“Utii wa Kimungu”—Mkusanyiko wa Wilaya wa Mashahidi wa Yehova wa 2005
1 Akiwa Mfundishaji Mkuu wetu, Yehova Mungu anatayarisha kwa ajili yetu mkusanyiko huu ili tufundishwe katika njia zake. (Isa. 30:20, 21; 54:13) Anafanya hivyo kupitia jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara, inayofanya mipango kuhusu mikutano kama vile mikusanyiko yetu ya wilaya ya kila mwaka. (Mt. 24:45-47) Tunajisikia kama mtunga zaburi Daudi, aliyeimba: “Kati ya makundi yaliyokutanika nitambariki Yehova.” (Zab. 26:12) Daudi alielewa waziwazi thamani ya kufunzwa na Yehova na aliazimia kuwa kati ya watu Wake wakati wowote ule wanapokusanyika pamoja.
2 Je, utakuwa kati ya “makundi yaliyokutanika” ya wale ambao watahudhuria Mkusanyiko wa Wilaya wenye kichwa “Utii wa Kimungu” mwaka huu? Ikiwa ndivyo, habari zifuatazo zitakusaidia katika kufanya matayarisho ya kuhudhuria.
3 Panga Sasa Kuhudhuria Kila Siku: “Mipango ya mwenye bidii bila shaka huleta faida.” (Met. 21:5) Je, maneno hayo hayakazii thamani ya kufanya mipango bila kuchelewa ili kuhudhuria mkusanyiko? Ili kuwa hakika kwamba hautakosa sehemu yoyote ya programu yenye kuburudisha kiroho, kwa hekima anza tangu sasa kufanya mipango yoyote inayohitajiwa ili uhudhurie siku zote hizo tatu. Ikiwa unahitaji kuomba bwana wako wa kazi wakati wa mapumziko, fanya hivyo tangu sasa. Ikiwa unahitaji kuzungumzia mipango yako pamoja na mwenzi wako asiyeamini, usingoje mpaka dakika ya mwisho. Sali kwa Yehova kuhusu magumu yoyote yale unayopambana nayo, ukiwa na tumaini kwamba kupitia msaada wake “mipango yako itafanywa imara.” (Met. 16:3) Kwa kuongezea, ingekuwa vema kusaidia wanafunzi wako wa Biblia kufanya matayarisho ili wawe hapo kwenye kila sehemu ya mkusanyiko.
4 Upangishaji: Mipango kuhusu upangishaji kwenye mji wa mkusanyiko inafanywa kwa kawaida katika nyumba za akina ndugu, katika Majumba ya Ufalme au katika nyumba za washiriki wa familia. Orodha yenye kuonyesha mahali pote pa mkusanyiko itawekwa kwenye ubao wa matangazo wa kutaniko baada ya kuchunguza nyongeza hii kwenye Mkutano wa Utumishi. Inapendekezwa kwamba kila mtu afikirie katika sala mahali atakapohudhuria mkusanyiko mnamo 2005. Ikiwa ungependa kupangishwa katika nyumba ya ndugu au katika Jumba la Ufalme, tunapendekeza kwamba mwandishi afanye mapema vya kutosha orodha ya wahubiri wote wanaoomba kupangishwa na kuituma kwa Idara ya Upangishaji katika mji wa mkusanyiko. Anapaswa kuonyesha jina la yule anayeomba kupangishwa, ikiwa ni mume au mke, umri wake na uhusiano wake wa kifamilia. Hilo litasaidia akina ndugu wanaohusika na Idara ya Upangishaji wawe na wakati wa kutosha ili kupata mahali pa kupangisha wote. Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko inapaswa kuchunguza sifa za mhubiri kabla ya kutuma maombi hayo kwenye Idara ya Upangishaji. Baada ya kupewa mahali pa kupanga, halitakuwa jambo lenye kufaa wakati huo kufanya mipango ya kipekee ili kuenda kukaa kwa ndugu au kwa rafiki mwingine. Hilo lingefanya kazi ya wale wanaohusika na upangishaji iwe ngumu zaidi. Hata hivyo, ikiwa muda wa mkusanyiko ndugu au dada anakusudia kupanga kwa mshiriki wa familia ambaye si ndugu wa kiroho, hapaswi kujaza na kutuma fomu ya kuomba kupangishwa.
