Kuhubiri Ufalme—Pendeleo Lenye Thamani
1 Kila siku, mabilioni ya watu duniani wanafaidika na mipango ya Yehova yenye ukarimu inayotegemeza uzima. (Mt. 5:45) Hata hivyo, ni watu wachache sana wanaofurahia pendeleo la pekee la kuonyesha shukrani kwa Muumba wao kwa kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu. (Mt. 24:14) Unathamini pendeleo hilo kubwa kwa kadiri gani?
2 Kuhubiri Ufalme kunamletea Mungu heshima na kunaleta tumaini na amani kwa watu wanaohuzunishwa na wakati wa leo wenye msukosuko. (Ebr. 13:15) Kwa wale wanaoitikia ujumbe, hilo linamaanisha uzima wa milele. (Yoh. 17:3) Ni kazi gani ya kimwili inayotolea faida kama hizo? Mtume Paulo alionyesha shukrani yake kuhusu huduma kutokana na namna alivyoitimiza. Aliiona kuwa hazina.—Mdo. 20:20, 21, 24; 2 Kor. 4:1, 7.
3 Kuonyesha Shukrani Kuhusu Pendeleo Letu Lenye Thamani: Njia moja ambayo kwa hiyo tunaonyesha shukrani kuhusu pendeleo letu la kuhubiri ni ile ya kutoa uangalifu kuhusu ubora wa utumishi wetu. Je, tunachukua wakati wa kutayarisha utoaji utakaogusa mioyo ya wasikilizaji wetu? Je, tunaweza kuboresha ufundi wetu kwa kutumia Maandiko na kwa kufikiri pamoja na watu? Je, tunatumika kikamili katika eneo tulilogawiwa? Je, tunaweza kuanzisha na kuongoza funzo la Biblia? Kama Wakristo waaminifu, wa zamani na wa sasa, tunachochewa na mtazamo unaofaa wa utendaji huu, na tunathamini pendeleo letu.—Mt. 25:14-23.
4 Tunaposumbuliwa na matokeo ya umri mkubwa, afya mbaya, au matatizo mengine, ni jambo lenye kufariji kujua kwamba jitihada zetu zenye bidii za kushiriki katika huduma zinathaminiwa kweli kwa kadiri kubwa. Neno la Mungu linatuhakikishia kwamba Yehova anathamini jitihada kama hizo za kumtumikia, hata ikiwa jitihada hizo zinaonekana kuwa hazivutii wengine.—Luka 21:1-4.
5 Kuhubiri Ufalme ni chanzo cha utoshelevu mkubwa. Dada mmoja mwenye umri wa miaka 92 alisema: “Ni pendeleo kabisa kutazama nyuma miaka zaidi ya 80 ya utumishi wa kujitoa kwa Mungu—bila hata kujuta! Kama ningeishi upya maisha yangu, ningeishi vivyo hivyo kwa sababu, kwa kweli, ‘fadhili za Mungu zenye upendo ni bora kuliko uzima.’” (Zaburi 63:3) Sisi sote na tuthamini sana pendeleo hilo lenye thamani kutoka kwa Mungu—kazi ya kuhubiri Ufalme.