“Mpeni Mungu Utukufu”—Kusanyiko la Wilaya la Mashahidi wa Yehova la 2003
1 Kupitia nabii wake mwaminifu Isaya, Yehova aliamuru: “Munisikilize, watu wangu; na tegeni masikio kwangu, taifa langu.” (Isa. 51:4) Wakati huu wa mwisho wenye hatari zaidi na zaidi, je, hatukubali kwamba kusikiliza amri za Yehova ni jambo la maana zaidi kuliko wakati mwingine wowote? Njia moja ambayo kwa hiyo ‘tunatega sikio’ kwa Yehova ni kwa kuheshimu amri yake ya kukusanyika kwa ajili ya ibada. Tunangojea kama nini nafasi ya pekee ambayo makusanyiko yetu ya wilaya ya kila mwaka yanatoa! Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova limepanga tena makusanyiko mengi ya wilaya yafanyike katika eneo letu mnamo mwaka wa 2003.
2 Kama inavyoonyeshwa katika toleo la Mnara wa Mlinzi wa Julai 1, 2002, makusanyiko ya kimataifa yatafanyika pia katika miji fulani-fulani, yakihudhuriwa na wajumbe kutoka ulimwenguni pote. Kwa kuwa hesabu ya miji ambako makusanyiko ya kimataifa yatafanyika ni ndogo, makutaniko yaliyoagizwa kuhudhuria makusanyiko hayo tu ndiyo yatakayoweza kuhudhuria. Lakini hali ya kimataifa itahisiwa kwenye makusanyiko yote ya wilaya. Wamishonari watakuwa kwenye makusanyiko katika mahali pengi, na kutakuwa na nafasi ya kusikiliza mambo fulani yaliyoonwa nao. Tunaweza kufanya nini ili kufaidika kikamili na mipango inayochukuliwa sasa kuhusiana na makusanyiko yetu?
3 Hudhuria Kila Siku: Ili kufaidika kikamili na mafundisho yanayoandaliwa kupitia jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara, tunataka kuhakikisha kwamba tutakuwako muda wa programu nzima. (Mt. 24:45) Je, unahitaji kumwomba bwana wako wa kazi mapumziko ili uhudhurie kila siku ya kusanyiko? Kabla ya Nehemia kuomba Mfalme Artashasta ruhusa ya kwenda Yerusalemu ili kujenga upya kuta, ‘aliomba Mungu wa mbinguni.’ (Neh. 2:4) Unapaswa hivyohivyo kumwomba Yehova ujasiri wa kuomba bwana wako wa kazi mapumziko ili kuhudhuria siku tatu zote za kusanyiko. Namna gani ikiwa bwana wako wa kazi anakataa kukupa mapumziko? Labda kumweleza kwamba mafundisho tunayopokea kwenye makusanyiko yetu yanatusaidia kuwa wafanyakazi wanyofu, wenye juhudi, na wenye kutumainika kunaweza kumsaidia aitikie ifaavyo. Zaidi ya hiyo, ikiwa tuna washiriki wa familia ambao si waamini, lingekuwa jambo lenye upendo kuwajulisha kuhusu mipango yetu ya kusanyiko mapema zaidi iwezekanavyo.
4 Upangishaji: Mipango imechukuliwa ili wajumbe wanaohitaji mahali pa kupanga wapangishwe hasa kwa watu binafsi. Tunapaswa kuwa wenye shukrani kwa ndugu watakaotukaribisha katika nyumba zao. Zaidi ya hayo, halingekuwa jambo lenye kufaa kwa wale wanaoonyeshwa ukaribishaji kama huo kuutumia vibaya kwa kuomba wapangishwe muda mrefu kabla au baada ya kusanyiko. Upangishaji unatolewa tu muda wa kusanyiko. Wale wanaofaidika na mpango huo wanapaswa kuheshimu mali ya yule anayewapangisha, kutoharibu kitu chochote, kutokwenda mahali wasipoalikwa, na kuangalia kwamba watoto wao wafanye hivyohivyo. Ikiwa wapangishaji fulani wanakabiliana na tatizo lolote upande huo, wanapaswa mara moja kujulisha Idara ya Upangishaji, ambayo itafurahi kuwatolea msaada. Kazi nzuri na matokeo mazuri ya idara ya upangishaji vinategemea ushirikiano wa kila mmoja. Tumepata ripoti kwamba wengine huacha kwa kutaka kwao wenyewe mahali walipopangishwa ili kwenda mahali pengine kunakopatikana labda rafiki au mtu mwingine wanayejuana naye. Hilo linafanya kazi ya akina ndugu wa Idara ya Upangishaji kuwa ngumu. Tunaomba wote washirikiane na idara hiyo.
5 Hakuna shaka kwamba Yehova anatoa utegemezo wake kwa kile kinachofanywa kwa ajili ya makusanyiko yetu ya kila mwaka. Kwa kuwa ndugu wengi wanaosafiri ili kuhudhuria kusanyiko la wilaya wanahitaji mahali pa kupangishwa, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atatosheleza ifaavyo mahitaji yao. Kwa kuwa mambo hayo yanahusiana na ibada ya kweli, tunapaswa kufuata kwa furaha maagizo yoyote yanayotolewa. Acheni tuonyeshe kwamba sisi ni waaminifu katika lililo dogo zaidi; hivyo tutaweza kupokea baraka tele zinazongojea wale wanaopendwa na Yehova.—Luka 16:10.
