Programu Mpya ya Kusanyiko la Mzunguko
1 Ili kusimama imara katika imani katika ulimwengu usiotulia, tunapaswa kumtumaini Yehova. Hilo linamaanisha nini kihalisi? Kumtumaini Yehova kuna matokeo gani juu ya maisha yetu ya kibinafsi na ya familia? Jambo hilo linatusaidiaje kupinga uvutano wa ulimwengu wa Shetani? Programu ya kusanyiko la mzunguko mnamo mwaka wa utumishi wa 2003 itajibu maulizo hayo. Kichwa cha kusanyiko hilo ni “Mtumaini Yehova na Ufanye Mema.”—Zab. 37:3.
2 Hatupaswi kuonyesha kwamba tunamtumaini Yehova kwenye matukio ya pekee tu au tunapokuwa katika uhitaji mkubwa. Tunamtumaini katika sehemu zote za maisha yetu ya kila siku. Hilo litakaziwa katika hotuba ya kufungua, yenye kichwa “Mtumaini Yehova Nyakati Zote.” (Zab. 62:8) Hotuba-mfululizo yenye sehemu nne na yenye kichwa “Tuonyeshe Kwamba Tunamtumaini Yehova” itatuonyesha jinsi ya kupata na kutumikisha habari zenye kutegemea Biblia, ambazo zinaweza kutusaidia kujenga ndoa yenye mafanikio, kushughulikia matatizo yanayotokea katika familia, na kutosheleza mahitaji yetu ya kimwili.
3 Ulimwengu wa Shetani unajaribu kutufanya tukubali maoni yenye kupotoka kuhusu lililo sawa na lililo kosa na kusababisha mvurugo kuhusu mambo tunayopaswa kutanguliza. (Isa. 5:20) Hotuba “Jilinde Dhidi ya Mambo ya Ubatili ya Maisha” na “Epukeni Mabaya—Iweni Watendaji wa Mema” zitaongeza azimio letu la kuunga mkono viwango vya juu vya Yehova.—Amo. 5:14.
4 Yehova atakapokomesha mfumo mbovu wa mambo wa sasa, watumishi wake watahitaji kumtumaini kikamili. Hilo litakaziwa katika hotuba ya watu wote, yenye kichwa “Ukombozi Kutoka Katika Taabu ya Ulimwengu Unakaribia.” Baada ya hotuba hiyo, tutaombwa kujichunguza katika sehemu yenye kichwa “Je, Wewe Utahesabiwa Kuwa Mwenye Kustahili Ufalme wa Mungu?” Programu itamalizika kwa himizo, “Tumaini Ahadi za Yehova.”
5 Tukio kubwa la kila kusanyiko ni hotuba ya ubatizo. Yeyote anayetaka kubatizwa anapaswa kumjulisha mwangalizi-msimamizi mapema zaidi iwezekanavyo ili mipango ya lazima ichukuliwe.
6 Nyakati hizi zisizo na uhakika, Yehova peke yake ndiye chanzo halisi cha tumaini na utulivu. (Zab. 118:8, 9) Na tutie nguvu tumaini letu katika yeye kwa kuhudhuria programu zima ya kusanyiko la mzunguko.