Tuwafundishe Wale Wasiojua Kusoma Vizuri
1. Ni tatizo gani tunaloweza kukutana nalo katika mahubiri?
1 Tunapohubiri, mara kwa mara tunakutana na tatizo la kufundisha kweli ya Biblia watu wasiojua kusoma vizuri. Ni nini tunaloweza kufanya?
2. Namna gani na kwa nini tunaonyesha heshima wale wasiojua kusoma vizuri?
2 Tuwaheshimu: Jambo lililo la maana kwa Yehova ni hali ya moyoni ya mutu, wala si elimu yake. (1 Sam. 16:7; Met. 21:2) Kwa hiyo, hatuzarau wale wasiojua kusoma vizuri. Labda watu kama hao watakubali msaada wetu tunapowaonyesha heshima na uvumilivu. (1 Pet. 3:15) Hilo linaweza kumaanisha pia kwamba tutaepuka kumkaza mutu asome andiko ao fungu. Mutu anapoendelea kujifunza kweli za Biblia ambazo ni za maana sana, anaweza kuwa na hamu sana ya kujifunza kusoma vizuri ili apate furaha inayotokana na kusoma Neno la Mungu “kwa sauti ya chini mchana na usiku.”—Zab. 1:2, 3.
3. Ni njia gani za kufundisha tunazoweza kutumia ili kufundisha wale wasiojua kusoma vizuri?
3 Tutumie Njia Mbalimbali za Kufundisha: Picha ni njia nzuri sana za kufundisha watu na kuwasaidia kukumbuka mambo wanayojifunza. Unaweza kuomba mwanafunzi aeleze mambo anayoona kwenye picha iliyo katika kitabu munachotumia. Kisha, tumia maulizo yaliyo wazi ili kumsaidia aelewe mambo ambayo picha inafundisha. Tumia maandiko yanayofundisha mambo fulani unayotaka kukazia kuhusiana na picha. Picha zinaweza pia kutumiwa ili kujikumbusha habari munayojifunza. Musijifunze mambo mengi mara moja. Kazia kichwa cha habari na mambo makuu, na pia epuka kuzungumzia mambo yasiyo katika habari munayochunguza. Soma maandiko moja kwa moja katika Biblia, na uliza maulizo ili kuhakikisha kwamba mwanafunzi anaelewa mambo muliyosoma. Hilo linaweza kumsaidia afurahie zaidi kujifunza kusoma vizuri ili kujitafutia yeye mwenyewe mambo katika Biblia.
4. Namna gani tunaweza kusaidia mwanafunzi wetu ajifunze kusoma vizuri?
4 Njia Zingine za Kujifunza Kusoma Vizuri: Watu wasiojua kusoma vizuri ao ambao hawakupata nafasi nyingi za kujifunza kusoma bila magumu wanaweza kuelewa vizuri sana habari wanazojifunza na kuzichunga akilini. Munaweza kuwatia moyo watu kama hao watumie kaseti ao CD zinazopatikana za vitabu vyetu. Kusikiliza kwa uangalifu usomaji na wakati huohuo kufuata katika kitabu, na hata kurudilia maneno kwa sauti ya chini, kutasaidia mutu ajue kusoma vizuri. Kitabu Jitahidi Kujifunza Kusoma na Kuandika kinaweza pia kumsaidia. Katika maeneo fulani, wazee wanaweza pia kupanga masomo ya kujifunza kusoma katika kutaniko. Mapendekezo hayo yenye kufaa yatatuwezesha kusaidia wale wasiojua kusoma vizuri waelewe “maandishi matakatifu,” ambayo yanaweza kuwafanya wawe wenye hekima kwa ajili ya wokovu.—2 Tim. 3:15.