Neno la Mungu Ni Kweli
1 “Jumla ya neno lako ni kweli,” aliandika mtunga-zaburi. (Zab. 119:160) Kupitia Neno lake lililoandikwa kwa uongozi wa roho takatifu, Yehova anatoa majibu yenye kutosheleza kwa maulizo ya maana zaidi maishani. Anatoa faraja na tumaini kwa wale walio na wasiwasi. Anatuonyesha pia jinsi tunavyoweza kumkaribia. “Kujifunza kweli kutoka Biblia ni sawa na kutoka mahali penye giza na huzuni nyingi na kuingia chumba kilicho wazi, changavu, na kipendezacho,” akasema mwanamke mmoja mwenye shukrani. Je, unajitahidi kuwaelezea wengine kweli ya Neno la Mungu kila wakati nafasi inapojitokeza?
2 Ina Nguvu ya Kugeuza na Inapendeza Ulimwengu Wote: Kweli ya Biblia ina nguvu ya kugusa mioyo na kugeuza maisha. (Ebr. 4:12) Mwanamke mmoja kijana anayeitwa Rosa, alikuwa amehusika katika ukahaba, na pia alkoholi na matumizi ya dawa za kulevya. “Siku moja, nilipokuwa nimetamauka sana,” yeye asema, “wenzi fulani wa ndoa walio Mashahidi walinizungumzia kuhusu jinsi Biblia iwezavyo kutusaidia kutatua matatizo yetu. Nilianza kujifunza Neno la Mungu, nalo lilinistaajabisha sana. Kwa muda wa mwezi mmoja nilipata nguvu ya kuanza upya maisha safi yaliyo mapya kabisa. Sasa kwa vile nilikuwa na kusudi maishani, sikuhitaji tena kutegemea kileo au dawa za kulevya. Na kwa kuwa nilitaka sana kuwa rafiki wa Yehova, niliazimia kuishi kwa viwango vyake. Kama isingalikuwa hekima yenye kutumika ya Neno la Mungu, nina hakika kwamba kufikia sasa ningekuwa nimejiua.”—Zab. 119:92.
3 Tofauti na vitabu vingi leo, Biblia inapendeza watu wa ‘mataifa yote, makabila yote, vikundi vyote vya watu na lugha zote.’ (Ufu. 7:9) Mapenzi ya Mungu ni “kwamba watu wa namna zote waokolewe na kuja kwenye ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Tim. 2:4) Kwa hiyo, hatupaswi kamwe kufikiri kwamba mtu hatapokea habari njema kwa sababu tu ya malezi yake. Badala yake, shiriki ujumbe wa Ufalme na wote, ukifanya hivyo moja kwa moja kutoka katika Biblia inapowezekana.
4 Kazia Maandiko: Kuna nafasi nyingi za kutumia Biblia katika huduma. Unapotolea watu magazeti, jaribu kutia ndani andiko linalopatikana katika utoaji unaopendekezwa. Wanapotumia toleo la vichapo la mwezi, wengine wanaona kuwa jambo lenye matokeo kutia ndani ya maneno yao ya utangulizi usomaji wa andiko moja lililochaguliwa kwa uangalifu. Unapofanya ziara za kurudia, shiriki kila wakati andiko moja la Biblia au zaidi ili kusaidia mwenye nyumba apate ujuzi sahihi hatua kwa hatua. Unapoongoza funzo la Biblia, kazia maandiko ya msingi muda wa mazungumzo. Unapokuwa haushiriki katika huduma iliyopangwa, uwe na Biblia ikiwa tayari ili uitumie nafasi ya kutoa ushahidi wa vivi hivi inapojitokeza.—2 Tim. 2:15.
5 Na tuwasaidie wengine wafaidike na nguvu yenye kuchochea ya kweli ya Neno la Mungu kwa kutumia Biblia kila wakati nafasi inayofaa inapojitokeza katika huduma yetu.—1 Thes. 2:13.
[Study Questions]
1. Ni habari gani ya maana inayopatikana katika Biblia?
2. Biblia inaboreshaje maisha za watu?
3. Kwa nini hatupaswi kujizuiza kushiriki ujumbe wa Biblia na wengine?
4. Tunawezaje kutumia Biblia tunapotoa ushahidi?
5. Kwa nini tunapaswa kujitahidi kutumia Biblia katika huduma yetu?