Pendezwa Kibinafsi na Wengine —Kwa Kuwahubiria Bila Ubaguzi
1 Mtume Yohana aliona malaika anayeruka katikati ya mbingu akiwa mwenye kutangaza habari njema ya milele kwa watu wa ‘kila taifa na kabila na luga.’ (Ufu. 14:6) Je, sisi tunafuata mfano wa malaika huyo kwa kuhubiria watu bila ubaguzi au upendeleo? Bila kujua, tunaweza kuwa na maoni yanayoonyesha kwamba tuna upendeleo. Tukiwa na maoni yasiyofaa juu ya watu tunaokutana nao, hilo linaweza kutuzuia kuwatolea habari njema inavyofaa. Kwa hiyo, tunapaswa kuonyesha kwamba kweli tunahangaikia watu kwa upendo, tunapowahubiria wale walio na malezi au elimu tofauti na yetu.
2 Fikiria Eneo Lenu: Je, kuna wageni au wakimbizi wanaoishi katika eneo lenu? Huenda tusiwafikirie sana. Chukua hatua ya kuwatafuta na ufanye nguvu ya kuwajua vizuri. Mahitaji yao na mahangaiko yao ni nini, ni mambo gani wanayopenda na ni mambo gani wasiyopenda, wasiwasi yao ni nini na wanachukia nini? Kulingana na hali hizo, jaribu sasa kupatanisha mahubiri yako na habari ya Ufalme. (1 Kor. 9:19-23) Kama vile mtume Paulo alivyojisikia, sisi pia tunapaswa kujisikia kuwa tunalazimishwa kuhubiria kila mtu aliye katika eneo letu habari njema, bila kusahau watu kutoka inchi ya kigeni, wale walio na desturi tofauti na zetu, wale wanaosema luga nyingine, na wale walio matajiri kabisa.—Rom. 1:14, maelezo yaliyo chini katika Rbi8-F.
3 Kwa hiyo, namna gani unaweza kuhubiria mtu anayezungumza luga tofauti na yako? Tumia vizuri kijitabu Habari Njema kwa Watu wa Mataifa Yote. Pia, unaweza kuchukua trakti fulani au broshua za luga za kigeni zinazozungumzwa katika eneo lenu (Ona Huduma Yetu ya Ufalme ya Julai 2003, uku. 4, fu. 2-3.) Zaidi ya mambo hayo, wahubiri wengine walifanya nguvu ya kujifunza namna ya kusalimia watu katika luga hizo za kigeni na namna ya kuhubiri kwa maneno machache katika luga hizo. Kwa kawaida, watu wanafurahi sana kusikia mtu fulani akijaribu kuzungumza nao katika luga yao, hata ikiwa haijuwe vizuri, na jambo hilo linaweza kuwavuta wasikilize habari njema.
4 Tufuate Mfano wa Yehova: Tunapohubiria watu walio na malezi au elimu tofauti na yetu, tunamwiga Yehova, Mungu wetu asiye na ubaguzi, “ambaye mapenzi yake ni kwamba watu wa namna zote waokolewe na kupata ujuzi sahihi wa kweli.”—1 Tim. 2:3, 4.