Ni Nani Mufalme wa Ufalme wa Mungu?
Mungu aliongoza waandikaji wengi wa Biblia kuandika mambo mbalimbali yenye ingesaidia kutambua Ule mwenye angekuwa Mufalme wa Ufalme wa Mungu. Ule Mutawala
Angechaguliwa na Mungu. “Mimi mwenyewe nimemuweka mufalme wangu . . . Nitakupatia mataifa kuwa uriti wako na miisho ya dunia kuwa mali yako.”—Zaburi 2:6, 8.
Angekuwa muriti wa Mufalme Daudi. “Mutoto amezaliwa kwetu, tumepewa mwana . . . Kuongezeka kwa utawala wake na amani, havitakuwa na mwisho, kwenye kiti cha ufalme cha Daudi na juu ya ufalme wake ili kuufanya kuwa imara kabisa.”—Isaya 9:6, 7.
Angezaliwa Betlehemu. “Ee Betlehemu . . . , mwenye atatawala . . . kwa ajili yangu atatokea kwako . . . Ukubwa wake utafika mupaka kwenye miisho ya dunia.”—Mika 5:2, 4.
Angekataliwa na wanadamu na kuuawa. “Alizarauliwa, na hatukumuona kuwa mutu wa maana. . . . Alitobolewa kwa silaha kwa ajili ya ukosaji wetu; alikuwa anapondwa kwa ajili ya makosa yetu.”—Isaya 53:3, 5.
Angefufuliwa kutoka kwa wafu na kutukuzwa. “Hautaniacha katika Kaburi. Hautaruhusu mushikamanifu wako aone shimo. . . . Furaha iko kwenye mukono wako wa kuume milele.”—Zaburi 16:10, 11.
Yesu Kristo Njo Mwenye Anastahili Kabisa Kutawala Wanadamu
Katika historia yote ya wanadamu, ni mutu mumoja tu njo mwenye ametimiza sifa zenye kustahili ili kuwa Mutawala muzuri; ule mutu ni Yesu Kristo. Malaika mumoja aliambia Maria, mama ya Yesu hivi: “Mungu atamupatia kiti cha ufalme cha Daudi baba yake, . . . na Ufalme wake hautakuwa na mwisho.”—Luka 1:31-33.
Yesu hajakuwaka mufalme ku dunia. Lakini atatawala wanadamu akiwa mbinguni kama Mufalme wa Ufalme wa Mungu. Ni nini yenye inamufanya akuwe Mutawala muzuri? Fikiria mambo yenye Yesu alifanya wakati alikuwa ku dunia.
Yesu alihangaikia watu. Yesu alisaidia wanaume na wanamuke, vijana na wazee, bila kuangalia hali yao ya maisha ao cheo chao. (Matayo 9:36; Marko 10:16) Wakati mutu mumoja mwenye alikuwa na ukoma alimulilia: “Kama tu unataka, unaweza kunifanya nikuwe safi,” Yesu alimusikilia huruma na akamuponyesha.—Marko 1:40-42.
Yesu alitufundisha namna ya kumufurahisha Mungu. Alisema hivi: “Hamuwezi kuwa watumwa wa Mungu na wa Utajiri.” Pia alisema kama tunapaswa kutendea wengine namna tungependa watutendee; ile kanuni imefikia kujulikana kuwa Kanuni ya Muzuri Sana. Tena, alisema kama Mungu hapendezwe tu na mambo yenye tunafanya, lakini anapendezwa pia na mawazo na hisia zetu. Kwa hiyo, ili kumupendeza Mungu, tunapaswa kuzuia hisia zetu za ndani. (Matayo 5:28; 6:24; 7:12) Yesu alikazia kama ili tukuwe wenye furaha kabisa, tunapaswa kujifunza na kufanya mambo yenye Mungu anapenda.—Luka 11:28.
Yesu alifundisha maana ya kupenda wengine. Maneno na matendo ya Yesu ilikuwa yenye nguvu na iligusa mioyo ya wasikilizaji wake. “Watu wengi wakashangazwa na namna yake ya kufundisha, kwa maana alikuwa anawafundisha kama mutu mwenye mamlaka.” (Matayo 7:28, 29) Aliwafundisha hivi: ‘Mupende maadui wenu.’ Hata alisali kwa ajili ya watu fulani wenye walifanya akufe; alisali hivi: “Baba, uwasamehe, kwa maana hawajue jambo lenye wanafanya.”—Matayo 5:44; Luka 23:34.
Yesu anastahili kabisa kuwa Mutawala wa ulimwengu mwenye kuwa tayari kusaidia wengine na mwenye kuwasikilia huruma. Lakini ataanza kutawala wakati gani?