Tuhubirie Watu Wanaozungumza Luga ya Kigeni
1. Tunakutana na watu gani tunapohubiri katika eneo letu?
1 Yesu Kristo alitabiri kwamba habari njema ingehubiriwa katika ulimwengu wote “ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote.” Wale wote wanaoshiriki katika kazi ya kuhubiri na kufundisha wanaona maneno hayo kuwa ya maana kabisa. (Mt. 24:14; 28:19, 20) Tunapohubiri na kufanya wanafunzi, tunaweza kukutana na watu wa inchi zingine wanaozungumza luga tofauti na yetu. Wao pia wanahitaji kusikia habari ya Ufalme na kushikilia kweli mbele ya kuja kwa ile siku ya Yehova yenye kuogopesha. (Mal. 3:18) Tunaweza kufanya nini ili kuhubiria watu wanaozungumza luga ya kigeni ambao wanaishi katika eneo letu?
2. Namna gani tunamwiga Yehova tunapohubiria wale wanaozungumza luga nyingine?
2 Tuwaone Wale Wanaozungumza Luga Nyingine Kama Yehova Anavyowaona: Ili kuonyesha kila mutu upendo wa Yehova bila ubaguzi katika eneo letu, tunapaswa kuwa na hamu kubwa ya kusaidia watu wapate ujuzi sahihi kumhusu Mungu wa kweli Yehova, iwe wanazungumza luga gani. (Zab. 83:18; Mdo. 10:34, 35) Hata ikiwa tunahubiria kwanza wale wanaozungumza luga ya kutaniko letu, tunapaswa kuwahangaikia pia wale wanaozungumza luga nyingine na kutafuta nafasi za kuwatolea ujumbe wa Ufalme wa Mungu. Kutokuhubiria wale wanaozungumza luga nyingine hakupatane na kusudi la Yehova anayetaka tutolee ushahidi watu wa mataifa yote. Basi, namna gani tunaweza kuwasaidia wale wanaozungumza luga tofauti na yetu?
3. Ni kijitabu gani chenye kusaidia ambacho tumetolewa, na namna gani tunaweza kujitayarisha ili kukitumia?
3 Tutumie Kijitabu Habari Njema kwa Ajili ya Watu wa Mataifa Yote: Kijitabu hicho kilichapishwa ili kutusaidia tunapokutana na watu wanaozungumza luga tofauti na yetu. Tukichukue kila wakati, tujue vizuri mambo yaliyo ndani, na tujitayarishe vizuri ili kukitumia. Ili kupata luga ya mutu kwa uharaka, tutie alama kwenye luga mbalimbali zinazozungumzwa katika eneo letu. Ikiwa kuna vitabu katika luga hizo, inaweza kuwa vizuri kuchukua vitabu fulani vya kutolea watu kisha kutumia habari iliyo katika kijitabu hicho.
4. Namna gani tunaweza kutumia kijitabu Mataifa katika kazi yetu ya kuhubiri?
4 Ikiwa katika mahubiri unakutana na mutu anayezungumza luga ambayo haujui, mwonyeshe kwanza jalada ya kijitabu hicho. Fungua kijitabu kwenye karte ya ulimwengu iliyo upande mwingine wa jalada ya kwanza, ujishote kidole wewe mwenyewe na uonyeshe inchi yako, na umwambie kwamba ungetaka kujua inchi yake na luga anayozungumza. Ukiisha kujua luga yake, fungua ukurasa unaoonyesha luga mbalimbali, tafuta luga na ukurasa ambako luga hiyo inapatikana, mwonyeshe maneno yenye kuandikwa kwa herufi nzito nyeusi yaliyo juu ya ukurasa, na kisha umwonyeshe kwamba ungetaka asome habari inayofuata. Anapomaliza kusoma, mtolee trakti katika luga yake ao umwonyeshe maneno yanayoandikwa katika rangi ya majivu, yanayoonyesha kwamba ungetaka kuja kumwona tena na kumletea kitabu katika luga yake. Kisha onyesha maneno “jina langu” yanayoandikwa kwa herufi nzito nyeusi, na utamke jina lako waziwazi. Onyesha maneno “jina lako” yanayoandikwa kwa herufi nzito nyeusi, na ungojee ajibu. Ufanye mpango wa kumrudilia.
