“Watendaji wa neno la mungu”—mkusanyiko wa wilaya 2000 wa mashahidi wa Yehova
1 “Nitakushukuru katika kusanyiko kubwa; nitakusifu katikati ya watu wengi.” (Zab. 35:18) Fikiria jinsi Daudi angesisimuka leo kuona maelfu mengi sana yakikusanyika pamoja kwa amani ili kutwaa maagizo ya kimungu kwenye mikusanyiko ya majira ya kiangazi! Je! ulikuwa kati ya wale zaidi ya 250,000 waliohudhuria mmoja wa Mikusanyiko ya Wilaya “Neno la Mungu la Kiunabii”? Kuanzia katikati ya Julai hadi sehemu ya mwisho ya Agosti 1999, jumla ya mikusanyiko 77 ilipangwa kufanywa katika miji 69 kuzunguka Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo na Congo-Brazzaville.
2 Kwenye Zaburi 122:1, mtunga-zaburi alisema kwa mkazo: “Nilifurahi wakati waliponiambia: ‘Twende kwa nyumba ya BWANA.’” Ni hakika kwamba wewe ulikuwa na furaha hiyohiyo wakati ulipopokea nyongeza ya Huduma Yetu ya Ufalme iliyotangaza mkusanyiko wa wilaya. Bila shaka unakumbuka mambo mazuri uliyojifunza kwenye mkusanyiko huo. Katika karne ya kwanza, mtume Petro alikumbusha Wakristo kwamba wangefanya vema kwa kukaza uangalifu kwa neno la kiunabii likiwa kama vile “taa yenye kung’aa mahali penye giza.” (2 Pet. 1:19) Jambo hilohilo ni kweli kwetu leo. Tukiwa wenye kuishi katika ulimwengu ulio katika uweza wa Shetani, sisi ni wenye shukrani kuona tumeitwa kutoka katika giza la kiroho. (Kol. 1:13; 1 Pet. 2:9; 1 Yn. 5:19). Ili kuendelea kutembea katika nuru, tunahitaji imani yenye nguvu inayopatikana kwa kukaza uangalifu kwa Neno la Yehova lililopuliziwa. Hivyo ndivyo mkusanyiko wa wilaya ulitutia moyo kufanya.
3 Je! matarajio ya wale waliohudhuria mkusanyiko yalitimizwa? Je! programu hiyo ilitimiza kusudi lake? Maelezo yaliyotolewa na wengi yanaonyesha kwamba kwa kweli programu hiyo ilikuwa yenye kufaa kwa ajili ya nyakati tunamoishi. Elezo moja lilisema: “Programu hiyo itanisaidia niendelee kuangalia hali yangu ya kutokamilika ili niweze kungojea siku ya Yehova nikiwa bila doa kutokana na ulimwengu.” Ndugu mmoja ambaye amekuwa katika kweli kwa siku nyingi alisema: “Programu hii inatutia kwenye njia ifaayo. Inatusaidia kuona ikiwa tungali katika njia iliyo sawa.” Ndugu mwingine alisema: “Nikifikiria yale magumu makubwa sana tunayovumilia sasa, sikufikiri ningeweza kuhudhuria mkusanyiko kama huu. Huo ulionyesha kwamba kwa kweli sisi ni wenye umoja katika imani ijapokuwa umbali unaotutenganisha. Yehova ni mkarimu; yeye ndiye upendo kwelikweli. Yeye anatujali.” Je! tunasikitikia jitihada tulizofanya ili kuhudhuria mkusanyiko mwaka huu? Bila shaka hapana.
4 Mikusanyiko yetu ya wilaya mnamo 2000 itatutolea nafasi mpya za kukusanyika pamoja na wasifaji wenzetu wa Yehova ambao ni “wenye kuona uhitaji wao wa kiroho,” wenye furaha na wenye hamu ya ‘kusikia lile ambalo roho huyaambia makutaniko.’—Mt. 5:3; Ufu. 2:29.
