Programu ya Ujenzi wa Majumba ya Ufalme Inasonga Mbele
1 Katika mwaka wa 1983 kwenye Makusanyiko ya Wilaya yenye kichwa “Umoja wa Ufalme” huko Amerika, ilitangazwa kwamba hazina ya pekee ingeanzishwa ili kutegemeza ujenzi na utengenezaji upya wa Majumba ya Ufalme kotekote katika Shirikisho la Amerika na Canada. Wakati huo hatukujua baraka ambazo zingetokana na mianzo hiyo midogo. Tulianza kujionea kikamili zaidi yale ambayo Zaburi 92:4 inaeleza ifaavyo: “Maana wewe BWANA, umenifurahisha kwa kazi yako, nitashangilia kazi za mikono yako.”
2 Tunafurahia yale yanayotimizwa sasa. Leo programu ya ujenzi wa Majumba ya Ufalme yenye kuendeshwa haraka ulimwenguni pote ni yenye kusonga mbele. Kwa njia moja au nyingine, sisi sote tuna pendeleo la kushiriki katika kazi hiyo. Tunafanya hivyo kwa kutoa michango mikubwa au midogo ya kifedha ili kusaidia kulipia gharama za ujenzi wa mahali zaidi pa ibada ulimwenguni pote. Ndugu wengi pia wanatoa kwa kujipendea vifaa vyao na pia wakati wao, uwezo wao, na ufundi wao kuhusiana na mipango kama hiyo. Mafanikio ya mpango huo wote yanatokana na uongozi wa Yehova, utegemezo wake, na baraka zake nyingi juu ya jitihada zetu zenye umoja.—Zab. 127:1.
3 Matawi mengi yamefuata kielelezo kilichoanzishwa kwa ajili ya makutaniko ya Shirikisho la Amerika. Katika Majumba ya Ufalme ya nchi nyingi, kuna kibweta ambamo wahubiri wanatia michango yao kwa ajili ya Hazina ya Majumba ya Ufalme. Katika Shirikisho la Amerika, Huduma Yetu ya Ufalme ya Machi 1997 ilitangaza rekebisho moja ambalo lingefanywa katika programu hiyo. Ilieleza: “Tangu Hazina ya Sosaiti ya Ujenzi wa Majumba ya Ufalme ilipoanzishwa katika 1983, akina ndugu wametoa michango kwa ukarimu, hivyo wakifanya iwezekane kutoa mikopo kwa ajili ya ujenzi wa Majumba ya Ufalme. Tayari makutaniko 2,700 hivi yamefaidika na mpango huo katika Shirikisho la Amerika. Bila mpango huo, makutaniko mengi hayangeweza kujenga Majumba ya Ufalme mapya au kutengeneza upya yale yaliyohitaji kurekebishwa. Sasa kuna uhitaji wa haraka wa kutumia sehemu ya fedha hizo zilizochangwa ili kutoa mikopo kwa makutaniko yanayopatikana katika nchi zenye kushuka kiuchumi. Utegemezo wenu wenye kuendelea wa mpango huu unathaminiwa sana na Sosaiti na yale makutaniko yanayofaidika na michango yenu.”
4 Tangazo hilo lilikuwa mwaliko wa kushiriki katika programu yenye kuendeshwa haraka ya ujenzi ya Majumba ya Ufalme. Hazina ya Majumba ya Ufalme ingepanuliwa ili itie ndani mahitaji ya ndugu zetu katika nchi nyinginezo huku mikopo ikiendelea kutolewa kwa ajili ya ujenzi wa Majumba ya Ufalme katika Shirikisho la Amerika. Makala iliyofuata katika toleo la Huduma Yetu ya Ufalme ya Agosti 1997 ilisema: “Kuna uhitaji wenye kuongezeka wa kujenga Majumba ya Ufalme ulimwenguni pote. Mnamo mwaka wa utumishi uliopita, makutaniko mapya 3,288 yaliundwa. Mengi ya makutaniko hayo yanapatikana Afrika, Asia, Amerika ya Kati na ya Kusini, na Ulaya ya Mashariki.”
5 Matokeo yamekuwa nini tangu wakati huo? Kitabu Annuaire 2001 kiliripoti: “Kupitia mpango huo, katika nchi 30, Majumba ya Ufalme 453 yamekwisha kukamilishwa, na mengine 727 ni yenye kujengwa sasa. Mkazo umetiwa juu ya kusitawisha plani za Majumba ya Ufalme zitakazofuatwa katika kila nchi, zikitumia vifaa na ufundi wa ujenzi wa mahali. Huko Kenya, mawe yanayochimbwa yanatumiwa; huko Togo ni jambo la kawaida kutumia matofali; huko Kamerun mabloku ya sementi yanayopigwa plasta ni yenye kutumiwa na wengi. Katika njia hiyo, akina ndugu wa nchini wanaweza kupata ufundi unaohitajiwa ili kutimiza fungu la maana katika programu ya nchi yao.”
6 Uhakikisho wa kwamba Yehova anabariki programu hii unaweza kupatikana katika bara kuu la Afrika. Unapotazama picha za Majumba ya Ufalme fulani ambayo yamejengwa, wazia uvutano ambao ujenzi huo umekuwa nao juu ya kazi ya Mashahidi wa Yehova! Hilo ni kweli katika sehemu tatu tofauti—umoja wa undugu wetu wa ulimwenguni pote, tokeo juu ya watu wa mahali, na ongezeko katika hudhurio kwenye mikutano ya kutaniko. Nyongeza hii inaonyesha Majumba ya Ufalme yaliyojengwa katika Afrika, lakini matoleo yajayo ya Huduma Yetu ya Ufalme yataonyesha jinsi programu ya ujenzi wa Majumba ya Ufalme inavyosonga mbele katika sehemu nyingine za dunia.
[Picha kwenye ukusara wa 3]
Bimbo, Bangui
JAMHURI YA AFRIKA YA KATI
Begoua, Bangui
Picha kwenye ukusara wa 4]
Ukonga, Tanzania
Accra, Ghana
Salala, Liberia
Allada, Benin—Jumba la Ufalme la zamani
Allada, Benin—Jumba la Ufalme jipya
Karoi, Zimbabwe
[Picha kwenye ukusara wa 5]
Kpeme, Togo
Sokodé, Togo
Fidjrosse, Benin
[Picha kwenye ukusara wa 6]
Lyenga, Zambia—Jumba la Ufalme la zamani
Lyenga, Zambia—Jumba la Ufalme jipya
Kinshasa, Congo
Musambira, Rwanda