Tusitawishe Urafiki wa Karibu Pamoja na Yehova
1 “Nimekuwa katika kweli kwa miaka 20 hivi iliyopita kwa kwenda tu kwenye mikutano na kushiriki katika huduma ya shambani,” akasema dada mmoja Mkristo. Hata hivyo, anaendelea kusema: “Nimekata maneno kwamba ingawa mambo hayo ni ya maana, hayo yenyewe hayawezi kunitegemeza wakati mambo yanapoanza kuwa magumu. . . . Sasa ninatambua kwamba lazima nibadili mafikiri yangu na kuanza programu yenye kusudi ya kujifunza ili nipate kumjua Yehova kwelikweli na kumpenda, na kuthamini yale ambayo Mwana wake ametupatia.”
2 Kujenga uhusiano wa kibinafsi na wa karibu pamoja na Yehova kunaomba jitihada. Kunaomba mengi zaidi kuliko kufuatia tu kawaida ya utendaji wa Kikristo. Ikiwa tunashindwa kupashana habari na Yehova kwa ukawaida, baada ya wakati fulani anaweza kuwa kwetu kama mtu aliyekuwa rafiki wa karibu lakini ambaye sasa hatuwasiliani naye tena. (Ufu. 2:4) Acheni tuchunguze jinsi funzo la kibinafsi la Biblia na sala inavyoweza kutusaidia tusitawishe urafiki wa karibu pamoja na Yehova.—Zab. 25:14.
3 Umaana wa Sala na Kutafakari: Funzo la kibinafsi linaloimarisha moyo linahusisha mengi zaidi kuliko kupiga mstari chini ya mambo makuu katika habari ya funzo na kuchunguza maandiko yanayotajwa. Linatuomba kutafakari juu ya yale ambayo habari inafunua kuhusu njia za Yehova, viwango vyake, na utu wake. (Kut. 33:13) Kupata kuelewa mambo ya kiroho kuna uvutano juu ya hisia-moyo zetu na kunatuchochea kufikiria maisha yetu wenyewe. (Zab. 119:35, 111) Tunapaswa kufanya funzo la kibinafsi tukiwa na lengo la kumkaribia Yehova. (Yak. 4:8) Funzo linalochukuliwa kwa uzito linaomba wakati na mahali panapofaa, na funzo la kawaida linaomba tujitie nidhamu. (Dan. 6:10) Hata ikiwa maisha yako ni yenye shughuli sana, je, unapanga wakati kila siku ili kutafakari sifa nzuri ajabu za Yehova?—Zab. 119:147, 148; 143:5.
4 Sala yenye kutoka moyoni ni sehemu ya maana ya funzo la kibinafsi lenye kusudi. Ili kweli za Biblia ziguse mioyo yetu na kutuchochea “kumtolea Mungu . . . utumishi mtakatifu kwa woga wa kimungu na heshima,” tunahitaji roho takatifu ya Mungu. (Ebr. 12:28) Kwa hiyo, tunapaswa kuanza kila kipindi cha funzo kwa kumwomba Yehova roho yake. (Mt. 5:3) Tunapotafakari Maandiko na kutumia vichapo vinavyotolewa na tengenezo la Yehova ili kutusaidia katika funzo, tunamfungulia Yehova moyo wetu. (Zab. 62:8) Kujifunza kwa namna hiyo ni tendo la ibada ambalo kupitia hilo tunaonyesha ujitoaji wetu kwa Yehova na kunaimarisha ufungamano wetu kwake.—Yuda 20, 21.
5 Kama ilivyo kuhusu uhusiano mbalimbali, uhusiano wetu na Yehova unapaswa kuendelea kusitawishwa ili kuufanya uzidi kukomaa muda wote wa maisha yetu. Kwa hiyo, na tununue wakati kila siku ili kumkaribia Mungu, tukijua kwamba yeye pia, kwa upande wake, atatukaribia sisi.—Zab. 1:2, 3; Efe. 5:15, 16.
[Study Questions]
1. Dada mmoja alikuja kutambua nini kuhusu kawaida yake ya kiroho?
2. Kwa nini ni jambo la maana kusitawisha urafiki ya karibu pamoja na Yehova?
3. Ni njia gani ya kufanya funzo la kibinafsi itakayotusaidia tumkaribie Mungu?
4. Sala kuhusiana na funzo la kibinafsi inatusaidiaje kusitawisha urafiki wa karibu pamoja na Yehova?
5. Kwa nini ni jambo la maana kwetu kutafakari Neno la Mungu kila siku?