Jinsi Waangalizi wa Funzo la Kitabu la Kutaniko Wanavyoonyesha Kupendezwa Kibinafsi
1 Shabaha ya Funzo la Kitabu la Kutaniko ni kufanya ‘iwezekane kila mtu apewe msaada wa kibinafsi kwa ajili ya ukuzi wa kiroho. Huo ni wonyesho wa fadhili zenye upendo za Yehova na utunzaji wake mpole wa watu wake.’ (om-SW uku. 75; Isa. 40:11) Mwangalizi wa funzo la kitabu ana daraka la maana sana katika kutoa uangalifu huo wa kibinafsi.
2 Kwenye Funzo la Kitabu: Kwa kuwa vikundi vya funzo la kitabu vinafanywa viendelee kuwa vidogo kwa kusudi, mwangalizi wa funzo la kitabu anaweza kupata kujua vizuri washiriki wa kikundi chake. (Mez. 27:23) Kwa kawaida kuna nafasi za kushirikiana kabla au baada ya funzo kila juma. Katika mwezi, huenda ikawezekana aongee karibu na kila mtu katika kikundi. Hilo linasaidia washiriki wa funzo la kitabu kuhisi wako huru kumkaribia wanapokabiliana na majaribu au wanapohitaji kitia-moyo.—Isa. 32:2.
3 Mwangalizi wa funzo la kitabu anajaribu kutia moyo wote katika kikundi washiriki wakati wa funzo. Njia moja ambayo kwa hiyo anafanya hivyo ni kwa kuongoza funzo kwa fadhili na kwa upole. (1 Thes. 2:7, 8) Anatafuta njia za kuhusisha wote katika mazungumzo, kutia ndani watoto wadogo. Ikiwa wengine wanaogopa kutoa maelezo, anaweza kutoa msaada kwa siri kwa kuchukua mipango kimbele ili wasome andiko au kutoa maelezo kuhusu fungu fulani hasa. Au anaweza kuwaonyesha jinsi ya kutoa maelezo katika maneno yao wenyewe.
4 Ikiwa msaidizi wa mwangalizi wa funzo la kitabu ni mtumishi wa huduma, mwangalizi atachukua mipango ili aongoze funzo mara moja kila miezi miwili. Jambo hilo litamwezesha mwangalizi atazame msaidizi na kumtolea mashauri yatakayomsaidia. Ni mpango mzuri kama nini kusaidia akina ndugu waboreshe ufundi wao wa kufundisha!—Tito 1:9.
5 Katika Huduma ya Shambani: Moja la madaraka ya msingi ya mwangalizi wa funzo la kitabu ni kuongoza kazi ya kueneza evanjeli. (Hes. 27:16, 17) Anachukua mipango yenye kutumika kwa ajili ya kutoa ushahidi katika kikundi na anajitahidi kusaidia wote katika kikundi wapate furaha katika huduma yao. (Efe. 4:11, 12) Ili kutimiza hilo, anajiwekea mradi wa kutumika na kila mshiriki wa kikundi katika utumishi. Anatumika pia na mwangalizi wa utumishi ili kuchukua mpango kusudi wale ambao wangependa kuboresha sehemu fulani ya huduma yao wapate msaada kutoka kwa mhubiri mwenye uzoefu zaidi.
6 Akiwa Mchungaji Mwenye Upendo: Mwangalizi wa funzo la kitabu anapendezwa na wale ambao, kwa sababu ya hali zao, wanaweza kushiriki katika kazi ya kuhubiri kwa kiasi kidogo tu. Kuhusu wale walio na vizuizi kwa sababu ya umri mkubwa au kwa sababu hawawezi kutoka nyumbani, na pia wale walio na vizuizi vya muda kwa sababu ya kugonjwa sana au kuumia vibaya, mwangalizi wa funzo la kitabu anahakikisha kwamba wanajua kuhusu ule mpango unaowaruhusu waripoti wakati waliopitisha katika utumishi wa shambani kwa vipindi vya dakika 15 ikiwa hawawezi kuripoti saa nzima katika mwezi moja. (Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko ndiyo inayoamua ni nani anayestahili uandalizi huo.) Anapendezwa pia na washiriki wa kikundi ambao huenda ni wasiotenda, akijitahidi kuwasaidia waanze tena utendaji wao pamoja na kutaniko.—Luka 15:4-7.
7 Sisi ni wenye shukrani kama nini kwa ajili ya kupendezwa kwenye upendo kunakoonyeshwa na waangalizi wa funzo la kitabu! Uangalifu wa kibinafsi wanaotoa unatusaidia “sote tuufikie umoja katika imani . . . , kufikia kipimo cha kimo ambacho ni cha ujao wa Kristo.”—Efe. 4:13.