Vutia Uangalifu wa Watu Kwenye “Nuru ya Ulimwengu”
1 Yehova alitabiri kupitia nabii Isaya: “Watu waliokuwa wakitembea katika giza wameona nuru kuu. Kwa habari ya wale wanaokaa katika nchi yenye kivuli kizito, nuru imewaangazia.” (Isa. 9:2) Hiyo “nuru kuu” ilionekana katika mambo ambayo Mwana wa Mungu, Yesu Kristo alitimiza. Kazi aliyofanya alipokuwa duniani na faida zilizotokana na dhabihu yake viliinua hali ya kiroho ya wale waliokuwa katika giza. Katika nyakati hizi zenye giza watu wanahitaji nuru kama hiyo. Mlo wa Jioni wa Bwana unatoa nafasi ya pekee ili tuvutie uangalifu wa watu kwenye “nuru ya ulimwengu.” (Yoh. 8:12) Mwaka uliopita, mamilioni ya watu walionyesha imani kwa kujiunga nasi katika kutii amri ya Yesu: “Endeleeni kufanya hivi kwa kunikumbuka mimi.” (Luka 22:19) Kwa kuwa mwadhimisho wa Ukumbusho wa mwaka huu unakaribia, tunawezaje kushiriki katika kuvutia uangalifu wa watu kwenye nuru kuu ambayo Yehova amefanya iangaze?—Flp. 2:15.
2 Uthamini wa Moyoni: Majira ya Ukumbusho ndio wakati unaofaa wa kutafakari juu ya upendo mkubwa ambao Yehova na Yesu walionyesha kwa kutoa dhabihu ya fidia kwa ajili ya wanadamu. (Yoh. 3:16; 2 Kor. 5:14, 15) Bila shaka, kufanya hivyo kutaongeza uthamini wetu wa moyoni kwa ajili ya tukio hilo takatifu. Watu wa Mungu wote watapenda kupanga wakati ili kusoma na kutafakari juu ya usomaji wa pekee wa Biblia wakati wa Ukumbusho, kama inavyoonyeshwa katika Kuyachunguza Maandiko Kila Siku. Tunapofikiri kuhusu sifa za Yehova zisizo na kifani, ambazo zinaonyeshwa kwa utukufu katika mpango wa fidia, hilo linatufanya tujivunie Mungu wetu. Tunapofikiri kuhusu maana ya fidia kwa ajili ya kila mmoja wetu, hilo linaongeza upendo wetu wa moyoni kwa Mungu na kwa Mwana wake na linatuchochea kujitahidi katika kufanya mapenzi ya Mungu.—Gal. 2:20.
3 Ikiwa tunaongeza shukrani tunayo kuhusu mpango wa Yehova wa wokovu, shauku yetu kuhusu Ukumbusho itaonwa na wanafunzi wa Biblia, watu tunaowatembelea katika ziara za kurudia, washiriki wa jamaa, majirani, wanafunzi wenzetu, wafanyakazi wenzetu, na wengine tunaoalika kwenye sherehe hiyo ya pekee. (Luka 6:45) Kwa hiyo, fanya jitihada ya pekee ili kualika watu hao wote, ukiwatolea kikaratasi cha mwaliko kilichochapishwa ili kiwasaidie wakumbuke tukio hilo. Ili wasisahau mtu, ndugu wengi wameona kuwa ni jambo lenye kufaa kulinda orodha yenye majina ya wale ambao wao wanaalika kwa kawaida kwenye Ukumbusho, wakiongeza majina mapya kila mwaka kwenye orodha hiyo. Tunapofanya hivyo kwa utaratibu na tunapoendelea kwa bidii kualika watu wenye kupendezwa, hilo litakuwa njia nzuri ya kuonyesha shukrani yetu kwa Yehova Mungu “kwa ajili ya zawadi yake ya bure isiyoelezeka.”—2 Kor. 9:15.
4 Pitisha Wakati Mwingi Katika Huduma: Je, unaweza kupitisha wakati mwingi katika huduma mnamo Machi na Aprili? Tunapojitahidi kuhubiria wengine “habari njema yenye utukufu juu ya Kristo,” hakika tutabarikiwa na Mungu. Yehova, aliye chanzo cha nuru yote ya kiroho, ameamuru: “nuru na iangaze kutoka katika giza.” (2 Kor. 4:4-6) Kama inavyohitajiwa, wazee watapangia saa nyingine za mikutano kwa ajili ya utumishi wa shambani na mahali tofauti, wakichukua uongozi ili kutegemeza wahubiri wanaotaka kupitisha wakati mwingi katika huduma. Hilo linaweza kutia ndani kazi ya kuhubiri barabarani mapema asubuhi au mipango ya kuhubiri katika eneo la biashara na kutoa ushahidi kwa njia ya simu kisha mchana-kati au jioni. Kama msaada ili kuongeza ushiriki wako katika huduma, jiwekee mradi wa saa unaoweza kutimiza, na jitahidi kuufikia. Kwa wengi, kumtolea Yehova lililo bora zaidi kunatia ndani pendeleo la kuwa painia msaidizi.—Kol. 3:23, 24.