5 Upangishaji Kwenye Jumba la Ufalme: Tunatoa hapa maagizo fulani kuhusu upangishaji kwenye Jumba la Ufalme. Halmashauri ya Mkusanyiko wa Wilaya itatoa mgawo kwa mzee mmoja ili asimamie mpango huo. Atakuwa na msaidizi, kwa kawaida mzee mwingine au mtumishi wa huduma mwenye sifa za kiroho. Jumba linapaswa kugawanywa katika sehemu mbili. Sehemu moja kwa ajili ya akina dada na watoto wao, na wasichana pia. Sehemu nyingine kwa ajili ya akina ndugu na washiriki wengine wa kiume. Jumba la Ufalme litatumiwa tu kuwa mahali pa kulala. Wote wanapokuwa hawako mahali pa mkusanyiko mchana, kazi ya kufanya ulinzi itapangwa kwa kupeana zamu ili kuzuia wizi wa vitu vya ndugu. Ndugu wenye kujiheshimu na wenye sifa za kiroho wanapaswa kutumiwa ili kufanya ulinzi huo. Haitaruhusiwa kupikia chakula katika Jumba la Ufalme. Kibanda cha muda kinaweza kujengwa katika kiwanja ili kitumiwe kuwa mahali pa kupikia chakula wakati wa mkusanyiko tu. Mwishoni mwa mkusanyiko, kibanda hicho kitabomolewa. Ni jambo la maana kwamba jumba na uwanja vilindwe vikiwa safi na vyenye utaratibu. Inafaa kuwa waangalifu ili jambo lolote lisiharibiwe. Wale wanaokaa katika jumba watafanya yote wawezayo ili kuonyesha mwenendo unaostahili Wakristo wa kweli, wenyewe kwa wenyewe na kuelekea majirani.—1 Kor. 10:31.
6 Mahitaji ya Pekee: Mtume Paulo alieleza kwamba ndugu fulani walikuwa ‘msaada wenye kumtia nguvu.’ (Kol. 4:7-11) Njia moja ambayo katika hiyo walisaidia ilikuwa kwa kumtimizia Paulo mahitaji yake ya kipekee. Unawezaje kuwa ‘msaada wenye kutia nguvu’ kwa wengine kuhusiana na mkusanyiko huu? Wahubiri walio wazeewazee, walemevu, wale walio katika utumishi wa wakati wote, na wengine, wanaweza kuhitaji msaada halisi wa usafirishaji au upangishaji. Watu wa jamaa wanalo daraka la kwanza la kushughulikia watu wa aina hiyo. (1 Tim. 5:4) Ikiwa hawawezi kufanya hivyo, waamini wenzao wanaweza kuwasaidia. (Yak. 1:27) Waangalizi wa funzo la kitabu wanapaswa kuchunguza ikiwa katika kikundi chao kuna wale walio na mahitaji ya pekee ili kuhakikisha kwamba mipango kuwahusu imechukuliwa kimbele kabisa kabla ya mkusanyiko.
7 Kuhudhuria Mkusanyiko Mwingine: Ili kuhakikisha kwamba kuna viti, vichapo, vyumba vya kupangia vya kutosha, na kadhalika, wahubiri wanatiwa moyo kuhudhuria mkusanyiko ambao kutaniko lao limealikwa. Ikiwa hali zinaomba uhudhurie mkusanyiko mahali pengine, tafadhali umwone mwandishi wa kutaniko lenu.
