Chukua kwa Uzito Kazi Yako ya Kuhubiri
1. Namna gani watu wengi katika ulimwengu wanaona kazi yetu ya kuhubiri?
1 Katika ulimwengu huu wa Shetani, watu wengi wanaona kazi yetu ya kuhubiri kuwa “upumbavu.” (1 Kor. 1:18-21) Ikiwa hatuko waangalifu, maoni hayo yasiyofaa yanaweza kutuvunja moyo na kutufanya tupunguze bidii yetu. (Met. 24:10; Isa. 5:20) Kwa nini tunapaswa kuchukua kwa uzito pendeleo letu la kuwa Mashahidi wa Yehova?—Isa. 43:10.
2. Kwa nini kazi ya kuhubiri inaweza kuitwa “kazi takatifu”?
2 Ni “Kazi Takatifu”: Mutume Paulo alisema kwamba kazi ya kuhubiri ni “kazi takatifu.” (Rom. 15:15, 16) Kwa nini kazi ya kuhubiri ni “kazi takatifu”? Tunapohubiri, ‘tunafanya kazi pamoja’ na ‘Mutakatifu,’ yaani, Yehova. Na tunapofanya kazi hiyo tunashiriki katika kulitakasa jina lake. (1 Kor. 3:9; 1 Pet. 1:15) Yehova anaona kazi yetu ya kuhubiri kuwa ‘zabihu ya sifa,’ kwa hiyo kazi ya kuhubiri ni sehemu ya maana ya ibada yetu.—Ebr. 13:15.
3. Kwa nini kuhubiri habari njema ni pendeleo nzuri sana?
3 Ni watu wachache tu ndio waliopewa pendeleo hilo nzuri la kuhubiri habari njema. Malaika wangepewa pendeleo hilo, wangeifanya kazi hiyo kwa furaha sana na bila shaka wangeifanya vizuri sana kuliko sisi. (1 Pet. 1:12) Lakini, Yehova ametuchagua sisi wanadamu wasiokamilika, “vyombo vya udongo,” ili tuchukue pendeleo hilo la ajabu sana!—2 Kor. 4:7.
4. Namna gani tunaweza kuonyesha kwamba tunachukua kwa uzito kazi yetu ya kuhubiri?
4 Ni Kazi ya Kutia pa Nafasi ya Kwanza: Kwa kuwa tunachukua kwa uzito kazi yetu ya kuhubiri, tunaiona kuwa kati ya “mambo yaliyo ya maana zaidi” maishani mwetu. (Flp. 1:10) Kwa hiyo, tunapanga wakati kila juma ili kuhubiri. Mwanamuziki anayechukua kwa uzito pendeleo lake la kucheza muziki katika kikundi cha wanamuziki chenye kujulikana sana atajitayarisha kila wakati wa kucheza muziki na atajikaza ili ufundi wake wa kucheza muziki uwe muzuri zaidi. Vivyo hivyo, tujitayarishe mbele ya kuenda kwenye mahubiri ili tuweze ‘kutumia sawasawa neno la kweli,’ na tujikaze kufanya ‘ufundi wetu wa kufundisha’ uwe muzuri zaidi.—2 Tim. 2:15; 4:2.
5. Ni nani wanaopendezwa na kazi yetu ya kuhubiri?
5 Tusiache hali ya watu fulani wasiopendezwa ituvunje moyo. Tukumbuke kwamba bado kuna watu wengi katika eneo letu wanaopenda tuwatembelee. Hata hivyo, hatutafute kukubaliwa na watu. Jambo la maana zaidi ni jinsi Yehova anavyoona kazi hiyo, na tuko hakika kwamba anapendezwa sana na bidii tunayofanya ili kuitimiza.—Isa. 52:7.