5 Je, Unaweza Kuwa Painia Msaidizi? Kumepita sasa miaka zaidi ya saba kuanzia wakati ambapo kiwango cha saa kuhusu upainia msaidizi kilipunguzwa. Rekebisho hilo limefanya iwezekane kwa wengi zaidi kuonja furaha na faida za utumishi wa upainia msaidizi. Je, umejaribu hilo? Wengine wanafanya kuwa jambo la kawaida kufanya hivyo kila mwaka. Katika makutaniko mengi wahubiri wengi wanafanya utumishi huo pamoja, na hilo linakuwa jambo la maana zaidi na lenye kutosheleza katika utendaji wa kutaniko wa mwaka. Je, unaweza kufanya programu ili utumikie ukiwa painia msaidizi katika mwezi wenye kufurahisha wakati wa majira ya Ukumbusho? Aprili inaweza kuwa mwezi unaofaa vizuri kwa wengine, kwa kuwa ina miisho-juma mitano.
6 Je, kutaniko lenu lina ziara ya mwangalizi wa mzunguko mnamo Machi au Aprili? Nafasi ya pekee inajitokeza kwenu. Kama ilivyotangazwa, katika mwaka wa utumishi wa 2006, wale wote wenye kutumikia wakiwa mapainia wasaidizi katika mwezi ambamo mwangalizi wa mzunguko anatembelea kutaniko, wataalikwa kuhudhuria kipindi cha kwanza cha mkutano pamoja na mapainia mnamo juma la ziara. Bila shaka habari yenye kutia nguvu kiroho inayotolewa kwenye mkutano huo itasaidia mapainia wasaidizi wengi kujitahidi kufikia pendeleo la upainia wa kawaida. Zaidi ya hilo, mnamo Machi tutakuwa na furaha ya kusaidia watu waingie katika nuru ya kiroho kwa njia ya kichapo kipya cha funzo Biblia Inafundisha Nini Hasa? Kwa nini usijiwekee mradi wa kuanza funzo la Biblia katika kitabu kipya?
7 Unapofikiria kiwango cha saa 50 cha painia msaidizi, fanya programu itakayokuruhusu kuangaza nuru ya kweli kwa karibu saa 12 kila juma. Zungumza kuhusu jambo hilo na wale ambao wamefanikiwa kufanya hivyo, na wengine pia. Hilo linaweza kuwatia moyo wajiunge nawe. Kwa kupanga mambo vizuri, wahubiri waliobatizwa, vijana na wale wenye umri mkubwa, wameona kwamba haikuwa vigumu sana kufikia mradi huo wenye kustahili pongezi. Sali kuhusu jambo hilo. Kisha, ikiwezekana, panga mambo yako, na furahia kufanya upainia msaidizi!—Mal. 3:10.
8 Familia nyingi zimeona kwamba jitihada zinazofanywa pamoja kwa ushirikiano zinaweza kuwezesha angalau mshiriki mmoja wa familia kufikia mradi huo. Familia moja iliamua kwamba washiriki wote watano waliobatizwa watumikie kama mapainia wasaidizi. Watoto wengine wawili ambao bado hawakuwa wenye kubatizwa walifanya jitihada ya pekee ili kuongeza utendaji wao. Familia hiyo ilifaidikaje na kufanya jitihada zaidi? Waliandika: “Mwezi huo ulikuwa wenye kupendeza sana, na tulijisikia kabisa kwamba uhusiano wa familia ulitiwa nguvu. Tunamshukuru Yehova kwa baraka hiyo nzuri ajabu!”
9 Je, utendaji wetu wa pekee mnamo Machi na Aprili utaonekana kuwa wenye kuchochea, ukifanya tumkaribie Baba yetu aliye mbinguni? Kufanikiwa kwetu kutategemea jitihada ya kibinafsi tutakayofanya ili kuongeza upendo wetu kwa Mungu na kwa Mwana wake na kuongeza kushiriki kwetu katika huduma. Azimio letu na liwe kama la mtunga-zaburi, aliyeimba: “Nitamsifu sana Yehova kwa kinywa changu, na katikati ya watu wengi nitamsifu.” (Zab. 109:30) Yehova atabariki utendaji wetu wenye bidii mnamo majira haya ya Ukumbusho. Kwa hiyo na tuache nuru kuu iangaze ili watu wengi zaidi watoke kwenye giza na ‘wawe na nuru ya uzima.’—Yoh. 8:12.
[Maulizo ya Funzo]
1. Ni nuru gani kuu ambayo ilitabiriwa katika Neno la Mungu, na ni tukio gani linalovutia uangalifu wa pekee kwenye nuru hiyo?
2. Tunawezaje kuongeza uthamini wetu wa moyoni kuhusu dhabihu ya fidia, na kufanya hivyo kutakuwa na matokeo gani?
3. Tunawezaje kuonyesha shukrani yetu kuhusu Ukumbusho?
4. Ni nini linaloweza kutusaidia kupitisha wakati mwingi katika huduma mnamo Machi na Aprili?
5. Wengi wanafaidika namna gani na kiwango cha saa kilichopunguzwa kuhusu upainia msaidizi?
6. Ni mipango gani yenye kusisimua ambayo imechukuliwa?
7, 8. (a) Ni nini linaloweza kutusaidia kupangia programu ili kufanya upainia msaidizi? (b) Ushirikiano wa familia unawezaje kusaidia, na familia nzima inafaidikaje?
9. Tunawezaje kuacha nuru yetu iangaze mnamo majira haya ya Ukumbusho?