“Ukombozi Unakaribia”—Mkusanyiko wa Wilaya wa Mashahidi wa Yehova wa 2006
1. Watu wa Mungu walionyesha namna gani uthamini wao kuhusu ibada ya kweli katika nyakati za kale, nasi tuna nafasi gani yenye kufanana na hiyo siku hizi?
1 Mfalme Hezekia wa Yuda la kale alitumia wakimbiaji wapeleke barua za kuita watu wakusanyike pamoja katika Yerusalemu. (2 Nya. 30:6, 13) Itikio la watu lilifunua mtazamo wao kuelekea ibada ya kweli. (2 Nya. 30:10-12) Katika miezi ijayo, watumishi wa Yehova wa siku hizi watakuwa na nafasi inayofanana na hiyo ili kuonyesha uthamini wao wa kutoka moyoni kuhusu pendeleo la kukusanyika pamoja ili kumwabudu Yehova. Barua ya kuwaalika kuhudhuria Mkusanyiko wa Wilaya wenye kichwa “Ukombozi Unakaribia” imekwisha kutumwa kwenye kutaniko lenu. Wewe utaitikia mwaliko huo namna gani?
2. Ni jambo gani tunaloweza kufanya sasa ili tufaidike kikamili na mkusanyiko?
2 Fanyeni Mipango Sasa: Ili tufaidike kikamili na programu hiyo ya kiroho inayotayarishwa kwa upendo, tunahitaji kuwapo muda wa programu nzima. Tumia hekima ili kuanza kufanya sasa mipango yoyote yenye kuhitajiwa ili wewe na familia yako mhudhurie siku zote tatu. (Met. 21:5) Matayarisho kama hayo yanaweza kutia ndani kuomba bwana wako wa kazi mapumziko, kuzungumzia mipango yako na mwenzi wako asiyeamini, kusaidia wanafunzi wako wa Biblia wahudhurie kila siku. Usingojee dakika ya mwisho ili kufanya mambo hayo ya lazima. Badala yake, sali kwa Yehova kuhusu mambo hayo, ukitumaini kwamba: ‘yeye mwenyewe atatenda.’—Zab. 37:5.
3. Kwa nini tunapaswa kufuata kikamili mipango ambayo imefanywa kwa ajili ya upangishaji wetu?
3 Tengenezo la Yehova limefanya kazi kwa bidii ili kuhakikisha kwamba nafasi za upangishaji za kutosha zinapatikana katika kila mji wa mkusanyiko. Shukrani zetu kwa ndugu wanaofanya kazi kwa bidii na kujidhabihu wakisaidia katika kufanya mipango hiyo, ufikirio kwa wahudhuriaji wenzetu, na kuheshimu utaratibu wa kitheokrasi vinapaswa kutuchochea tufuate kikamili miongozo yenye kutolewa katika makala hii.—1 Kor. 13:5; 1 The. 5:12, 13; Ebr. 13:17.
4-6. (a) Ni mambo gani ya maana unayopaswa kulinda akilini unapohitaji kupangishwa, na kwa nini? (b) Ni mipango ya aina gani inayopaswa kuchukuliwa ikiwa ndugu na dada wanapangishwa katika Jumba la Ufalme? (c) Ni mambo gani fulani unayopaswa kufikiria unapopanga kuhudhuria Mkusanyiko wa Wilaya (Ona kisanduku kwenye ukurasa wa 4.)
4 Upangishaji: Upangishaji katika mji wa mkusanyiko unafanywa kwa kawaida katika nyumba za ndugu, katika Majumba ya Ufalme au katika nyumba za washiriki wa jamaa. Orodha ya mahali pote ambako mkusanyiko utafanywa itawekwa kwenye ubao wa matangazo wa kutaniko baada ya kuchunguza nyongeza hii kwenye Mkutano wa Utumishi. Inapendekezwa kwamba wote wafikirie katika sala mahali ambapo watahudhuria mkusanyiko mnamo mwaka wa 2006.