6 Tazama Pote Katika Kutaniko: Ikiwa tunajua kwamba ndugu au dada fulani ana uhitaji wa kimwili ambao unaweza kufanya iwe vigumu kwake kuhudhuria kusanyiko, je, tunaweza ‘kupanuka’ katika upendo wetu na kutoa msaada fulani? (2 Kor. 6:12, 13; Kum. 15:7) Hiyo ndiyo roho ambayo Paulo alichochea kwenye 2 Wakorintho 8:14. Kwa nini usialike watu kama hao wasafiri nawe kwenda kwenye kusanyiko? Ikiwa wao ni mapainia, yaelekea wana mambo mengi yaliyoonwa ya kushiriki nawe mnaposafiri. Ikiwa wao ni washiriki wa kutaniko wenye umri mkubwa, huenda wakawa na historia nzuri ajabu ya kitheokrasi ambayo haujapata kamwe kusikia. Je, kushirikiana na ndugu na dada kama hao hakutakuwa na uvutano mzuri juu yako na familia yako? Roho yako ya ukarimu itathaminiwa nao, nayo itathawabishwa na Yehova.—Mez. 28:27; Mt. 10:42.
7 Ingawa wale walio na mahitaji ya pekee hushughulikiwa kwanza na washiriki wa familia zao walio Wakristo, wazee na wengine katika kutaniko wanaojua mahitaji kama hayo wanaweza kwa upendo kusaidia katika kuchukua mipango. (1 Tim. 5:4) Wakati barua za Ombi la Chumba kwa Ajili ya Mahitaji ya Pekee zinapotolewa kwa Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko, halmashauri inapaswa kuchunguza sifa za kila mtu anayetoa ombi kabla ya kutuma maombi hayo kwenye Idara ya Upangishaji.
8 Itikia kwa Utayari Kuwa Mfanyakazi wa Kujitolea: Wakati wa kusanyiko, mamia ya wafanyakazi wa kujitolea husaidia kuendesha vizuri zile idara mbalimbali. Wakaribishaji wanaotumikia mahali wanapokaa wasikilizaji na mahali pa kuegeshea magari hutoa mwelekezo kuhusiana na viti, nao huchunga magari yetu na makinga yetu wakati wa mchana. Idara ya Usafi inalo pendeleo la kulinda sifa tuliyo nayo ya kuwa safi, ikiacha mahali petu pa ibada pa muda pakiwa safi kuliko jinsi tulivyopakuta. Je, tunaweza kusaidia idara hizo au zingine zinazoweza kutumia utegemezo wetu? Je, utakuwa mfanyakazi wa kujitolea ili kutumikia “bega kwa bega” pamoja na ndugu zako?—Zef. 3:9, NW.
9 Kwa kuwa “mandhari ya ulimwengu huu inabadilika,” tunahitaji makusanyiko yetu ya wilaya ili yatusaidie tubaki waangalifu kiroho. (1 Kor. 7:31) Kuchukua mipango ili kuhudhuria kila siku kutaomba jitihada, lakini jitihada hiyo ni yenye kufaa. Kusanyiko la Wilaya la mwaka huu lenye kichwa “Mpeni Mungu Utukufu” limetayarishwa ili kutusaidia tubaki imara tunapongojea kutekelezwa kwa hukumu ya Yehova juu ya ulimwengu wa Shetani. Tusiache kitu chochote kituzuie kupokea mafundisho ambayo Yehova ametayarisha kwa ajili yetu.—Isa. 51:4, 5.
[Kisanduku kwenye ukurasa wa 3]
Saa za Programu
Siku ya Tano na Siku ya Posho
3:30 - 11:00
Siku ya Yenga
3:30 - 10:05
[Kisanduku kwenye ukurasa wa 4]
Mipango Fulani ya Kuchukua kwa Ajili ya Kuhudhuria Kusanyiko la Wilaya Lenye Kichwa “Mpeni Mungu Utukufu”
1. Ikiwa unapaswa kutembea mwendo mrefu ili kuhudhuria kusanyiko, anza kuweka akibani fedha ili kulipia safari yako na ya familia yako, na pia chakula chenu.
2. Fikiria pia kutegemeza matayarisho ya kusanyiko kupitia zawadi zako za kujitakia. ‘Usitokee mbele ya Yehova na mikono mitupu,’ lakini ‘mheshimu Yehova kwa vitu vyako vya thamani.’—Kum. 16:16; Mez. 3:9.
3. Tunatukuza pia jina la Yehova kwa kuwa na mwenendo mzuri na mavazi safi na yenye kufaa wakati wa mikusanyiko.—1 Kor. 10:31.
4. Azimieni kushirikiana na akina ndugu wanaoshughulika na utaratibu. Usichunge nafasi bure, ila tu kwa ajili ya washiriki wa familia yako au wale unaosafiri nao.
5. Wakati wa mapumziko, angalia kwamba ule chakula chepesi kusudi uweze kufaidika kikamili na vipindi vya kisha mchana-kati. Chakula kizito huleta usingizi.—Luka 8:18.
6. Usafi humheshimisha Yehova. Baada ya kila kipindi cha kusanyiko, kila mmoja atataka kutimiza fungu lake ili kuacha mahali pa kusanyiko pakiwa safi kwa kuokota karatasi na mambo mengine yenye kufanana na hayo kusudi hayo yatupwe katika mapipa ya kutupia takataka yaliyotayarishwa kwa kusudi hilo.—1 Pet. 1:15, 16.