“Walimu wa neno la Mungu”—Mkusanyiko wa Wilaya 2001 wa Mashahidi wa Yehova
1 Nabii Isaya alieleza Yehova kuwa yule Mfundishaji Mkuu, ambaye kama baba anasihi watu wake: “Njia ni hii, mwifuate.” (Isa. 30:20, 21) Lakini tunasikiaje maneno ya Yehova yanayosemwa kwa faida yetu? Yehova husema na watu wake kupitia kurasa za Biblia na pia vichapo vyenye msingi juu ya Biblia, mikutano, matukio katika mzunguko, na mikusanyiko ya wilaya inayotayarishwa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mt. 24:45) Tunaweza kuwa wenye shukrani kwa Yehova kuona anaendelea kutuongoza katika njia ambayo tunapaswa kutembea.
2 Kila mwaka, mkusanyiko wa wilaya unatutolea nafasi ya kukusanyika pamoja na waamini wenzetu na kusikiliza kwa uangalifu maagizo ya Yehova. Mwaka uliopita, maelfu ya watu walihudhuria ile Mikusanyiko ya Wilaya “Watendaji wa Neno la Mungu” yenye kuburudisha. Mnamo 2001, Mikusanyiko ya Wilaya ya siku tatu “Walimu wa Neno la Mungu” itafanywa mahali pote katika Congo-Kinshasa na Congo-Brazzaville.
3 Mikusanyiko yetu ya Wilaya ya 2001 itatutolea nafasi mpya ya kumsifu Yehova pamoja na washiriki wenzetu ambao ni “wenye kuona uhitaji wao wa kiroho” na ambao wanangoja kwa hamu ‘kusikia lile ambalo roho huyaambia makutaniko.’—Mt. 5:3; Ufu. 2:29.
4 Je, tutakuwako? Acheni tupange mambo yetu tangu sasa. Acheni tuazimie kuhudhuria zile siku tatu za karamu hiyo tamu ya kiroho, kuanzia wimbo wa kufungua mpaka sala ya kumalizia. Katika hali zilizo nyingi, mkusanyiko ambao mnaalikwa kuhudhuria ni ule ulio karibu zaidi na kwenu. Sosaiti ilifanya jitihada zote ili kufanya mambo kuwa mepesi kwa ajili yenu. Nafasi mpya imeongezwa juu ya zile za mwaka uliopita ili kuwezesha kila mmoja wetu alishwe kiroho pamoja na washiriki wa familia yake. (Kum. 31:12) Sasa ndio wakati wa kufikiria yale ambayo mtaweza kufanya ili kukusanya fedha zinazohitajiwa kwa ajili ya safari yenu nyote. Wengine walifanya jitihada za kusifiwa ili kuhudhuria mkusanyiko wa mwaka wa 2000. Dada mmoja, mume wake na watoto wao wawili walitembea kilometa 150 kwa mguu ili kufika mahali pa mkusanyiko. Dada huyo alikuwa na mimba yenye kukomaa, naye alikuwa akingoja mtoto wake wa tatu mnamo juma la mkusanyiko. Ikichochewa kwa kuona wakusanyikaji wengine wakipita, familia hiyo ikaamua kuanza safari. Alipotembea kilometa 70 kutoka nyumbani kwake, dada huyo akazaa kitoto kizuri chenye afya bora. Usiku-usiku, familia hiyo ikaendelea na safari iliyobaki, nayo ikafika mahali pa mkusanyiko mapema vya kutosha ili kuhudhuria vipindi vyote vya mkusanyiko muda wa siku hizo tatu. Tutaonyesha shukrani yetu kwa ajili ya jitihada zinazofanywa na Sosaiti kwa kufanya yote tuwezayo ili kuhudhuria mmoja wa mikusanyiko itakayofanyika mnamo 2001.
