Tangazeni Ujumbe wa Ufalme
1 “Ni lazima nitangaze habari njema ya ufalme wa Mungu, kwa sababu kwa ajili ya hili nilitumwa.” (Luka 4:43) Kupitia maneno hayo, Yesu alitambulisha kichwa cha huduma yake—Ufalme wa Mungu. Ujumbe tunaotangaza leo pia unakazia Ufalme, kama ilivyotabiriwa katika Mathayo 24:14: “Na habari njema hii ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa kwa ajili ya kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo mwisho utakapokuja.” Ni kweli gani kuhusu Ufalme wa Mungu ambazo watu wanahitaji kusikia?
2 Ufalme wa Mungu unatawala sasa kutoka mbinguni na karibuni utachukua mahali pa utawala wote wa kibinadamu. Ibilisi amekwisha kuondolewa kutoka mbinguni, na mfumo mbovu wa mambo wa sasa umeingia katika siku zake za mwisho. (Ufu. 12:10, 12) Mfumo mbovu wa mambo wa Shetani utaharibiwa kikamili, lakini Ufalme wa Mungu hautatikisika. Utadumu milele.—Dan. 2:44; Ebr. 12:28.
3 Ufalme utatosheleza tamaa zinazofaa za wanadamu watiifu wote. Utaondoa kuteseka kunakosababishwa na vita, jeuri, uonevu, na umaskini. (Zab. 46:8, 9; 72:12-14) Kutakuwa chakula kingi kwa ajili ya wote. (Zab. 72:16; Isa. 25:6) Magonjwa na ulemavu yatakuwa mambo ya zamani. (Isa. 33:24; 35:5, 6) Kadiri wanadamu watakavyokuwa wakisonga mbele kuelekea ukamilifu, dunia itageuzwa kuwa paradiso, na watu watakaa pamoja kwa umoja.—Isa. 11:6-9.
4 Tunaonyesha kwamba tunataka kuwa raia wa Ufalme wa Mungu kupitia namna tunavyoishi sasa. Ujumbe wa Ufalme unapaswa kuwa na uvutano juu ya maisha yetu yote, kutia ndani miradi yetu na mambo tunayotanguliza. Kwa mfano, ingawa tuna wajibu wa kutolea watu wa nyumbani mwetu vitu wanavyohitaji, hatuwezi kuruhusu mahangaiko ya kimwili yasonge faida za Ufalme. (Mt. 13:22; 1 Tim. 5:8) Badala yake, tunapaswa kufuata shauri la Yesu: “Basi, fulizeni kutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake, na vitu vingine vyote hivi [mambo ya kimwili yanayohitajiwa maishani] mtaongezewa.”—Mt. 6:33.
5 Ni jambo la haraka kwamba watu wasikie na kutenda kulingana na ujumbe wa Ufalme kabla haijakuwa kuchelewa mno. Acheni tuwasaidie wafanye hivyo kwa “kutumia ushawishi kuhusu ufalme wa Mungu.”—Mdo 19:8.