5. Ni mpango gani wa lazima tunaoweza kufanya ili kushugulikia vizuri wale wanaozungumza luga nyingine ambao wanapendezwa na kweli?
5 Tufanye Mipango Ili Watembelewe: Tunapaswa kujikaza sana ili kurudilia wale wanaoonyesha kupendezwa na ujumbe wa Ufalme, iwe wanazungumza luga gani. Tukiisha kuona kwamba mutu anampenda Mungu na kupendezwa na Neno lake, Biblia, tunapaswa kujaza fomu Tafadhali Fuatia Upendezi (S-43) na kuitolea bila kukawia mwandishi wa kutaniko; yeye ataituma kwenye biro ya tawi ili mutu huyo atembelewe na mhubiri fulani anayezungumza luga yake. Kisha, biro ya tawi itatuma fomu hiyo kwenye kikundi kinachotumia luga hiyo. Watakapoipata, watafanya mipango ili mutu huyo atembelewe bila kukawia. Mwandishi anaweza kumtolea mwangalizi wa utumishi kopi ya fomu hiyo ili ajue kwamba katika eneo, kuna watu wanaozungumza luga fulani ambao wanapendezwa na kweli. Fomu hiyo itatumiwa tu ikiwa mutu anapendezwa kabisa.
6. Tuna daraka gani ikiwa tunakutana na mutu mwenye kupendezwa anayezungumza luga nyingine?
6 Kunaweza kupita muda fulani kuanzia wakati ambapo fomu S-43 ilitumwa mpaka wakati ambapo mutu mwenye kupendezwa anatembelewa na mhubiri anayezungumza luga yake. Kwa hiyo, ili kumsaidia mutu mwenye kupendezwa, mhubiri aliyejaza fomu S-43 anaweza kumsaidia aendelee kupendezwa mpaka atakapotembelewa na mhubiri anayezungumza luga yake. Katika hali fulani, funzo la Biblia linaweza kuanzishwa pamoja na mutu huyo mwenye kupendezwa. Hata hivyo, kwa kungojea atembelewe na mutu fulani anayezungumza luga yake, namna gani mhubiri anaweza kupata vitabu katika luga ya mutu huyo anayependezwa?
7. Ni mpango gani unaoweza kutusaidia kupata vitabu katika luga za wale tunaoweza kukutana nao?
7 Vitabu vya Kutumia: Makutaniko hayapaswi kuwa na vitabu vingi katika luga zingine. Lakini, ikiwa mwangalizi wa utumishi anaona kwamba kuna watu wengi wanaozungumza luga fulani ambao wameanza kupendezwa na kweli, anaweza kuona kuwa jambo lenye kufaa kuchunga katika stoki vitabu fulani katika luga hiyo ambavyo wahubiri wanaweza kutumia. Ikiwa kutaniko halina vitabu katika luga hiyo, wanaweza kuvifanyia ombi. Inaweza kuchukua muda fulani mbele ya kupata vitabu hivyo. Kwa hiyo, kuna mpango wa kuchapisha vitabu kutoka kwenye kituo chetu cha Internet www.watchtower.org. Kwenye kituo hicho, kuna vitabu vingi katika luga mbalimbali ambavyo wahubiri ao watu wanaopendezwa wanaweza kupata mara moja. Bila shaka, mpango huo utakuwa wenye kufaa ili kuendelea kusaidia wale wenye kupendezwa wanaozungumza luga nyingine.