5 Upangishaji: Kwa kawaida, upangishaji unafanywa kwa watu binafsi. Tunapaswa kuonyesha shukrani kwa akina ndugu na dada wanaokubali kutupangisha. Zaidi ya hayo, halingekuwa jambo lenye kufaa kwa wale wanaoonyeshwa ukaribishaji huo kuutumia vibaya kwa kuomba wapangishwe muda mrefu kabla au baada ya mkusanyiko. Upangishaji unatolewa tu muda wa mkusanyiko. Wale wanaofaidika na aina hiyo ya upangishaji wanapaswa kuheshimu mali ya wale wanaowapangisha, kutoharibu kitu chochote, kutokwenda mahali wasipoalikwa, na kuangalia kwamba watoto wao wafanye hivyohivyo. Ikiwa wapangishaji fulani wanakabiliana na tatizo lolote upande huo, wanapaswa mara moja kujulisha idara ya upangishaji, ambayo itafurahi kuwatolea msaada. Kazi nzuri na matokeo mazuri ya idara ya upangishaji vinategemea ushirikiano wa kila mmoja. (Ebr. 13:17) Tumepata ripoti kwamba wengine huacha kwa kutaka kwao wenyewe mahali walipopangishwa ili kwenda mahali pengine kunakopatikana labda rafiki au mtu mwingine wanayejuana naye. Hilo linafanya kazi ya akina ndugu wa idara ya upangishaji kuwa ngumu. Tunaomba wote washirikiane na idara hiyo.
6 Hakuna shaka kwamba Yehova anatoa utegemezo wake kwa kile kinachofanywa kwa ajili ya mikusanyiko ya kila mwaka. Kwa kuwa ndugu wengi wanaosafiri ili kwenda kwenye mkusanyiko wa wilaya wanahitaji mahali pa kupangishwa, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atatosheleza ifaavyo mahitaji yao. Kwa kuwa mambo hayo yanahusiana na ibada ya kweli, tunapaswa kufuata kwa furaha maagizo yanayotolewa. Acheni tuonyeshe kwamba sisi ni waaminifu katika lililo dogo zaidi; hivyo tutaweza kupokea baraka tele zinazongojea wale wanaopendwa na Yehova.—Luka 16:10.
7 Kushughulikia Hali za Pekee: Watu wazee-wazee au vilema, watumishi wa wakati wote au wengine wanahitaji labda msaada ili kuhudhuria mkusanyiko. Ndugu zao wa kimwili, wazee au washiriki fulani wa kutaniko wanaojua hali yao ya pekee, wanaweza kwa upendo kufanya yale yanayohitajiwa, badala ya kutupa daraka lao juu ya ndugu wanaosimamia mkusanyiko.—Ona 1 Timotheo 5:4.
8 Kupanga Mambo ili Kuwako Muda wa Zile Siku Tatu: Je, Shetani amejaribu kukukengeusha kutoka kwenye mambo ya kiroho? Kwa kusikitisha, ndugu na dada wengi na familia zao hujinyima chakula cha kiroho chenye thamani. Namna gani hivyo? Kwa kutohudhuria vipindi vya mkusanyiko vya Siku ya Tano. Muda wa mikusanyiko fulani, ilionekana kwamba hesabu kubwa ya akina ndugu na dada walikosa elimu ya kiroho na ushirika wa kindugu ambao wangefaidika nao muda wa vipindi vya mkusanyiko vya Siku ya Tano. Inaelekea kwamba wengine wamevunjika moyo wasihudhurie mikusanyiko kwa sababu waibaji walivunja nyumba yao na kuiba wakati walipokuwa hawako. Ili kuzuia hali hizo za kuvunjiwa nyumba na kuibiwa, wengine wamechukua mipango ili washiriki wa familia wasio waamini wachunge nyumba wakati wao wanapohudhuria mkusanyiko pamoja na washiriki wa familia zao.