5 Je! Utakuwako? Panga mambo tangu sasa. Azimia kuhudhuria zile siku tatu za karamu hii tamu ya kiroho, kuanzia wimbo wa kwanza hadi sala ya kumalizia. Katika hali zilizo nyingi, unaalikwa kuhudhuria mkusanyiko ulio karibu zaidi na kwenu. Sosaiti inafanya yote iwezayo ili kuwarahisishia nyinyi mambo. Nafasi mpya imeongezwa kwa zile za mwaka uliopita ili kusaidia kila mmoja wetu alishwe kiroho pamoja na familia yake. (Kum. 31:12) Sasa ndio wakati wa kuweka kando fedha kwa ajili ya kulipia safari ya familia yako. Wengine wamefanya jitihada kubwa ili kuhudhuria mikusanyiko ya wilaya mnamo 1999. Kwa mfano, ndugu mmoja alitembea kilometa 300 kwa kinga akiwa na mtoto wake mgongoni hadi mahali pa mkusanyiko. Yeye aliondoka kijiji chake siku tatu baada ya kifo cha mke wake ambaye alikufa wakati wa kuzaa. Baada ya kuacha kitoto mikononi mwa familia ya mke wake ili kukitunza, ndugu huyo alisafiri kwenda kwenye mkusanyiko ambako alitoa hata hotuba yake! Shukrani zetu kwa mipango iliyochukuliwa na Sosaiti zingepaswa kutuchochea tufanye yote tuwezayo ili kuhudhuria mikusanyiko mnamo 2000.
6 Upangishaji: Kwa kawaida, upangishaji hufanywa kwa watu binafsi. Tunapaswa kuonyesha shukrani kwa akina ndugu na dada wanaokubali kutupangisha. Kwa kuongezea, lingekuwa jambo lisilofaa kwa wale wanaopewa ukaribishaji kama huo kuutumia vibaya kwa kuomba wapangishwe muda mrefu kabla au baada ya mkusanyiko. Upangishaji unatolewa tu muda wa mkusanyiko. Wale wanaofaidika na aina hiyo ya upangishaji wanapaswa kuheshimu mali ya yule anayewakaribisha, wasiharibu jambo lolote, wasiende mahali wasikoalikwa, na kuangalia kwamba watoto wao wafanye vivyo hivyo. Ikiwa wakaribishaji fulani wanapambana na tatizo lolote upande huo, wanapaswa mara moja kujulisha idara ya upangishaji, ambayo itakuwa yenye furaha kutoa msaada. Kazi nzuri na matokeo ya idara ya upangishaji vinategemea ushirikiano wa kila mtu. (Ebr. 13:17) Tumepata ripoti kwamba wengine huacha kwa kutaka kwao wenyewe nyumba walimopangishwa ili kwenda mahali pengine kunakopatikana labda rafiki au mtu wanayejuana naye. Hilo hufanya kazi ya akina ndugu wa idara ya upangishaji kuwa ngumu. Tunaomba wote kushirikiana na idara hiyo.
7 Hakuna shaka kwamba Yehova anatoa utegemezo wake kwa kile kinachofanywa kwa ajili ya mikusanyiko ya kila mwaka. Kwa kuwa ndugu wengi wanaosafiri ili kwenda kwenye mkusanyiko wa wilaya wanahitaji mahali pa kupangishwa, tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atatosheleza ifaavyo mahitaji yao. Kwa kuwa mambo hayo yanahusiana na ibada ya kweli, tungepaswa kufuata kwa furaha maagizo yanayotolewa. Acheni tuonyeshe kwamba sisi ni waaminifu katika lililo dogo zaidi; hivyo tutaweza kupokea baraka tele zinazongojea wale wanaopendwa na Yehova.—Luka 16:10.
8 Kushughulikia wale walio na mahitaji ya pekee: Labda wazee-wazee au vilema, watumishi wa wakati wote au wengine wanahitaji msaada ili kuhudhuria mkusanyiko. Ndugu zao wa kimwili, wazee au washiriki wa kutaniko wanaojua hali yao ya pekee, wanaweza kwa upendo kufanya linalohitajiwa, badala ya kutupa daraka lao juu ya ndugu wanaosimamia mkusanyiko.—Ona 1 Timotheo 5:4.
9 Je! Shetani amejaribu kukukengeusha usitoe uangalifu kwa mambo ya kiroho? Kwa kusikitisha, ndugu na dada wengi na familia zao ni wenye kupoteza nafasi ya kupata chakula cha kiroho kilicho cha maana sana. Namna gani? Kwa kutohudhuria vipindi vya mkusanyiko wa wilaya vya Siku ya Tano. Katika hali nyingine, imeonekana kwamba asilimia kubwa ya ndugu zetu ni wenye kukosa kupata maagizo na ushirika wa kiroho ambao vipindi vya Siku ya Tano huandaa.