5 Ikiwa ungependa kupangishwa katika nyumba ya ndugu, au katika Jumba la Ufalme, tunapendekeza kwamba mwandishi afanye orodha ya wahubiri wote wanaoomba kupangishwa na kuituma kwenye Idara ya Upangishaji katika mji wa mkusanyiko mapema vya kutosha. Katika orodha hiyo, anapaswa kujulisha jina, aina (mume au mke), umri, na uhusiano wa kifamilia wa kila mhubiri. Hilo litaruhusu ndugu wanaoshughulika na Idara ya Upangishaji wapate wakati wa kutosha ili kupata mahali pa kupangisha wote. Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko inapaswa kuchunguza sifa za mhubiri kabla ya kutuma maombi hayo kwenye Idara ya Upangishaji. Mara tukiisha kutolewa mahali pa kupanga, halitakuwa jambo lenye kufaa kufanya kisha hapo mipango ya kibinafsi ili kwenda kukaa pamoja na ndugu au rafiki mwingine. Jambo hilo linaweza kufanya kazi iwe ngumu zaidi kwa wale wanaoshughulika na Idara ya Upangishaji. Hata hivyo, ikiwa yeyote anakusudia kukaa muda wa mkusanyiko pamoja na mshiriki wa jamaa asiye ndugu wa kiroho, hapaswi kuomba mwandishi kutia jina lake kwenye orodha ya wenye kuhitaji upangishaji.
6 Upangishaji Katika Jumba la Ufalme: Tunawatolea maagizo fulani hapa kuhusu namna ya kushughulikia upangishaji katika Jumba la Ufalme. Halmashauri ya Mkusanyiko wa Wilaya itatoa mgawo kwa mzee mmoja ili asimamie mpango huo. Atakuwa na msaidizi, kwa kawaida mzee mwingine au mtumishi wa huduma mwenye sifa za kiroho. Jumba linapaswa kugawanywa katika sehemu mbili: sehemu moja kwa ajili ya akina dada na watoto wao, kama vile wasichana, na sehemu nyingine kwa ajili ya akina ndugu na washiriki wengine wa kiume. Jumba la Ufalme litatumiwa kwa ajili ya kulala tu. Wote wanapokuwa mahali pa mkusanyiko mchana, kazi ya ulinzi itapangwa kwa kupeana zamu ili kuzuia wizi wa vitu vya ndugu. Ndugu wenye kujiheshimu, wenye sifa za kiroho ndio wanaopaswa kutumiwa ili kufanya kazi ya ulinzi. Haitaruhusiwa kupikia chakula ndani ya Jumba la Ufalme. Kibanda cha muda kinaweza kujengwa katika uwanja, ili kitumiwe kuwa mahali pa kupikia muda wa mkusanyiko tu. Mwishoni mwa mkusanyiko kibanda hicho kitabomolewa. Ni jambo la maana kwamba jumba, na vilevile uwanja, vilindwe katika hali ya usafi na utaratibu. Inafaa kuwa waangalifu ili kitu chochote kisiharibiwe. Wale wanaokaa katika jumba watafanya yote wawezayo ili waonyeshe mwenendo unaostahili Wakristo wa kweli kati yao wenyewe na vilevile kuelekea majirani.—1 Kor. 10:31.
7. Wale walio na mahitaji ya pekee wanaweza kushughulikiwa namna gani?
7 Mahitaji ya Pekee: Methali 3:27 inasema: “Usiwanyime watu mema wanayostahili, mkono wako ukiwa na uwezo wa kuyafanya.” Unaweza kufanya mema kwa wengine namna gani kuhusiana na mkusanyiko? Wahubiri walio wazee-wazee, walemavu, wale walio katika utumishi wa wakati wote, na wengine wanaweza kuhitaji msaada halisi kwa ajili ya usafirishaji au upangishaji. Washiriki wa jamaa ndio wanalo daraka la kwanza la kushughulikia mahitaji ya watu kama hao. (1 Tim. 5:4) Ikiwa hawawezi kufanya hivyo, waamini wenzao wanaweza kuwasaidia. (Gal. 6:10) Waangalizi wa funzo la kitabu wanapaswa kuchunguza ikiwa kuna wale walio na mahitaji ya pekee katika vikundi vyao ili wahakikishe kwamba mipango kuwahusu imechukuliwa kimbele kabisa kabla ya mkusanyiko.
8. Kwa nini tunapaswa kuhudhuria mkusanyiko wa mahali ambapo kutaniko letu limealikwa?
8 Kuhudhuria Mkusanyiko Mahali Pengine: Ili kuhakikisha kwamba kuna viti, vichapo, vyumba vya kupangia vya kutosha, na kadhalika, unatiwa moyo kuhudhuria mkusanyiko wa mahali ambapo kutaniko lenu limealikwa. Hata hivyo, ikiwa hali zako hazikuruhusu uhudhurie mkusanyiko wa mahali ambapo kutaniko lenu limealikwa, tafadhali unaweza kuhudhuria mkusanyiko wa mahali pengine.
