Onyesha Kupendezwa Kibinafsi na Wengine—Kwa Kutumia Maulizo na Kusikiliza
1 Watu wengi wanafurahia kutoa mawazo yao lakini hawapendi ionekane kwamba wanafundishwa au kwamba wanaulizwaulizwa. Kwa hiyo, tukiwa wahudumu Wakristo, tunahitaji kujifunza ufundi wa kutumia maulizo ili kusaidia watu watoe mawazo yao.—Met. 20:5.
2 Maulizo yetu yanapaswa kuchochea watu wafikiri, wala si kuwadhuru. Alipokuwa akihubiri nyumba kwa nyumba, ndugu mmoja aliuliza, “Je, unafikiri kwamba kutakuwapo wakati ambapo watu watatendeana kwa heshima na staha mmoja na mwenzake?” Kutokana na jibu, aliendelea kusema, “Unafikiri ni jambo gani lenye kuhitajiwa ili kutimiza hilo?” au “Kwa nini unafikiri hivyo?” Alipokuwa akitoa ushahidi wa vivi hivi mahali pa watu wote, ndugu mwengine aliuliza wale walio na watoto, “Katika kuwa mzazi, ni jambo gani linalokufurahisha sana?” Kisha aliuliza, “Hangaiko lako kubwa ni gani?” Ona kwamba maulizo haya yanaruhusu watu waeleze mawazo yao bila kuwatatanisha. Kwa kuwa hali ni zenye kubadilika, huenda kubadili habari na namna yetu ya kuuliza maulizo kuwafae wale walio katika eneo letu.
3 Kufanya Watu Watoe Mawazo Yao: Ikiwa watu wanapenda kukuelezea mawazo yao, wasikilize kwa uvumilivu bila kuwakatiza isivyofaa. (Yak. 1:19) Kubali maelezo yao kwa fadhili. (Kol. 4:6) Unaweza tu kusema: “Ni jambo lenye kupendeza. Asante kwa maelezo hayo.” Wapongeze kwa unyoofu ikiwa unaweza kufanya hivyo. Kwa fadhili uliza maulizo ya ziada ili kujua mambo wanayofikiri na kwa nini wanafikiri hivyo. Tafuta yale mambo mnayokubaliana. Unapotaka kuelekeza uangalifu wao kwenye andiko, unaweza kusema, “Je, umewahi kufikiria jambo hilo kama inavyoonyeshwa hapa?” Epuka kuwa mbishi na mwenye kushikilia maoni yako.—2 Tim. 2:24, 25.
4 Namna wengine wanavyoitikia maulizo yetu, inaweza kutegemea sana jinsi tunavyowasikiliza. Watu wanaweza kutambua ikiwa tunawasikiliza kwa unyoofu. Mwangalizi mmoja msafiri alieleza, “Unapoonyesha nia ya kusikiliza watu kwa uvumilivu, ni jambo lenye kuvutia sana na ni njia nzuri ajabu ya kuonyesha shauku na kupendezwa kibinafsi na wengine.” Kusikiliza wengine kunawaletea heshima, na kunaweza kuwachochea kusikiliza habari njema ambazo tunataka kuwatolea.—Rom. 12:10.