Mradi Unaofaa kwa Ajili ya Mwaka Mpya wa Utumishi
1 Tunapaswa kujiwekea miradi ikiwa tunataka kufanya maendeleo ya kiroho. Ni miradi gani ya kipekee ambayo umejiwekea kwa ajili ya mwaka mpya wa utumishi? Mradi mzuri sana ni kufanya kazi ya upainia msaidizi kwa mwezi mmoja au zaidi. Kwa kuwa utumishi huo wenye kufurahisha unaomba kufanya mipango mbele ya wakati, sasa ni wakati mzuri wa kuanza kufanya mipango. Kwa nini tusifikirie mradi wa kufanya kazi ya upainia msaidizi?
2 Sababu za Kufanya Upainia Msaidizi: Kufanya kazi ya upainia msaidizi kunatuwezesha kumpendeza Baba yetu wa mbinguni “kwa ukamili zaidi” kwa kutumia wakati mwingi zaidi katika kazi ya kuhubiri. (1 The. 4:1) Tunapofikiria mambo yote ambayo Yehova ametutendea, mioyo yetu inatuchochea kuelezea wengine kumhusu. (Zab. 34:1, 2) Yehova anaona na anafurahia sana namna kila mtu anavyojitoa ili kufanya mengi zaidi katika kazi ya kuhubiri. (Ebr. 6:10) Kujua kwamba tunampendeza Yehova kupitia kazi yetu ngumu kunatuletea furaha kubwa.—1 Nya. 29:9.
3 Kwa kawaida, kadiri tunavyofanya mara nyingi jambo fulani, ndivyo linavyokuwa jepesi zaidi na lenye kufurahisha. Kutumia wakati mwingi katika kazi ya kuhubiri kunafanya uwe mwenye kutulia unapohubiri mlango kwa mlango. Utakuwa na ufundi zaidi wa kuanzisha mazungumzo na pia ufundi wa kutumia Biblia. Kadiri unavyozungumzia zaidi imani yako, ndivyo itakavyokuwa yenye nguvu. Wengi ambao hawakuwa wakiongoza funzo la Biblia wameanzisha funzo moja walipofanya kazi ya upainia msaidizi.
4 Kufanya kazi ya upainia msaidizi kunaweza kuwa ndicho kitia-moyo kinachohitajiwa ili kutoka katika hali ya kutofanya maendeleo ya kiroho. Ndugu mmoja aliyekuwa painia wa kawaida hapo mbele alitambua kwamba alikuwa akitumia wakati mwingi sana kwa kufanya kazi yake ya kimwili na hivyo aliamua kufanya upainia msaidizi kwa mwezi mmoja. Alisema hivi: “Nilishangaa sana jinsi mwezi huo mmoja ulivyonitia nguvu kiroho! Nilifanya mipango ya kuwa painia msaidizi bila kukatiza na hilo liliniwezesha kuwa tena painia wa kawaida.”
5 Jinsi ya Kushinda Vizuizi: Ndugu au dada wengine wanaweza kusita kujaza ombi la upainia msaidizi kwa kuwa wanajisikia kuwa wahubiri wasio na ufundi. Ikiwa jambo hilo ndilo linalokuzuia, Yehova anaweza kukusaidia kama alivyomsaidia Yeremia. (Yer. 1:6-10) Ijapokuwa Musa alikuwa na ‘kinywa kizito na ulimi mzito,’ Yehova alimtumia ili kutimiza mapenzi Yake. (Kut. 4:10-12) Ikiwa unajisikia kwamba haustahili, mlilie Yehova akupe bidii.
6 Je, unasita kujaza ombi la upainia kwa sababu ya matatizo ya afya au kwa kuwa una kazi nyingi? Ikiwa wewe ni mlemavu, kutumika kulingana na hali yako kunaweza kukuwezesha kufanya upainia msaidizi. Ikiwa una kazi nyingi, labda unaweza kupanga kufanya zile zisizo za maana sana mwezi ujao. Ndugu wengine walio na kazi inayowachukua wakati wote wameweza kununua wakati ili kufanya upainia msaidizi kwa kuchukua siku moja ao siku mbili za mapumziko.—Kol. 4:5.
7 Jinsi ya Kufanya Upainia Msaidizi: Sali kuhusu nia yako ya kutaka kufanya upainia msaidizi. Omba Yehova abariki bidii yako ya kuongeza kazi yako ya kuhubiri. (Rom. 12:11, 12) Anaweza kukusaidia ufanye maamuzi yenye hekima kuhusu namna ya kutengeneza programu yako. (Yak. 1:5) Ikiwa tamaa ya kufanya upainia haikufikie moyoni, omba basi Yehova akusaidie upate furaha katika kazi ya kuhubiri.—Luka 10:1, 17.
