“Tembea na Mungu” Mkusanyiko wa Wilaya wa Mashahidi wa Yehova wa 2004
1 Ni nini kinachofanya mikusanyiko yetu ya wilaya ya kila mwaka iwe ya pekee kwako? Je, ni hotuba zenye kujenga na drama ambazo “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” hutayarisha kwa ajili yetu? (Mt. 24:45-47) Je, ni vichapo vipya vilivyo na chakula cha kiroho kinachofika pa wakati unaofaa? Je, ni ndugu na dada wanaosimulia mambo yao yaliyoonwa kuhusu jinsi Biblia ilivyobadili maisha yao na kuyafanya yawe bora? Je, ni ripoti kuhusu jinsi kazi ya kuhubiri Ufalme inavyoendelea katika nchi nyinginezo? Je, ni ushirika pamoja na waamini wenzetu wa umri zote? Ndiyo, tunatazamia kwa hamu mikusanyiko yetu kwa sababu hizo na nyingine nyingi!
2 Hudhuria Siku Zote Tatu: Kupitia Musa, Yehova aliamuru: “Wakutanishe watu . . . ili wasikilize na ili wajifunze.” (Kum. 31:12) Kupitia jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara, Yehova ametayarisha programu ya pekee ya elimu kwa ajili yetu kila siku ya mkusanyiko wetu. Kwa kuwa anatufundisha ili ‘tujifaidi wenyewe,’ tunataka kuwako ili kufuata mafundisho yake yote. (Isa. 48:17) Ikiwa unahitaji kuomba tajiri wako akuruhusu usiende kazini, sali kwa Yehova na ufanye ombi lako, ukifuata mfano wenye ujasiri wa Nehemia. (Neh. 1:11; 2:4) Pia, lingekuwa jambo lenye upendo kujulisha washiriki wa familia yako wasio Mashahidi kuhusu mipango yako ya kuhudhuria mkusanyiko; wajulishe mapema zaidi iwezekanavyo.
3 Upangishaji: Mipango kwa ajili ya upangishaji kwenye mji wa mkusanyiko inafanywa kwa kawaida katika nyumba za akina ndugu binafsi, katika Majumba ya Ufalme, au katika nyumba za washiriki wa familia. Orodha ya mahali pote pa mkusanyiko itawekwa kwenye ubao wa matangazo katika kutaniko baada ya nyongeza hii kuchunguzwa kwenye Mkutano wa Utumishi. Inapendekezwa kwamba kila mtu afikirie katika sala mkusanyiko atakaohudhuria mnamo 2004. Ikiwa ungependa kupangishwa katika nyumba ya ndugu binafsi, au katika Jumba la Ufalme, tunapendekeza mwandishi afanye mapema vya kutosha orodha ya wahubiri wote wanaoomba kupangishwa na kuituma kwa Idara ya Upangishaji katika mji wa mkusanyiko. Anapaswa kuonyesha jina la yule anayeomba kupangishwa, kusema ikiwa ni mume au mke, kutoa umri wake na uhusiano wake wa kifamilia. Hilo litafanya akina ndugu wanaosimamia Idara ya Upangishaji wawe na wakati wa kutosha ili kupata mahali pa kupangisha wote. Baada ya kupewa mahali pa kupanga, halitakuwa jambo lenye kufaa wakati huo kufanya mipango ya kibinafsi ili kukaa na ndugu au rafiki mwingine. Hilo lingefanya kazi ya wale wanaosimamia Idara ya Upangishaji iwe ngumu zaidi. Hata hivyo, ikiwa muda wa mkusanyiko mtu fulani anakusudia kukaa na mshiriki wa familia ambaye si ndugu wa kiroho, mtu huyo hapaswi tena kujaza na kutuma fomu ya kuomba kupangishwa.
