Mabadiliko Yenye Kufurahisha Kuhusu Gazeti Mnara wa Mlinzi!
1 Mwanzoni mwa mwaka huu, makutaniko yalipokea tangazo lenye kufurahisha, tangazo hilo lilisema kwamba kuanzia mwezi wa kwanza mwaka wa 2008, gazeti Mnara wa Mlinzi litakuwa na magazeti mawili tofauti, moja kwa ajili ya watu wote na lingine kwa ajili ya ndugu na dada zetu (Mashahidi wa Yehova tu)! Labda mmekuwa mkijiuliza hivi: ‘Magazeti hayo yatakuwa tofauti kwa njia gani? Kuna faida gani za kuwa na magazeti mawili tofauti? Je, kuna mambo mapya katika magazeti hayo?’
2 Mambo Yaliyo Tofauti Katika Magazeti Hayo Mawili: Mnara wa Mlinzi wa tarehe 1 ya kila mwezi utaitwa Gazeti la Watu Wote. Habari zote katika gazeti hilo zitatayarishwa kwa faida ya watu wote. Mnara wa Mlinzi wa tarehe 15 ya kila mwezi utaitwa Gazeti la Funzo na hatutatolea watu gazeti hilo katika mahubiri. Litakuwa na habari zote za funzo kuhusu mwezi mmoja na pia habari zingine ambazo zinapendeza zaidi watumishi wa Yehova. Gazeti la Watu Wote litavutia pia Mashahidi wa Yehova, lakini litapendeza zaidi watu wasio Mashahidi ambao wanakubali Biblia. Kwa upande mwingine, gazeti Amkeni! litaendelea kuchapishwa kwa ajili ya watu wengi zaidi, kutia ndani watu wenye mashaka na wale wa makanisa yasiyo ya Kikristo.
3 Faida Mbalimbali: Katika Gazeti la Funzo, haitakuwa tena lazima kufasiria maneno kama vile “painia” ili kusaidia watu wasio Mashahidi. Gazeti hilo linaweza pia kuwa na habari zenye kufaa zilizotayarishwa kwa ajili ya Mashahidi wa Yehova tu au wanafunzi wa Biblia wenye kufanya maendeleo ya kiroho. Tuseme nini kuhusu Gazeti la Watu Wote? Kwa kuwa habari zitakazoandikwa katika gazeti hilo na namna zitakavyoandikwa ni kwa faida ya watu wote, mtu asiye Shahidi atafurahia kusoma gazeti hilo tangu mwanzo mpaka mwisho. Bila shaka, kila Shahidi wa Yehova atafaidika na usomaji wa magazeti hayo mawili. Kwa kuwa, kila mwezi, tutatolea watu katika mahubiri Mnara wa Mlinzi moja tu na Amkeni! moja, tutakuwa na mwezi mzima ili kuzungumzia kwa kirefu utoaji mbalimbali kwa matokeo mazuri.
4 Mambo Mapya: Kuna mambo mapya fulani yenye kufurahisha yanayopangwa kwa ajili ya gazeti Mnara wa Mlinzi la Watu Wote. Habari moja itazungumzia mafundisho ya msingi ya Maandiko katika njia nyepesi sana. Habari nyingine itaonyesha jinsi Biblia inavyoweza kusaidia familia. Mipango ya kujifunza Biblia itaonyeshwa kwa ajili ya vijana. Kila gazeti litakuwa na habari yenye kukazia maandiko fulani ya Biblia yanayotufundisha kuhusu sifa za Yehova.
5 Tunaomba Yehova abariki mpango huu mpya kwa ajili ya Mnara wa Mlinzi. Acheni gazeti hilo pamoja na Amkeni!, yafikishie habari njema watu wengi zaidi wenye kustahili.—Mt. 10:11.