Je, Unajitayarisha kwa Ajili ya Misiba?
1 Kila mwaka, mamilioni ya watu ulimwenguni pote, kutia ndani ndugu na dada zetu wengi, wanatatizwa kwa sababu ya matetemeko ya dunia, misiba yenye kutokezwa na mtutumuko wa bahari na kuharibu vitu, maji ya mitoni inayofurika, upepo mkali, na mvua kubwakubwa. Kwa kuwa misiba inatokea bila kutazamiwa na inaweza kupata mtu yeyote kati yetu, basi, ni jambo la hekima kujitayarisha.—Met. 21:5.
2 Mambo ya Kufanya Mbele ya Msiba Kutokea: Nyakati nyingine viongozi wanaweza kujulisha watu kuhusu misiba inayotaka kutokea. Ni jambo la maana kusikiliza maonyo hayo kwa uangalifu. (Met. 22:3) Katika hali hizo, wazee watajaribu kuonana au kupashana habari na washiriki wote wa kutaniko ili kuwasaidia wajitayarishe kama inavyofaa. Baada ya msiba, wazee watajikaza tena kuonana na watu wote wa kutaniko ili kuona ikiwa wako salama na kutambua ni msaada gani wanaohitaji. Wazee wanaweza kupoteza wakati ikiwa hawajui mahali ambapo washiriki wa kutaniko wanapatikana. Kwa hiyo, ni jambo la maana wahubiri wajulishe mwandishi wa kutaniko na mwangalizi wa funzo lao la kitabu adresi zao na namba zao za telefone.
3 Ikiwa kutaniko liko katika eneo lenye kupatwa na misiba mara nyingi, wazee wanaweza kuomba kila mhubiri awatolee jina na namba ya telefone ya mtu wa jamaa au rafiki mwenye kuishi mbali na eneo hilo, ambaye wanaweza kupashana naye habari ikiwa kuna lazima ya kutoa msaada kwa haraka. Hilo litawezesha wazee kujua mahali wanapopatikana wale waliohamishwa. Wazee wanaweza pia kupanga mambo mbele ya wakati ambayo kutaniko litafanya msiba unapotokea, mambo kama vile kuandika vitu vya lazima ambavyo mtu anapaswa kuwa navyo msiba unapotokea, mipango kuhusu kuhamisha watu, na kusaidia watu wanaohitaji msaada wa pekee. Ni jambo la maana kuunga wazee mkono katika mipango hiyo yenye upendo.—Ebr. 13:17.
4 Mambo ya Kufanya Kisha Msiba: Wewe utafanya nini msiba unapotokea katika eneo lenu? Fanya nguvu ili mahitaji ya kimwili ya familia yako yatimizwe. Saidia pia wengine ambao wamepatwa na msiba ikiwa una uwezo wa kufanya hivyo. Ujikaze kupashana habari na mwangalizi wa funzo lenu la kitabu au mzee mwingine haraka iwezekanavyo. Utafanya hivyo hata ikiwa wewe ni salama na hauna lazima ya msaada. Ikiwa una lazima ya msaada, jua hakika kwamba ndugu zako ni wenye kufanya yote wawezayo ili upate msaada huo. (1 Kor. 13:4, 7) Kumbuka kwamba Yehova anajua hali yako; umtegemee ili akusaidie. (Zab. 37:39; 62:8) Tafuta nafasi za kutolea wengine msaada wa kiroho na kuwafariji. (2 Kor. 1:3, 4) Rudilia kwa haraka programu yako ya mambo ya kiroho ya kawaida.—Mt. 6:33.
5 Ijapokuwa hatari inayotokezwa na misiba inaogopesha sana watu, sisi tunaweza kutumainia mambo mema wakati ujao. Hivi karibuni, misiba yote itakuwa mambo ya zamani. (Ufu. 21:4) Kwa wakati huu, tunaweza kufanya mambo yenye kuonyesha hekima ili kujitayarisha kwa ajili ya wakati wa taabu na matatizo, tukiendelea kuhubiria wengine habari njema kwa bidii.
[Maulizo ya Funzo]
1. Kwa nini ni jambo la hekima kujitayarisha kwa ajili ya misiba?
2. Kwa nini tunapaswa kujulisha wazee adresi zetu na namba zetu za telefone?
3. Namna gani tunaweza kuunga wazee mkono ikiwa tunaishi katika eneo lenye kupatwa na misiba mara nyingi?
4. Tutafanya nini ikiwa msiba unatokea katika eneo letu?
5. Hatari zinazotokana na msiba zinakuwa na uvutano gani kwetu sisi Wakristo?