8 Wajitoleaji Wanahitajiwa: Yesu alitoa mfano mkamilifu katika kushughulikia kwa unyenyekevu mahitaji ya wengine. (Luka 9:12-17; Yoh. 13:5, 14-16) Wale ambao wanajitolea ili kutumika kwenye mikusanyiko wanaonyesha roho ileile. Ili kutimiza mahitaji ya idara za mkusanyiko, karibuni Halmashauri za Mkusanyiko zitaalika wengine kutumika pamoja nao. Kuna uhitaji hasa wa wazee kujitolea na kukubali migawo. Roho yao ya kujitolea inatoa mfano bora kwa wote katika kutaniko.—1 Pet. 5:2, 3.
9 Mambo Ambayo Wengine Wanaona: Mkubwa mmoja wa hoteli alisema: “Ninyi ni kikundi tunachopenda sana. Mnapolinganishwa na kikundi kingine chochote ninyi mnajiendesha vizuri sana. Watunza-nyumba wote wanaeleza jinsi mnavyowatendea vizuri na jinsi wanavyopokea zawadi zenu. Kwa hakika, kila mtu anataka kutumika mwisho-juma mnapokuwa hapa!” Mwakilishi mwingine wa hoteli alieleza: “Mashahidi wa Yehova ndicho kikundi rahisi zaidi cha kutumika nacho.” Huenda mfano wako mzuri katika mwenendo wako ulichangia katika taarifa hizo. Fikiria ile furaha aliyo nayo Yehova anapotuona tukitenda katika njia inayoleta sifa kama hiyo!—1 Pet. 2:12.
10 Kupitia “msimamizi-nyumba mwaminifu,” Yehova Mungu amechukua mpango ili watu wake wakusanyike ili kupokea maagizo ya kiroho mwaka huu. (Luka 12:42) Kufanya matayarisho ili kuhudhuria siku hizo tatu kutaomba bidii, lakini ni bidii inayofaa. Hakika, Mkusanyiko wa Wilaya “Utii wa Kimungu” wa mwaka huu utatia nguvu azimio letu la kumtumikia Yehova sasa na hata milele. Na tuazimie kufuata shauri hili la mtunga zaburi: “Katika makundi yaliyokutanika mbarikini Mungu.”—Zab. 68:26.
[Kisanduku Kwenye Ukurasa wa 3]
Saa za Programu
Siku ya Tano na Siku ya Posho
3:30 asubuhi - 11:05 kisha mchana-kati
Siku ya Yenga
3:30 asubuhi - 10:10 kisha mchana-kati
[Kisanduku Kwenye Ukurasa wa 4]
Mambo fulani ya kuchunguza unapofikiria kuhudhuria Mkusanyiko wa Wilaya
1. Ikiwa unapaswa kufanya safari ndefu ili kuhudhuria mkusanyiko, anza kuweka fedha ili kulipia safari yako na ya familia yako na pia chakula chenu.
2. Fikiria pia kutegemeza mipango ya mkusanyiko kupitia zawadi zako za kujipendea. “Mtu yeyote asionekani mbele za Yehova mikono mitupu,” lakini “Mheshimu Yehova kwa vitu vyako vyenye thamani.”—Kum. 16:16; Met. 3:9.
3. Wakati wa mkusanyiko, tunatukuza jina la Yehova kupitia mwenendo wetu mzuri na mavazi safi na yenye heshima.—1 Kor. 10:31.
4. Azimieni kushirikiana na wakaribishaji na ndugu wengine walio na daraka la kulinda utaratibu. Usichunge viti bure, ila tu kwa ajili ya washiriki wa karibu wa familia yako au wale unaosafiri nao.
5. Ili kufaidika kikamili na kipindi cha kisha mchana-kati, angalia kwamba ule tu chakula chepesi mwishoni mwa vipindi vya asubuhi. Chakula kizito kinaweza kuleta usingizi.—Luka 8:18.
6. Usafi unaheshimisha Yehova. Mwishoni mwa kila kipindi cha mkusanyiko, kila mmoja anaweza kutimiza fungu lake ili kuacha mahali pa mkusanyiko pakiwa safi kwa kuokota karatasi na takataka nyingine na kuzitupa katika mapipa ya kutupia takataka yaliyotayarishwa kwa kusudi hilo.—1 Pet. 1:15, 16.