Endeleeni Kuangalia Sana Jinsi Mnavyotumia Wakati Wenu
1 Katika siku zetu kuna vyombo vingi vinavyopunguza wakati na kazi, inaonekana kuwa wengi wanajikuta wakiwa na mambo mengi zaidi ya kufanya na wakati mdogo zaidi wa kuyafanya. Je, ni vigumu kwako kudumisha kawaida nzuri ya kiroho? Je, wewe ungetaka kuwa na wakati zaidi kwa ajili ya huduma? Tunawezaje kutumia vizuri zaidi wakati wetu?—Zab. 90:12; Flp. 1:9-11.
2 Tutambue Vipoteza-Wakati: Mara kwa mara, sisi sote tunapaswa kuchunguza jinsi tunavyotumia wakati wetu. Biblia inahimiza: “Endeleeni kuangalia sana kwamba jinsi mnavyotembea si kama watu wasio na hekima bali kama watu wenye hekima, mkijinunulia wakati unaofaa, kwa sababu siku hizi ni zenye uovu.” (Efe. 5:15, 16) Fikiria matatizo yanayotokezwa na maendeleo ya tekinolojia ya kompyuta na vyombo vingine vya kielektroniki. Ingawa vyombo hivyo vina matumizi yenye kufaa, vinaweza kuwa mtego ikiwa hatuangalie sana jinsi tunavyotumia wakati wetu.—1 Kor. 7:29, 31.
3 Kila mmoja wetu anapaswa kujiuliza: ‘Je, ninapoteza wakati kila siku nikisoma au kujibu ujumbe mbalimbali wa kielektroniki ambao ni wa kuudhi tu? Je, ninawasiliana mara nyingi kwa njia ya simu au ninajihusisha sana katika kutuma ujumbe wa kielektroniki kuhusu mambo ya ovyoovyo? (1 Tim. 5:13) Je, ninajikuta nikisoma-soma mambo katika Internet bila kusudi lolote au kubadilibadili stesheni bila kusudi, ninapotazama televisheni? Je, michezo ya kompyuta imeanza kuchukua wakati wangu wa funzo la Neno la Mungu?’ Ufuatiaji wa namna huo unaweza kuharibu polepole hali yetu ya kiroho.—Met. 12:11.
4 Tutumie Wakati Kwa Hekima: Vyombo vya kielektroniki vina mwelekeo wa kuchukua wakati na uangalifu wetu. Kijana mmoja aliyejiingiza sana katika michezo ya kompyuta alikubali: “Nyakati nyingine nilipokuwa nimecheza kabla ya kwenda kuhubiri au kabla ya kuhudhuria mkutano wa Kikristo, ilikuwa vigumu sana kwangu kukaza fikira. Mara nyingi nilifikiria jinsi nitakavyocheza vizuri zaidi wakati nitakaporudi nyumbani. Nilipuuza funzo la pekee na kusoma Biblia kwa ukawaida. Furaha yangu ya kumtumikia Mungu ilianza kupungua.” Akitambua kwamba alipaswa kufanya mabadiliko, yeye alifuta michezo yake yote ya kompyuta. “Haikuwa rahisi kufanya hivyo,” yeye anakumbuka. “Nilitambua kwamba nilipenda sana michezo hiyo. Lakini pia nilijisikia vizuri sana niliposhinda pambano hilo kwani ilikuwa kwa faida yangu.”—Mt. 5:29, 30.
5 Inaweza kuwa lazima kuchukua hatua kama hizo ikiwa kuna sehemu ambazo unahitaji kufanyia marekebisho. Je, unaweza kununua kila siku nusu-saa kutoka shughuli zisizo za lazima? Huo ndio karibu wakati unaohitaji kila siku ili kusoma Biblia nzima katika mwaka moja. Ni jambo lenye kuthawabisha kiroho kama nini! (Zab. 19:7-11; 119:97-100) Jiwekee wakati kamili wa kusoma Biblia, wa kutayarisha mikutano, na wa kufanya huduma ya shambani. (1 Kor. 15:58) Kufanya hivyo kutakusaidia ushinde vipoteza-wakati na kutakusaidia ‘uendelee kufahamu yale yaliyo mapenzi ya Yehova.’—Efe. 5:17.
[Maulizo ya Funzo]
1. Kila mahali leo, watu wanapambana na tatizo gani?
2, 3. Ni tatizo gani linalotokezwa na tekinolojia ya kompyuta na vyombo vya kielektroniki, na namna gani kila mmoja wetu anaweza kujichunguza?
4. Ni marekebisho gani ambayo kijana mmoja alifanya, na kwa nini?
5. Tunawezaje kununua wakati kwa ajili ya ufuatiaji wa mambo ya kiroho, na tunafaidikaje kwa kufanya hivyo?