Kazi Inayoburudisha
1 Ujumbe wa Biblia unaburudisha wote wanaoukubali na kuutumikisha katika maishani yao. (Zab. 19:7, 8) Unawasaidia wajiweke huru kutoka katika mafundisho ya uwongo na mazoea yenye kuumiza na unatoa tumaini la wakati ujao lenye kutegemeka. Hata hivyo, si wale wanaopokea habari njema peke yao ndio wanaofaidika. Wale wanaoshiriki na wengine kweli za Biblia zenye kuburudisha wanaburudishwa wenyewe pia.—Mez. 11:25.
2 Huduma Inatutia Nguvu: Yesu alisema kwamba wale wanaokubali nira ya kuwa wanafunzi Wakristo, inayotia ndani kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi, ‘watapata burudisho kwa ajili ya nafsi zao.’ (Mt. 11:29) Yeye mwenyewe alitambua kwamba kutolea wengine ushahidi kunatia nguvu. Kulikuwa kama chakula kwake. (Yoh. 4:34) Alipotuma wale wanafunzi 70 waende kuhubiri, hao walishangilia walipoona jinsi Yehova alivyotegemeza jitihada zao.—Luka 10:17.
3 Vivyo hivyo, Wakristo wengi leo wanatiwa nguvu kwa kushiriki katika kazi ya kuhubiri. Dada mmoja alisema: “Huduma huburudisha kwa kuwa inafanya maisha yangu yawe na kusudi. Ninaposhiriki katika utumishi, sifikirii sana matatizo yangu ya kibinafsi na mikazo ninayopata kila siku.” Mhudumu mwingine mwenye bidii alisema: “Ninaposhiriki huduma, Yehova huwa halisi kwangu kila siku na ninapata kiasi fulani cha amani na furaha ya moyoni isiyoweza kupatikana kwa njia nyingine yoyote.” Ni pendeleo kama nini tulilo nalo kuwa “wafanyakazi wenzi wa Mungu”!—1 Kor. 3:9.
4 Nira ya Kristo Ni ya Fadhili: Ingawa Wakristo wanahimizwa ‘wajikakamue wenyewe kisulubu,’ Yesu hatuombi zaidi ya yale tunayoweza kutoa. (Luka 13:24) Kwa kweli, anatualika kwa upendo ‘tujitie chini ya nira yake pamoja naye.’ (Mt. 11:29, kielezi-chini) Wale wanaolazimika kupambana na hali ngumu wanaweza kuwa na uhakika kwamba utumishi wao wa nafsi yote, hata ikiwa ni mdogo, unapendeza Mungu.—Marko 14:6-8; Kol. 3:23.
5 Ni jambo lenye kuburudisha kama nini kutumikia Mungu anayethamini lolote tunalofanya kwa ajili ya jina lake! (Ebr. 6:10) Na tujitahidi sikuzote kumtolea kilicho bora tulicho nacho.