9. Ni katika njia moja gani tunaweza kuchangia katika furaha ya mkusanyiko unaokaribia?
9 Wajitoleaji Wenye Kujipendea: Bila shaka, wale wote wenye kuhudhuria mkusanyiko na wanaofaidika na chakula cha kiroho na ushirika wenye kujenga, watakuwa na furaha nyingi. Furaha yetu itakuwa nyingi zaidi ikiwa tunajitolea kusaidia katika kazi zinazopaswa kufanywa ili mkusanyiko ufanikiwe. (Mdo. 20:35) Karibuni Halmashauri za Mkusanyiko zitaalika wengine ili wasaidie katika kazi hiyo. Je, unaweza kuwa tayari?—Zab. 110:3.
10. Ni jambo gani unalothamini kuhusu mkusanyiko wa wilaya wa kila mwaka, na adhimio letu linapaswa kuwa gani?
10 Alipohudhuria Mkusanyiko wa Wilaya, mvulana mwenye umri wa miaka 5 alisema: “Mkusanyiko wa Wilaya ni sehemu ninayopendelea ya kumwabudu Yehova.” Maelezo hayo ya kutoka moyoni yanatusaidia sisi wote kuelewa jinsi tunavyofurahia kuhudhuria mkusanyiko wetu wa wilaya wa kila mwaka. Tunaona ukweli wa maneno aliyoimba mtunga-zaburi: “Kwa maana siku moja katika nyua zako ni bora kuliko siku elfu moja kwingineko.” (Zab. 84:10) Daudi alieleza katika wimbo tamaa yake ya ‘kukaa katika nyumba ya Yehova siku zote za maisha yake ili kulitazama kwa uthamini hekalu la Yehova.’ (Zab. 27:4) Daudi alipendezwa sana kukaa pamoja na waabudu wa Yehova. Je, tunaweza kuiga uthamini wake kuelekea ibada ya kweli kwa kuhudhuria kwa muda wote wa siku tatu Mkusanyiko wa Wilaya wenye kichwa “Ukombozi Unakaribia”?
[Kisanduku kwenye ukurasa wa 3]
Saa za Programu
Siku ya Tano na Siku ya Posho
3:30 asubuhi - 11:05 kisha mchana-kati
Siku ya Yenga
3:30 asubuhi - 10:10 kisha mchana-kati
[Kisanduku kwenye ukurasa wa 4]
Mambo fulani ya kufikiria unapotazamia kuhudhuria Mkusanyiko wa Wilaya
1. Ikiwa unahitaji kufanya safari ndefu ili kuhudhuria mkusanyiko, hivyo basi anza kuchunga fedha mapema iwezekanavyo ili uhakikishe kwamba utapata fedha za lazima za usafirishaji na chakula kwa ajili yako mwenyewe na familia yako pia.
2. Fikiria pia kutegemeza mipango ya mkusanyiko kupitia zawadi zako za kujipendea. ‘Mtu yeyote asionekane mbele za Yehova mikono mitupu,’ lakini pia ‘Mweshimu Yehova kwa vitu vyako vyenye thamani.’—Kum. 16:16; Met. 3:9.
3. Wakati wa mkusanyiko, tunatukuza jina la Yehova kupitia mwenendo wetu mzuri na mavazi safi na yenye heshima.—1 Kor. 10:31.
4. Azimia kushirikiana na wakaribishaji na ndugu wengine wenye kuwa na daraka la kulinda utaratibu. Usichunge viti bure, isipokuwa kwa ajili ya washiriki wa karibu wa familia yako au wale wanaosafiri pamoja nawe.
5. Ili ufaidike kikamili na kipindi cha kisha mchana-kati, angalia kwamba ule tu chakula chepesi mwishoni mwa kipindi cha asubuhi. Chakula kizito kinaweza kuleta usingizi.—Luka 8:18.
6. Usafi unamheshimisha Yehova. Mwishoni mwa kila kipindi, kila mmoja wetu anaweza kutimiza fungu lake ili kuacha mahali pa mkusanyiko pakiwa safi kwa kuokota vikaratasi na takataka nyingine na kuzitupa katika mapipa ya kutupia takataka yaliyotayarishwa kwa kusudi hilo.—1 Pet. 1:15, 16.