4 Kupangisha Watu Katika Jumba la Ufalme: Tunatoa hapa maagizo fulani kuhusu jinsi ya kupangisha watu katika Jumba la Ufalme. Halmashauri ya Mkusanyiko wa Wilaya itatoa mgawo kwa mzee mmoja ili asimamie mpango huo. Atakuwa na msaidizi, kwa kawaida mzee mwingine au mtumishi wa huduma mwenye sifa za kiroho. Jumba linapaswa kugawanywa katika sehemu mbili. Sehemu moja kwa ajili ya akina dada na watoto wao, na wasichana pia. Sehemu nyingine kwa ajili ya akina ndugu na pia washiriki wengine wa kiume. Jumba la Ufalme litatumiwa tu kuwa mahali pa kulala. Wote wanapokuwa hawako mahali pa mkusanyiko mchana, kazi ya kufanya ulinzi itapangwa kwa kupeana zamu ili kuzuia wizi wa mali za watu binafsi. Ndugu wenye tabia nzuri na wenye sifa za kiroho wanapaswa kutumiwa ili kufanya ulinzi huo. Haitaruhusiwa kupikia chakula katika Jumba la Ufalme. Kibanda cha muda kinaweza kujengwa katika kiwanja ili kitumiwe kuwa mahali pa kupikia chakula wakati wa mkusanyiko tu. Mwishoni mwa mkusanyiko, kibanda hicho kitabomolewa. Ni jambo la maana kwamba jumba na viwanja vilindwe vikiwa safi na vyenye utaratibu. Inafaa kuwa waangalifu ili jambo lolote lisiharibiwe. Wale wanaokaa katika jumba watafanya yote wawezayo ili kuonyesha mwenendo unaostahili Wakristo wa kweli, wenyewe kwa wenyewe na kuelekea majirani.—1 Kor. 10:31.
5 Mtume Paulo alikumbusha makutaniko katika Galatia ‘watendee wote mema, na hasa wale ambao katika imani ni jamaa zao.’ (Gal. 6:10) Huenda ndugu na dada wazeewazee, walemavu, wazazi wanaolea watoto peke yao, mafukara au wale walio katika utumishi wa wakati wote wasiombe msaada, lakini huenda wakawa na matatizo wanayopaswa kushinda ili kuhudhuria mkusanyiko. Je, unaweza ‘kutenda mema’ kuwaelekea na kuwatolea msaada fulani? Washiriki wa familia walio Wakristo na wazee hasa wanapaswa kutambua hali za watu hao.
6 Uandalizi huo ni kwa ajili ya wahubiri wenye msimamo mzuri tu, na pia watoto wao wanaojiendesha vizuri. Ikiwa ndugu wa Idara ya Upangishaji wana maulizo yoyote kuhusu ombi fulani, watawasiliana na mwandishi wa kutaniko.
7 Kwenye mkusanyiko mmoja wa watu wa Yehova uliofanyika karibu miaka 2,500 iliyopita, Ezra na Walawi wenzake walisoma Neno la Mungu na kulifafanulia watu waliokusanyika pamoja. Matokeo? Andiko la Nehemia 8:12 linatueleza kwamba “watu wote wakaenda zao . . . kushangilia sana, kwa maana walikuwa wameelewa maneno ambayo walijulishwa.” Je, sisi si wenye shukrani kuona kwamba jamii ya mtumwa iliyotiwa mafuta, kama Ezra na Walawi, inatumia Neno la Mungu, inalifafanua, na kutuonyesha jinsi ya kulitumikisha katika maisha zetu? Kwa kufanya hivyo, mtumwa huyo anaonyesha upendo wa Yehova na hangaiko lake la kweli kuelekea watu Wake wote. Fanya liwe azimio lako kutokosa hata siku moja ya Mkusanyiko wa Wilaya “Tembea na Mungu”!
8 Utumishi wa Kujitolea: Watumishi waaminifu wa Yehova huonyesha sikuzote roho ya kujinyima kwa kujitoa kwa utayari kuwa wafanyakazi wa kujitolea. Kwa mfano, nafasi ilipotolewa ili kutumika kuwa mjumbe wa Mungu, nabii Isaya aliitikia bila kukawia akisema: “Mimi hapa! Nitume mimi.” (Isa. 6:8) Kutayarisha na kupanga mkusanyiko kunaomba wakati mwingi na jitihada nyingi. Bila shaka, makutaniko ya mji unaopokea mkusanyiko yatataka kuitikia ifaavyo ombi la kutoa wafanyakazi wa kujitolea. Wazee na watumishi wa huduma hasa watataka kutoa mfano bora katika njia hiyo. Upendo wetu kwa Yehova Mungu, kwa ibada safi, na kwa ndugu zetu unapaswa kutuchochea kujitoa. Kuna methali inayosema: “Kidole kimoja hakivunji chawa.”
