (Congo) (1996-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili (Congo)
    • Tumia Wengine
    • Préférences
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Kanuni za Matumizi
    • Kanuni za Kutunza Siri
    • Paramètres Kuhusu Kutunza Siri
    • JW.ORG
    • Ingia
    Tumia Wengine