9 Ni Faida Gani Tunazopata Kutokana na Mikusanyiko Yetu? Ndugu mmoja aliyeguswa moyo na drama “Vielelezo vya Kuonya Leo” alisema: “Kichwa hicho ni chenye kufaa wakati tunaoishi, ambao unafanana na ule wa Waisraeli katika jangwa wakati walipokuwa karibu na kuingia katika nchi ya ahadi. Dhambi walizofanya Waisraeli ni sawa na zile ambazo watu wanafanya leo, zaidi sana ibada ya sanamu (ibada inayotolewa kwa watu wenye kujulikana sana) na uasherati. Hiyo ndiyo sababu inayofanya drama hii iwe onyo.” Je, wewe pia uliguswa moyo na mafundisho yaliyotokana na drama hiyo?
10 Maneno ya Kumalizia: Kadiri wakati unavyokaribia kwa ajili yenu kuhudhuria mkusanyiko wenu wa wilaya, fanyeni jambo hilo kuwa shabaha ya sala kwa Yehova kusudi mhudhurie vipindi vyote vya mkusanyiko muda wa siku zote tatu na kupata faida kubwa zaidi kutokana na programu. Je, mmekwisha kuomba mapumziko kutoka kazini kwa ajili ya zile siku tatu za mkusanyiko mnaopanga kuhudhuria? Ikiwa hamjaomba mapumziko hayo, fanyeni hivyo mapema zaidi iwezekanavyo. Kwa kawaida, maombi ya mapumziko kutoka kazini yanayofanywa kwenye dakika za mwisho hayakubaliwi. Mtumwa mwaminifu na mwenye busara amepanga Mkusanyiko wa Wilaya wa mwaka huu “Walimu wa Neno la Mungu” ili kututolea maagizo ya kiroho na kujenga imani yetu. Kwa hiyo, anzeni kuchukua mipango yenu sasa ili kuhudhuria, mkifuata shauri la mtunga-zaburi: “Barikini Mungu katika makusanyiko”!—Zab. 68:26.
[Box on page 3]
Saa za Programu
Siku ya Tano na Siku ya Posho
3:30 – 11:00
Siku ya Yenga
3:30 – 10:00
[Box on page 4]
Mipango Fulani ya Kuchukua kwa Ajili ya Kuhudhuria Mikusanyiko “Walimu wa Neno la Mungu”
1. Ikiwa unapaswa kutembea mwendo mrefu ili kuhudhuria mkusanyiko, anza kuweka kando fedha ili kulipia safari yako na ya familia yako, na pia chakula chenu.
2. Fikiria pia kutegemeza matayarisho ya mkusanyiko kupitia zawadi zako za kujitakia. ‘Usitokee mbele ya Yehova na mikono mitupu,’ lakini ‘mheshimu Yehova kwa vitu vyako vya thamani.’—Kum. 16:16; Mez. 3:9.
3. Tunatukuza pia jina la Yehova kwa kuwa na mwenendo mzuri na mavazi safi na yenye kufaa wakati wa mikusanyiko.—1 Kor. 10:31.
4. Azimieni kushirikiana na akina ndugu wanaoshughulika na utaratibu. Usichunge nafasi bure, ila tu kwa ajili ya washiriki wa familia yako au wale unaosafiri nao.
5. Wakati wa mapumziko, angalia kwamba ule chakula chepesi kusudi uweze kufaidika kikamili na vipindi vya kisha mchana-kati. Chakula kizito huleta usingizi.—Luka 8:18.
6. Usafi humheshimisha Yehova. Baada ya kila kipindi cha mkusanyiko, kila mmoja atataka kutimiza fungu lake ili kuacha mahali pa mkusanyiko pakiwa safi kwa kuokota karatasi na mambo mengine yenye kufanana na hayo kusudi hayo yatupwe katika mapipa ya kutupia takataka, mapipa yaliyotayarishwa kwa kusudi hilo.—1 Pet. 1:15, 16.