9 Itikia kwa Utayari Kuwa Mfanyakazi wa Kujitolea: Wakati wa mkusanyiko, mamia ya wafanyakazi wa kujitolea husaidia kuendesha vizuri zile idara mbalimbali. Wakaribishaji wanaotumikia mahali wanapokaa wasikilizaji na mahali pa kuegeshea magari hutoa mwelekezo kuhusu viti, nao huchunga magari yetu mchana. Idara ya Usafishaji ina pendeleo la kulinda sifa tuliyo nayo ya kuwa watu safi, ikiacha mahali petu pa muda pa ibada pakiwa safi zaidi kuliko tulivyopakuta. Je, tunaweza kusaidia idara hizo au nyinginezo zinazoweza kutumia utegemezo wetu? Je, utatoa msaada wako ili kutumika “bega kwa bega” pamoja na ndugu zako?—Sef. 3:9.
10 Kwa kuwa “tamasha ya ulimwengu huu inabadilika,” tunahitaji mikusanyiko yetu ya wilaya ili itusaidie tubaki waangalifu kiroho. (1 Kor. 7:31) Kuchukua mpango ili kuhudhuria kila siku kutaomba jitihada, lakini jitihada hiyo ni yenye kufaa. Mkusanyiko wa Wilaya wa mwaka huu, wenye kichwa “Tembea na Mungu,” umetayarishwa ili kutusaidia tubaki imara tunapongojea kutekelezwa kwa hukumu ya Yehova juu ya ulimwengu wa Shetani. Tusiache kitu chochote kituzuie kupokea mafundisho ambayo Yehova ametayarisha kwa ajili yetu.—Isa. 51:4, 5.
[Kisanduku kwenye ukurasa wa 3]
Saa za Programu
Siku ya Tano na Siku ya Posho
3:30 - 11:10 hivi
Siku ya Yenga
3:30 - 10:05 hivi
[Kisanduku kwenye ukurasa wa 4]
Mipango Fulani ya Kuchukua kwa Ajili ya Kuhudhuria Mkusanyiko wa Wilaya Wenye Kichwa “Tembea na Mungu”
1. Ikiwa unapaswa kusafiri mwendo mrefu ili kuhudhuria mkusanyiko, anza kuweka akibani fedha ili kulipia safari yako na ya familia yako, na pia chakula chenu.
2. Fikiria pia kutegemeza matayarisho ya mkusanyiko kupitia zawadi zako za kujipendea. “Mtu yeyote asionekane mbele za Yehova mikono mitupu,” lakini “Mheshimu Yehova kwa vitu vyako vyenye thamani.”—Kumb. 16:16; Met. 3:9.
3. Wakati wa mkusanyiko, tunatukuza jina la Yehova kupitia mwenendo wetu mzuri na mavazi safi na yenye heshima—1 Kor. 10:31.
4. Azimieni kushirikiana na wakaribishaji na ndugu wengine walio na daraka la kulinda utaratibu. Usichunge viti bure, ila tu kwa ajili ya washiriki wa karibu wa familia yako au wale unaosafiri nao.
5. Ili kufaidika kikamili na kipindi cha kisha mchana-kati, angalia kwamba ule tu chakula chepesi mwishoni mwa vipindi vya asubuhi. Chakula kizito kinaweza kuleta usingizi.—Luka 8:18.
6. Usafi humheshimisha Yehova. Mwishoni mwa kila kipindi cha kusanyiko, kila mmoja anaweza kutimiza fungu lake ili kuacha mahali pa mkusanyiko pakiwa safi kwa kuokota karatasi na takataka nyingine na kuzitupa katika mapipa ya kutupia takataka yaliyotayarishwa kwa kusudi hilo.—1 Pet. 1:15, 16.