10 Inawezekana kwamba ndugu fulani-fulani ni wenye kusita kukaribia wakubwa wao wa kazi ili kuomba likizo kwa ajili ya kuhudhuria mkusanyiko. Je! hiyo ndiyo hali yako? Kwa nini usisali kwa Yehova kuhusu jambo hilo na kujipa moyo ili kufasiria hali yako kwa mkubwa wako wa kazi? Kumbuka matokeo mazuri aliyopata Nehemia, aliyekuwa katika hali hiyohiyo. (Neh. 2:1-6) Uwe na imani katika nia ya Baba yetu wa mbinguni ya kukusaidia, ukijua kwamba ikiwa unatia faida za Ufalme pa nafasi ya kwanza, yeye atatimiza mahitaji ya maisha.—Mt. 6:32b, 33.
11 Mikusanyiko yetu ina uvutano gani juu yako? Dada mmoja katika mashariki mwa Shirikisho la Amerika aliandika: “Aksanti sana kwa mkusanyiko wa wilaya 1999. Kushirikiana na ndugu ambao ninaona mara moja tu kila mwaka kunaniletea furaha nyingi. Nilijua kweli nikiwa tineja mwenye mimba, na bado ninakumbuka kwa kupenda sana wakati kiongozi wangu wa funzo la Biblia aliponipeleka kwenye mkusanyiko wangu wa kwanza. Kadiri tulivyoimba wimbo wa Ufalme ‘Ndugu Makumi ya Elfu,’ niliangalia mawingu juu yangu katika uwanja usiofunikwa wa mpira, na nikalia. ‘Kukiwa watu hawa wote wazuri-wazuri kunizunguka,’ nikajiuliza, ‘Yehova anawezaje kunitaka mimi?’ Siku hiyo nikaamua kutumikia Yehova kikamili.” Ni jambo lenye kuchangamsha moyo kama nini! Bila shaka ni jambo lenye kupendeza kushirikiana na watu wa Yehova walio safi, sivyo?
12 Katika sehemu ya mwisho ya siku za mwisho, tunahitaji zaidi kuliko wakati wowote uliopita mkusanyiko wetu wa wilaya. Ni uandalizi kutoka kwa Yehova ili kudumisha afya yetu na usawaziko wetu wa kiroho. Kwa hiyo, uwe mwenye kuazimia kuhudhuria zile siku tatu za Mkusanyiko wa Wilaya wa mwaka huu “Watendaji wa Neno la Mungu.” Unawezaje kutimiza azimio lako? Omba mkubwa wako wa kazi mbele ya wakati likizo kwa ajili ya kuhudhuria mkusanyiko wote. Ikiwa hauna mali nyingi, anza sasa kuweka kando fedha zinazohitajiwa kwa ajili ya kuhudhuria. Mwombe Yehova akusaidie ushinde kitu chochote kinachoweza kukuzuia. Kwa kufanya hivyo, unaweza kutazamia kufurahia ushirika wenye shauku wa ndugu na dada zako na kusikia semi za uhai udumuo milele kutoka kwa Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo, Yehova.—Linganisha Yohana 6:68.
[Box on page 3]
Saa za programu
Siku ya Tano na Siku ya Posho
9:30 – 11:00
Siku ya Yenga
9:30 – 10:00
[Box on page 4]
Mipango fulani ya kuchukua kwa ajili ya kuhudhuria mikusanyiko “watendaji wa neno la Mungu”
1. Ikiwa unapaswa kutembea mwendo mrefu ili kuhudhuria mkusanyiko, anza kuweka kando fedha ili kulipia safari yako na ya familia yako, na pia chakula chenu.
2. Fikiria pia kutegemeza matayarisho ya mkusanyiko kupitia zawadi zako za kujitakia. ‘Usitokee mbele ya Yehova na mikono mitupu,’ lakini ‘mheshimu Yehova kwa vitu vyako vya thamani.’—Kum. 16:16 ; Mez. 3:9.
3. Tunatukuza pia jina la Yehova kwa kuwa na mwenendo mzuri na mavazi safi na yenye kufaa wakati wa mikusanyiko.—1 Kor. 10:31.
4. Azimieni kushirikiana na akina ndugu wanaoshughulika na utaratibu. Usichunge nafasi bure, ila tu kwa ajili ya washiriki wa familia yako au wale unaosafiri nao.
5. Wakati wa mapumziko, angalia kwamba ule chakula chepesi kusudi uweze kufaidika kikamili na vipindi vya kisha mchana-kati. Chakula kizito huleta usingizi.—Luka 8:18.
6. Usafi humheshimisha Yehova. Baada ya kila kipindi cha mkusanyiko, kila mmoja atataka kutimiza fungu lake ili kuacha mahali pa mkusanyiko pakiwa safi kwa kuokota karatasi na mambo mengine yenye kufanana na hayo kusudi hayo yatupwe katika mapipa ya kutupia takataka yaliyotayarishwa kwa kusudi hilo.—1 Petro 1:15, 16.