Kutoa Ushahidi Pamoja Kunaleta Shangwe
1 Alipotuma wanafunzi 70 waende kuhubiri, Yesu aliwapa maagizo kuhusu mambo ya kusema, aliwapanga wakiwa vikundi vya wawili-wawili, na akawajulisha eneo walilopaswa kutembelea. Hilo lilichangia furaha waliyopata. (Luka 10:1-17) Hivyohivyo leo, kutoa ushahidi pamoja kunasaidia kuwaandalia vifaa, kupanga, na kutia moyo watu wa Mungu kwa ajili ya kazi ya kuhubiri.
2 Wazee Wanachukua Uongozi: Wazee wanatimiza fungu la maana katika kusaidia wote washiriki kwa ukawaida katika kazi ya kuhubiri. Mwangalizi wa utumishi anachukua uongozi katika kufanya mipango kwa ajili ya utumishi katikati ya juma. Kila mwangalizi wa funzo la kitabu ana daraka la kupanga utendaji katika kikundi chake, hasa kwenye mwisho-juma. Pindi kwa pindi kutaniko linapokutana kwa ajili ya utumishi wa shambani, kama vile baada ya Funzo la Mnara wa Mlinzi, kila mwangalizi wa funzo la kitabu atashughulikia mahitaji ya kikundi chake mwenyewe.
3 “Kwa Adabu na kwa Mpango”: Yule aliyechaguliwa ili kuongoza mkutano kwa ajili ya utumishi wa shambani ataanza pa wakati na kufanya mkutano usizidi dakika 10 au 15. Ni vizuri zaidi apange watu watakaotoa ushahidi pamoja na kugawa eneo (isipokuwa waangalizi wa mafunzo ya kitabu watakuwa wenye kushughulikia jambo hilo, kama ilivyoonyeshwa mapema) kabla ya kumalizia kwa sala. Jambo hilo linapunguza uhitaji wa wahubiri kukusanyika katika eneo, jambo ambalo linaweza kupunguza heshima ya kazi yetu. Pia, jambo hilo linapatana na shauri la Paulo: “Acheni mambo yote yatukie kwa adabu na kwa mpango.” (1 Kor. 14:40) Wote wanaohudhuria mikutano hiyo wanapaswa kuchangia mafanikio ya mpango huo kwa kufika pa wakati, kushirikiana kikamili na yule anayechukua uongozi, na kwenda haraka katika eneo baada tu ya kikundi kuruhusiwa kwenda.
4 Wenye Kuunganishwa kwa Umoja: Mipango ya kutoa ushahidi pamoja inatutolea nafasi bora ya kupata kujua wengine katika kutaniko. Ingawa hakuna sababu ya kukataza kufanya mipango kimbele ili kutumika na mtu fulani, linaweza pia kuwa jambo lenye kuthawabisha kwetu kuhudhuria mikutano kwa ajili ya utumishi wa shambani bila kufanya mipango kimbele. Tunaweza kupewa mgawo wa kutumika na mtu fulani tusiyemjua vizuri, jambo litakalotuwezesha ‘kupanuka’ katika upendo wetu.—2 Kor. 6:11-13.
5 Kutoa ushahidi pamoja kunatutia moyo na kunatuunganisha tukiwa “wafanyakazi wenzi katika kweli.” (3 Yn. 8) Na tushiriki kikamili katika kazi ya kutoa ushahidi pamoja!