Tufundishe kwa Njia Rahisi
1. Ni jambo gani moja la maana linalofanya mafundisho yaweze kumsaidia mutu anayejifunza?
1 Kufundisha kwa njia iliyo rahisi ni jambo la maana sana ili mafundisho yamsaidie mutu anayejifunza. Kufikiria kwa uangalifu jinsi Yesu, Mwalimu Mkuu, alivyofundisha kunaweza kutusaidia kufanya ‘ufundi wetu wa kufundisha’ uwe mzuri zaidi.—2 Tim. 4:2; Yoh. 13:13.
2. Kufundisha kwa njia rahisi kunaomba nini, na kuna matokeo gani?
2 Tutumie Maneno Rahisi: Mahubiri ya Yesu ya Mlimani yana kweli fulani za maana zaidi ambazo hazijafundishwa na mutu yeyote; kweli hizo zote zilielezwa kwa njia rahisi. (Mt., sura 5-7) Mkutano wa watu waliomsikiliza Yesu ‘walishangazwa na njia yake ya kufundisha.’ Maofisa waliotumwa ili kumkamata waliguswa na mafundisho yake na kusema: “Mtu mwingine hajapata kamwe kusema kama huyu.” (Mt. 7:28, 29; Yoh. 7:46) Hatuhitaji kutumia maneno ya kujionyesha kwamba tunajua lugha, misemwa isiyoeleweka ao mifano mingi ili kufanya kweli isadikishe kabisa wengine. Tunaweza kueleza kweli waziwazi kwa kutumia maneno ambayo watu wanafahamu vizuri.
3. Kwa nini watu fulani wana mwelekeo wa kuwafundisha wasikilizaji wao habari nyingi sana, na namna gani tunaweza kuepuke kufanya hivyo?
3 Tusifundishe Habari Nyingi kwa Wakati Mmoja: Yesu alifikiria wasikilizaji wake. Hakufundisha habari nyingi kwa wakati mmoja. (Yoh. 16:12) Tunapaswa kuwa na uwezo wa kutambua mahitaji ya wasikilizaji wetu na kuwa tayari kupatanisha ujumbe wetu na mahitaji yao, zaidi sana tunapohubiria watu wa jamaa, wapya wenye kupendezwa, ao watoto. Tunapaswa kuwa waangalifu ili tusiwafundishe habari nyingi sana hata ikiwa wanaonekana kuwa wenye kutufuata kwa uangalifu. Wale walio na mioyo yenye haki wataendelea kujifunza kumjua Mungu wa kweli Yehova.—Yoh. 17:3; 1 Kor. 3:6.
4. Kwa nini ni jambo lenye faida kukazia mambo makuu kuliko kuongeza habari nyingi zisizo za maana?
4 Tukazie Mambo Makuu: Yesu hakufanya mafundisho yake yawe magumu kwa kuzungumzia habari nyingi zaidi. Aliposema: ‘Wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho watatoka,’ haikuwa wakati wa kutoa habari nyingi kuhusu watu watakaofufuliwa ili kuishi mbinguni na kuhusu watu watakaofufuliwa ili kuishi duniani. (Yoh. 5:28, 29) Tunapoongoza mafunzo ya Biblia, tunapaswa kukazia mambo makuu na kuepuka mwelekeo wa kuongeza habari zisizo za maana ambazo hazipatikane katika kitabu.
5. Ni baraka gani tunayoweza kupata ikiwa tunafundisha kwa njia rahisi?
5 Sisi ni wenye shukrani kabisa kwa kuwa Yehova ametufundisha kwa njia rahisi mambo yote tunayohitaji kujua. (Mt. 11:25) Basi, na tufundishe kwa njia rahisi na kupata furaha inayotokana na utumishi wenye kuzaa matunda.