“Neno la Unabii la Mungu” Kusanyiko la Wilaya la Mashahidi wa Yehova 1999
1 Waisraeli walipokuwa jangwani, Yehova aliamuru Musa atengeneze baragumu mbili za fedha. Ikiwa baragumu moja tu ilipigwa, wakuu wa makabila walipaswa kukutana kwenye mlango wa hema la kusanyiko. Ikiwa zile baragumu mbili zilipigwa, mkutano wote wa Israeli ulipaswa kukutana. (Hes. 10:1-4) Leo, je! sisi si wenye furaha kusikia tangazo linalofanana kidogo na kupigwa kwa baragumu, kuhusu kusanyiko letu la wilaya? Wakati wa makusanyiko yetu, Yehova hutupa maagizo na mashauri kupitia Neno lake na kupitia mawakili wake waliowekwa rasmi. Hilo hufanya iwezekane kwetu kubaki wenye kushikamana na utumishi wa Mungu. Je! sisi si wenye furaha kuona maelfu, labda hata makumi ya maelfu, ya waabudu waaminifu wakikusanyika katika upendo na amani? Bila shaka!—Zab. 122:1, 7, 8.
2 Toka Agosti hadi Septemba 1998, makusanyiko ya wilaya 58 “Njia ya Mungu ya Maisha” yalipangwa katika miji 56 ya eneo letu. Katika Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo, makusanyiko saba hayakufanywa tarehe zilizopangwa kwa sababu ya hali iliyopo katika nchi. Kwa msaada wa Yehova, tunatumaini kufanya yale makusanyiko mengine 7 karibuni. Tunawapongeza kweli kwa ujasiri mlioonyesha kwa kukusanyika ingawa mkazo na mashaka vya wakati huu. Ripoti zinaonyesha kwamba wengi, kutia ndani familia nzima nzima na vilema, walitembea miendo mirefu kwa mguu ili wahudhurie mkusanyiko huo. Wengine walitembea kwa muda wa siku, au hata majuma. Ndugu mmoja kipofu alitembea kilometa 260 kwa mguu ili ahudhurie kusanyiko la wilaya huko Mbuji Mayi. Hivyo ndivyo anavyofanya kila mwaka. Je! jitihada hizo zilizofanywa zilistahili? Bila shaka! Wahudhuriaji wote walikuwa wenye furaha ‘kutiana moyo zaidi sana kadiri waonavyo siku ile kuwa inakaribia.’ Ndugu mmoja alisema: “Kila mtu alitiwa nguvu na mikutano hiyo ya kiroho.” Wakati wa kusanyiko letu la wilaya mnamo 1999, tutakuwa tena na nafasi za kufurahia udugu wetu wenye kupendwa sana na kumshukuru Yehova kwa sababu ya umoja anaotupa.
3 Panga mambo yako kimbele ili uhudhurie kwenye zile siku tatu za karamu tamu ya kiroho, tangu wimbo wa kwanza hadi sala ya mwisho. Mara nyingi, unaalikwa kuhudhuria kusanyiko lililo karibu zaidi na kwako. Kwa upande huo, Sosaiti imejitahidi sana kufanya mambo yawe rahisi kwako. Nafasi mpya nne za kusanyiko zimeongezwa juu ya zile za mwaka uliopita ili kufanya iwezekane kwa kila mmoja wenu kulishwa kiroho pamoja na watu wa familia yake wote. (Kum. 31:12) Nafasi hizo ni Nyabihanga, Burundi; Luiza, Kasai ya Magharibi; Basankusu na Bosondjo, Équateur. Sasa ndiyo wakati wa kufikiria kile utakachoweza kufanya ili kukusanya fedha zinazohitajiwa kwa ajili ya safari yenu wote. Ili kuonyesha shukrani kwa jitihada zilizofanywa na Sosaiti, tunatazamia kwamba kila mmoja atahudhuria kusanyiko ambalo mzunguko wake umealikwa uhudhurie. Hata hivyo, jisikie huru kuhudhuria kusanyiko jingine ikiwa kuna sababu ya maana ya kufanya hivyo.
4 Utakapofanya mipango ya kuhudhuria kusanyiko la wilaya, onyesha upendo kwa kufikiria wale wanaohitaji msaada, zaidi sana wale waliopendezwa na kweli juzijuzi, kusudi wao pia waweko kwenye vipindi vyote vya kusanyiko. Lingekuwa jambo lenye manufaa sana kuchunguza habari zinazopatikana katika makala hii na watu wanaojifunza Biblia pamoja nawe na ambao wanapanga kuhudhuria kusanyiko. (Gal. 6:6, 10) Siku ya Tano na Siku ya Posho, kusanyiko litaanza na muziki pa saa 3:30 na litamalizika pa saa 11:00 hivi. Kipindi cha kusanyiko Siku ya Yenga asubuhi kitaanza pa saa 3:30, na kusanyiko hilo litamalizika pa saa 10:00 hivi. Kupashwa habari ifuatayo kutakusaidia katika kujitayarisha kwako.
