Wametuwekea Mfano wa Uaminifu
1 Aina mpya ya utumishi wa wakati wote ilianzishwa katika mwaka wa 1937. Utumishi huo ni upainia wa pekee. Wanaume na wanawake wenye uwezo, wenye kujua mambo mengi kuhusu kazi ya kuhubiri, walikubali kwa kujipendea maeneo ya kutumika popote ambapo tengenezo liliwatuma. Sasa, baada ya miaka mingi, mapainia wa pekee wanaendelea kuonyesha mfano wa uaminifu unaostahili kuigwa.—Ebr. 6:12.
2 Walikuwa Mbele Katika Utumishi: Hapo mwanzo, mapainia wa pekee walianzisha kazi ya kuhubiri wakitumia fonografe kwenye milango. Waliporudilia watu, walitumia pia habari za Biblia zilizotiwa katika kaseti ili kuzungumza nao. Walifanya hivyo katika miji mikubwa ambamo makutaniko yalikuwa yamekwisha kuundwa. Baadaye, mapainia wa pekee walitumwa katika maeneo ambako kulikuwa uhitaji mkubwa wa wahubiri wa Ufalme. Waliendelea kutembelea watu wote waliopendezwa na habari ya Ufalme na waliongoza mafunzo ya Biblia. Kwa kuwa walijikaza sana kwa bidii, mamia ya makutaniko mapya yalianzishwa. Kazi yao ya kuhubiri habari njema bila kuchoka ilisaidia tengenezo lipanuke kabisa kufikia hali tunayoona leo. (Isa. 60:22) Mapainia wa pekee wanaendelea kufanya kazi ya maana katika kueneza habari njema “katika uumbaji wote ulio chini ya mbingu.”—Kol. 1:23.
3 Mapainia wa Pekee Wanastahili Kuigwa: Mapainia wa pekee fulani wamefanya utumishi wa wakati wote kwa miaka mingi. Miaka yote hiyo, wanaume na wanawake hao waaminifu wamefanya imani yao ikomae kutokana na hali tofauti-tofauti. (1 Pet. 1:6, 7) Kwa kujipendea, wameacha raha ya vitu vya kimwili ili kutumikia mahali ambapo kuna uhitaji wa kipekee. Wengine wao sasa ni wazee wenye kuwa na afya zaifu, au wanashindana na magumu mengine. (2 Kor. 4:16, 17) Hata hivyo ‘wataendelea kusitawi wakati wa kuwa na kichwa chenye mvi.’ (Zab. 92:14) Wanatia tumaini lao katika Yehova na wanabarikiwa naye.—Zab. 34:8; Met. 10:22.
4 Bila shaka, mapainia wa pekee wanastahili shukrani zenye upendo. Ikiwa muna pendeleo la kuwa na mapainia wa pekee katika kutaniko lenu, tumieni nafasi hiyo ili kutumia wakati mwingi pamoja nao na kupata faida kutokana na ujuzi wao wa mambo mengi. Uwashukuru kwa ajili ya kazi yao ya uaminifu kuhusu Ufalme. Ushikamanifu wao na ukutie nguvu. Wote wanaoiga imani yao wanaweza pia kufurahia upendeleo na baraka ya Yehova kwa kuwa “wanaotenda kwa uaminifu ni furaha kwake.”—Met. 12:22.