Tangazeni Utukufu wa Yehova
1 Mtunga-zaburi alitangaza: “Mwimbieni Yehova, enyi watu wote wa dunia. . . . Tangazeni utukufu wake kati ya mataifa, kazi zake za ajabu kati ya vikundi vyote vya watu.” Tunapofikiria kwa uzito yale ambayo Yehova ametufanyia, yale anayotufanyia, na yale ambayo bado atatufanyia, mioyo yetu inatuchochea kutangaza utukufu wake!—Zab. 96:1, 3.
2 Katika Huduma Yetu: Mashahidi wa Yehova wana pendeleo la kuchukua jina la Mungu na kulisifu peupe duniani kote. (Mal. 1:11) Wao ni tofauti kabisa na viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo, ambao kwa kiburi wanaondoa jina la Mungu katika tafsiri zao za Biblia. Kazi ya kujulisha jina la Mungu ni ya haraka, kwa kuwa watu wanapaswa kuliitia jina hilo kwa imani ili kuokolewa wakati wa dhiki kubwa inayokuja. (Rom. 10:13-15) Zaidi ya hilo, amani ya ulimwenguni pote, kutia ndani amani kati ya wakaaji wa dunia, inategemea utakaso wa jina la Mungu. Hakika, kazi zote za Mungu zinahusiana na jina lake.
3 “Yehova ni mkuu na wa kusifiwa sana.” Lakini kusudi watu ‘wamhesabie Yehova utukufu wa jina lake,’ wanapaswa kujua kweli kumhusu. (Zab. 96:4, 8) Hata hivyo, watu fulani wanakana kuwako kwa Mungu. (Zab. 14:1) Wengine wanamsengenya kuwa asiye na nguvu, au wanadai kwamba yeye hapendezwi na mambo ya wanadamu. Tunaposaidia wenye mioyo minyoofu kupata ujuzi sahihi kuhusu Muumba wetu, makusudi yake, na utu wake wenye kuvutia, tunamtukuza Yehova.
4 Kupitia Mwenendo Wetu: Tunamheshimu Yehova kwa kuishi kulingana na viwango vyake vyenye uadilifu. Mwenendo wetu bora haukosi kuonekana. (1 Pet. 2:12) Kwa mfano, mvalio wetu safi na kujipamba kwetu vinaweza kuchochea wengine watoe maelezo yenye kufaa, hilo likitutolea nafasi ya kuzungumza kuhusu faida za kuishi kulingana na kanuni zilizo katika Neno la Mungu. (1 Tim. 2:9, 10) Sisi ni wenye kupendezwa kabisa wakati wengine ‘wanaona matendo yetu mazuri na kumpa utukufu Baba yetu aliye mbinguni.’—Mt. 5:16.
5 Kupitia usemi wetu na matendo yetu, na tumsifu Mungu wetu mtukufu kila siku tukiitikia mwito huu wenye shangwe: “Mwimbieni Yehova, libarikini jina lake. Tangazeni habari njema za wokovu wake siku baada ya siku.”—Zab. 96:2.