8 Zungumzieni mradi wa upainia msaidizi katika familia. (Met. 15:22) Labda mshiriki mmoja wa familia anaweza kuwa painia msaidizi ikiwa washiriki wengine wa familia wanamuunga mkono. Zungumza na washiriki wengine wa kutaniko kuhusu nia yako ya kufanya upainia, zaidi sana wale walio katika hali zenye kufanana na zako. Hilo linaweza kuchochea sana hamu ya kufanya kazi ya upainia msaidizi.
9 Unapochunguza programu yako ya mahubiri kwa ajili ya mwaka mpya wa utumishi, unafikiri kwamba unaweza kuwa painia msaidizi wakati gani? Ikiwa kazi yako inakuchukua wakati wote ao unaenda kwenye masomo, labda utataka kuchunguza miezi iliyo na siku ya mapumziko ao miezi iliyo na Siku za Posho tano au Siku za Yenga tano. Kwa mfano, mwezi wa 9, wa 12, wa 3, na wa 8 ina Siku za Posho tano na Siku za Yenga tano. Mwezi wa 5 una Siku za Posho tano na mwezi wa 6 una Siku za Yenga tano. Ikiwa una matatizo ya afya, chunguza miezi ambayo kwa kawaida hali ya hewa ni nzuri. Labda unaweza pia kufanya upainia katika mwezi ambao mwangalizi wa mzunguko atatembelea kutaniko lenu. Wakati wa matembezi yake, utapata pendeleo la zaidi la kuhuzuria kipindi cha kwanza cha mkutano atakaofanya pamoja na mapainia wa kawaida. Kwa kuwa Ukumbusho utafanywa tarehe 22 mwezi wa 3 mwaka ujao, mwezi wa 3, wa 4 na wa 5 ni miezi mizuri ili kufanya kazi ya upainia msaidizi. Baada ya kuchagua mwezi au miezi ambayo unataka kufanya kazi ya upainia msaidizi, anza kuandika programu itakayokuwezesha kutimiza saa zinazoombwa.
10 Hata ikiwa unaona kwamba hautaweza kufanya kazi ya upainia msaidizi mnamo mwaka wa utumishi ujao, unaweza kuendelea kuwa na roho ya upainia. Endelea kufanya yote uwezayo katika kazi ya kuhubiri, ukiwa hakika kwamba Yehova anafurahia jinsi unavyojikaza kwa nafsi yote kumtolea yote uliyo nayo kulingana na uwezo wako. (Gal. 6:4) Uwe mwenye kutegemeza na kutia moyo wale walio na uwezo wa kufanya kazi ya upainia msaidizi. Labda unaweza kutengeneza programu yako ili kuhubiri nao siku fulani ingine katika juma.
11 Watu wa Yehova wanatambua ulazima wa kutenda kwa haraka. Kuna kazi inayopaswa kufanywa—kazi ya kuhubiri habari njema. Maisha ya watu yanapatikana katika hatari, na wakati unaobaki ni mchache sana. (1 Kor. 7:29-31) Upendo kwa Yehova na kwa jirani utatuchochea tufanye yote tuwezayo katika kazi ya kuhubiri. Tukijikaza na kufanya programu nzuri, tunaweza kufanya kazi ya upainia msaidizi hata mwezi mmoja katika mwaka mpya wa utumishi unaokuja—huo ni mradi unaofaa kwelikweli!
[Maulizo ya Funzo]
1. Ni mradi gani tunaoweza kufikiria kwa ajili ya mwaka mpya wa utumishi?
2. Kwa nini kufikiria mradi wa kufanya kazi ya upainia msaidizi?
3, 4. Ni faida gani tunazopata kwa kufanya kazi ya upainia msaidizi?
5. Namna gani tunaweza kushinda mawazo ya kujisikia kuwa hatustahili?
6. Namna gani inawezekana kufanya upainia msaidizi hata ikiwa mtu ana matatizo ya afya ao kazi nyingi sana?
7. Kwa nini ni jambo lenye faida kusali sana kuhusu upainia msaidizi?
8. Namna gani kutumia Andiko la Methali 15:22 kunaweza kukuwezesha ufanye kazi ya upainia msaidizi?
9. Ni miezi gani ambayo unaweza kuchagua kufanya upainia msaidizi?
10. Unaweza kufanya nini ikiwa haiwezekani kufanya kazi ya upainia msaidizi?
11. Kwa nini tunapaswa kutambua ulazima wa kutenda kwa haraka?