Kisanduku Cha Maulizo
◼ Tunaweza Kufanya Nini ili Kuwasaidia Mapainia?
Katika mwaka wa utumishi wa 2009, karibu ndugu na dada 800,000 walitumika kama mapainia wa kawaida na wa pekee ulimwenguni pote. Watumishi hao wa wakati wote walijinyima mambo mengi; na walitoa wakati wao, nguvu zao, na mali yao ili kueneza habari njema ya Ufalme. (Met. 3:9) Yehova anapendezwa kabisa na bidii yao! Ni katika njia gani tunaweza kuonyesha kwamba, kama Yehova, sisi pia tunapendezwa na bidii ya mapainia wetu na kuwasaidia wapate furaha na kuendelea na kazi yao ya upainia?
Kwa kweli maneno yetu yenye kuchaguliwa vizuri yanaweza kuwatia moyo waendelee katika kazi ya upainia. (Met. 25:11) Je, tunaweza kubadili programu yetu ya kila juma ili tuhubiri pamoja nao? Tunapohubiri pamoja nao tunaweza kuwasaidia kuhusu kulipia garama zao za usafirishaji. (1 Kor. 13:5; Flp. 2:4) Pia, tunawategemeza kwa upendo kwa kuwaonyesha ukaribishaji na kuwaalika nyumbani kwetu wakati fulani fulani ili kula pamoja nao.—1 Pet. 4:8, 9.
Maandiko yanatuhakikishia kwamba Yehova atawatolea wale wanaotafuta kwanza Ufalme mambo wanayohitaji. (Zab. 37:25; Mt. 6:33) Njia moja anayotumia ili kufanya hivyo ni kupitia ndugu na dada zetu wenye upendo. (1 Yoh. 3:16-18) Kwa kweli, mapainia hawatazamie wengine wawatolee feza ili kutosheleza mahitaji yao. Na huenda wasituambie kwamba wana shida fulani. Hata hivyo, ikiwa sisi tuna utambuzi na ikiwa sisi tunajua kutazama vizuri, tunaweza kuwasaidia mapainia hao waaminifu na ‘kuwajazia upungufu wao.’—2 Kor. 8:14, 15.
Fibi, mhubiri mwenye bidii wa kutaniko la Kenkrea katika karne ya kwanza, aliposafiri kwenda Roma, Paulo aliwatia moyo ndugu wa huko Roma ‘wamkaribishe katika Bwana kwa njia inayowastahili watakatifu, na wamsaidie katika jambo lolote ambalo huenda akawahitaji wao.’ (Rom. 16:1, 2) Sisi pia tuna nafasi ya kuonyesha roho hiyo ya kuwategemeza kwa upendo ndugu na dada walio katika kutaniko letu, ambao wanatangaza habari njema bila kuacha wakiwa mapainia wa kawaida na wa pekee.—Mdo. 5:42.