Namna ya Kuwasaidia Wale Wasiojua Kusoma Vizuri
1. Kuwafundisha Biblia wale wasiojua kusoma vizuri kuna magumu gani?
1 Wasikilizaji wasiojua kusoma vizuri wanaweza kupendezwa na mambo ya kiroho, lakini wanaogopeshwa na Biblia na vitabu vingine. Pengine hatuwezi kupata matokeo mazuri tukiwatolea watu hao kitabu Biblia Inafundisha tunapokutana nao kwa mara ya kwanza. Namna gani tunaweza kuwasaidia watu hao wamujue Mungu? Tuliuliza wahubiri wenye uzoefu kutoka inchi zaidi ya 20 watuambie wanafanya nini ili kuwasaidia watu hao. Walitoa mashauri yanayopatikana hapa chini.
2. Ni vichapo gani tunaweza kutumia ili kumusaidia mutu asiyejua kusoma vizuri?
2 Ikiwa mwanafunzi hajue kusoma vizuri ao hajue hata kusoma, unaweza kuanza kwa kutumia broshua, Umusikilize Mungu ao Umusikilize Mungu Ili Uishi Milele. Painia mumoja kutoka Amerika anamuonyesha mwanafunzi broshua zote mbili kisha anamuuliza ni broshua gani anafurahia sana. Biro ya tawi ya Kenya ilitoa ripoti ya kwamba broshua hizo mbili ni vyombo vizuri sana vya kutumia kwa sababu, kwa kawaida, watu wa Afrika wanafundishwa kwa kuelezewa mambo kuliko kutumia maulizo na majibu. Mutu anayejua kusoma vizuri anaweza kufurahia kujifunza kwa kusoma na kuulizwa maulizo. Lakini, mutu asiyejua kusoma vizuri pengine hatafurahia njia hiyo. Ikiwa mwanafunzi ana uwezo fulani wa kusoma, wahubiri wengi wanafurahia kutumia broshua Habari njema inayotoka kwa Mungu!, ao Unaweza Kuwa Rafiki ya Mungu!, ao pengine Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia ili kuanzisha funzo.
3. Tunapaswa kuelewa mambo gani kuhusu wale wasiojua kusoma yanayoweza kutusaidia tupate matokeo mazuri tunapowafundisha?
3 Pongeza Mwanafunzi: Wale wasiojua kusoma vizuri wanaweza kusikia haya, na wengi wanajiona kuwa wa hali ya chini. Kwa kawaida, kuwafanya watu hao wajione kuwa wa lazima ni hatua ya kwanza ya kuwasaidia wajifunze kweli. Watu wengi wasiojua kusoma wana akili ya kujifunza na wanaweza kuelewa mambo. Waonyeshe heshima ambayo wanastahili, na usiwazarau. (1 Pet. 3:15) Watachochewa kuendelea kujifunza ikiwa wanajisikia kwamba bidii yao inafurahisha wengine na kutambua kwamba wanafanya maendeleo ya kiroho. Kwa hiyo, uwapongeze kila mara.
4. Namna gani tunaweza kuwatia moyo wale wasiojua kusoma vizuri wajitayarishe kwa ajili ya funzo?
4 Hata kama mwanafunzi hajue kusoma vizuri, umutie moyo atayarishe funzo. Wahubiri fulani katika Afrika Kusini, wanawatia moyo wanafunzi wao wamuombe mutu wa jamaa ao rafiki anayejua kusoma vizuri awasaidie. Muhubiri mumoja wa Uingereza anawatia moyo wanafunzi wake kutayarisha kwa kuwapatia kitabu chake wanapozungumuzia mafungu fulani ili waone kwamba ni rahisi kupata majibu katika kitabu ikiwa yametiwa mistari. Ndugu mumoja wa India anawatia moyo wanafunzi wake waangalie picha katika somo watakalojifunza juma linalokuja na kutafakari kuhusu picha hizo mbele ya wakati.
5. Namna gani tunaweza kuonyesha uvumilivu tunapoongoza funzo?
5 Uwe Mwenye Uvumilivu: Hata iwe unatumia kichapo gani, kazia mambo ya lazima, na umusaidie mwanafunzi wako aelewe vizuri mambo hayo. Mwanzoni, munaweza kuzungumuza kwa dakika 10 ao 15 tu. Musijifunze mambo mengi sana kwa wakati mumoja, munaweza kujifunza mafungu machache tu wakati wa kila funzo. Uwe mwenye uvumilivu ikiwa mwanafunzi anasoma polepole. Pengine atachochewa kusoma vizuri zaidi anapoendelea kumupenda Yehova. Ili kumusaidia mwanafunzi wako afanye hivyo, ni vizuri kumualika ahuzurie mikutano unapojifunza naye kwa mara ya kwanza.
6. Namna gani tunaweza kuwasaidia watu wajifunze kusoma?
6 Ikiwa wanafunzi wa Biblia wamejua kusoma vizuri, watafanya maendeleo ya kiroho haraka. (Zab. 1:1-3) Wahubiri wengi wamewasaidia wanafunzi wao kusoma kwa kutumia broshua Jitahidi Kusoma na Kuandika kwa dakika fulani kila mwisho wa funzo. Ikiwa mwanafunzi anavunjika moyo, unaweza kumuonyesha maendeleo fulani ambayo amefanya tangu mulipoanza kujifunza naye. Umuhakikishie kwamba Yehova atabariki kujikaza kwake, na umutie moyo aombe Yehova musaada. (Met. 16:3; 1 Yoh. 5:14, 15) Wahubiri fulani wa Uingereza wanawatia moyo wanafunzi wao wajiwekee miradi fulani wanayoweza kutimiza hatua kwa hatua, pengine kuanza kujua vizuri herufi ao alfabeti, kisha kutafuta na kusoma maandiko fulani, na mwishowe kusoma vichapo vya Biblia vinavyopatikana katika luga rahisi. Kuwasaidia watu wajue kusoma kunamaanisha mara nyingi pia kuwatia moyo wapende kufanya hivyo, si kuwafundisha tu namna ya kusoma.
7. Sababu gani hatupaswe kusita kuwahubiria wale wasiojua kusoma vizuri?
7 Yehova hawazarau wale wasiojua kusoma vizuri. (Ayu. 34:19) Yehova anachunguza moyo wa mutu. (1 Nya. 28:9) Kwa hiyo, usisite kuwahubiria wale wasiojua kusoma vizuri. Una vyombo vingi vizuri unavyoweza kuanza navyo. Baadaye, unaweza kumupeleka mwanafunzi katika kitabu Biblia Inafundisha na kumutolea nafasi ya kujifunza mengi zaidi kuhusu Maandiko.
Wale wasiojua kusoma wanaweza kusikia haya, na wengi wanajiona kuwa wa hali ya chini. Kwa kawaida, kuwafanya watu hao wajione kuwa wa lazima ni hatua ya kwanza ya kuwasaidia wajifunze kweli