5 Upangishaji hufanywa kwa kawaida katika nyumba za watu binafsi. Tunapaswa kuwa wenye shukrani kwa akina ndugu na dada hao wanaokubali kutupangisha. Zaidi ya hayo, halingekuwa jambo zuri kwa wale wanaopewa ukaribishaji huo wautumie vibaya na kuomba wapangishwe wakati mrefu kabla au baada ya kusanyiko. Upangishaji hutolewa tu wakati wa kusanyiko. Wale wanaopangishwa namna hiyo wanapaswa kuheshimu mali ya wapangishaji wao, wasiharibu kitu chochote, wasiende mahali ambapo hawakaribishwi, na waangalie kwamba watoto wao wafanye vivyo hivyo. Ikiwa wapangishaji wanapambana na tatizo lolote upande huo, wanapaswa mara moja kujulisha idara ya upangishaji ambayo itakuwa na furaha kuwasaidia. Kazi nzuri na matokeo mazuri ya idara ya upangishaji vyategemea kushiriki kwa kila mmoja. (Ebr. 13:17) Imeripotiwa kwetu kwamba wengine huacha kwa makusudi nyumba walimopangishwa na kwenda katika nyumba nyingine kunakopatikana rafiki yao au mtu mwingine wanayejuana naye. Jambo hilo hufanya kazi ya akina ndugu wa idara ya upangishaji iwe ngumu. Tunawaomba nyote mshirikiane na idara hiyo.
6 Huenda watu wazee-wazee au vilema, watumishi wa wakati wote au watu wengine wakahitaji kusaidiwa ili wahudhurie kusanyiko. Ndugu zao wa kimwili, wazee au washiriki wa kutaniko wanaojua hali yao ya pekee wanaweza kufanya kwa upendo yale yanayohitajiwa, badala ya kutupa mzigo huo juu ya ndugu wanaosimamia kusanyiko.—Ona 1 Timotheo 5:4.
7 Bila shaka, Yehova hutegemeza yale yanayofanywa kwa ajili ya makusanyiko ya kila mwaka. Kwa kuwa ndugu wengi wanaosafiri ili kwenda kwenye kusanyiko la wilaya wanahitaji mahali pa kupanga, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atatosheleza inavyofaa mahitaji yao. Kwa kuwa mambo hayo yanahusiana na ibada ya kweli, tunapaswa kufuata maagizo tunayopewa. Acheni tuonyeshe kwamba sisi ni waaminifu katika lililo dogo; tutaweza hivyo kupokea faida tele zinazowangoja wale wanaopendwa na Yehova.—Luka 16:10.
8 Tunawatia moyo mfanye mipango yenu tangu sasa kusudi mhudhurie muda wa siku tatu kwenye kusanyiko la wilaya 1999 “Neno la Unabii la Mungu.” Kama nyinyi, tunangoja kwa hamu kusikia ‘sauti ya furaha na sifa’ itakayotolewa na waabudu wa Yehova wenye umoja. (Zab. 42:4) Yehova na abariki matayarisho yote yanayofanywa kwa ajili ya kututajirisha kiroho!
[Caption on page 3]
Saa za Kukusanyika
Siku ya Tano na Siku ya Posho: 3:30 – 11:00
Siku ya Yenga: 3:30 – 10:00
[Box on page 5]
Mipango Utakayofanya ili Uhudhurie Makusanyiko “Neno la Unabii la Mungu”
1. Ikiwa utatembea mwendo mrefu ili uhudhurie kusanyiko, anza kuweka kando fedha ya kulipia safari yako na ya familia yako, na pia chakula chenu.
2. Fikiria vilevile kutegemeza matayarisho ya kusanyiko kwa zawadi zako za kujipendea. ‘Usitokee mbele ya Yehova na mikono mitupu,’ lakini ‘mheshimu Yehova kwa mali yako.’—Kum. 16:16; Mez. 3:9.
3. Sisi tutalitukuza jina la Yehova pia kwa kuwa na mwenendo mzuri na mavazi safi na yenye kutengenezwa vema, wakati wa makusanyiko.—1 Kor. 10:31.
4. Uwe na nia thabiti ya kushirikiana na akina ndugu wanaoshughulika na utaratibu. Usikamate nafasi ovyo ovyo, isipokuwa kwa ajili ya washiriki wa familia yako au wale wanaosafiri pamoja nawe.
5. Wakati wa mapumziko, ule chakula chepesi kusudi ufaidike kikamili na vipindi vyote vya alasiri. Chakula kizito huleta usingizi.—Luka 8:18.
6. Usafi humtukuza Yehova. Baada ya kila kipindi cha kusanyiko, kila mmoja atatimiza fungu lake ili tuache mahali pa kusanyiko pakiwa safi kwa kuokota karatasi na uchafu mwingine na kuutupa katika makopo ya kutupia takataka yaliyotayarishwa kwa kusudi hilo.—1 Pet. 1:15, 16.