8. Kutaniko lina daraka gani katika kuendelea kusaidia wale wenye kupendezwa wanaozungumza luga nyingine?
8 Daraka la Kutaniko: Mahali fulani ambako kuna watu wengi wanaozungumza luga ya kigeni, labda kusiwe kutaniko lililo karibu linalotumia luga yao. Kwa hiyo, watu wenye kupendezwa wanaozungumza luga ya kigeni wanaweza kualikwa wahuzurie mikutano yenu. Kuwakaribisha kwa uchangamfu na kupendezwa nao kunaweza kuwatia moyo wahuzurie mikutano kwa ukawaida. Mwanzoni, kunaweza kuwa kizuizi kwa sababu ya luga na malezi, lakini hakuna jambo lolote linaloweza kuwazuia Mashahidi wa Yehova wa ulimwenguni pote kuonyesha upendo wa kweli wa Kikristo. (Zef. 3:9; Yoh. 13:35) Je, unazungumza vizuri luga nyingine? Ikiwa ni hivyo na ikiwa uko tayari kuwarudilia watu wanaozungumza luga hiyo, tafazali julisha mwandishi wa kutaniko lenu ili ajulishe biro ya tawi. Jambo hilo litakuwa lenye kusaidia wakati biro ya tawi inatafuta mhubiri anayeweza kuendelea kusaidia watu wanaozungumza luga nyingine.
9. Ni wakati gani litakuwa jambo lenye kufaa wahubiri wajifunze luga nyingine, na hilo litafanywa namna gani?
9 Kujifunza Luga Nyingine: Tunapowasaidia wale wanaozungumza luga nyingine, ni vizuri zaidi kuwatia moyo waanze kuhuzuria mikutano katika kutaniko linalotumia luga yao ikiwa kutaniko hilo haliko mbali nao. Hata hivyo, ikiwa hilo haliwezekane, wahubiri fulani wanaweza kujifunza luga ya watu hao wenye kupendezwa ili waweze kuwasaidia. Ikiwa hakuna kutaniko lililo karibu, biro ya tawi inaweza kuamua kuanzisha masomo ya kujifunza luga kwa sababu eneo lina watu wengi wanaozungumza luga nyingine waliotoka inchi nyingine ao wazaliwa wa inchi. Ikiwa ni hivyo, biro ya tawi inaweza kujulisha makutaniko yaliyo karibu kuhusu uhitaji wa kuwa na masomo ya kujifunza luga ya kigeni na itatoa tangazo kuhusu masomo hayo. Wale watakaofuata masomo hayo watakuwa na kusudi la kuhamia katika kikundi ao kutaniko la luga wanayojifunza ili kuhubiria watu wanaozungumza luga hiyo.
10. Kikundi cha luga ya kigeni kinaweza kuundwa wakati gani, na ni mambo gani yanayopaswa kutimizwa?
10 Kuunda Kikundi cha Luga Nyingine: Ili kuunda kikundi cha luga fulani, ni lazima mambo mane yatimizwe. (1) Kunapaswa kuwe kiasi cha kutosha cha watu wenye kupendezwa wanaozungumza luga hiyo. (2) Wahubiri fulani wanapaswa kujua ao kuwa wenye kujifunza luga hiyo. (3) Mzee ao mtumishi wa huduma anayestahili anapaswa kuwa tayari kusimamia kikundi na kuongoza mkutano mmoja hivi kila juma katika luga hiyo. (4) Baraza la wazee linapaswa kuwa tayari kutegemeza kikundi hicho. Wakati mambo hayo yanatimizwa kwa kiasi fulani, hivyo baraza la wazee litajulisha biro ya tawi kuhusu hali fulani za kikundi hicho na watafanya ombi ili kutaniko hilo litambuliwe na biro ya tawi kwamba linategemeza kikundi kinachotumia luga ya kigeni. (Ona kitabu Tengenezo, uku. 106-107.) Mzee atakayeshugulikia kikundi ataitwa “mwangalizi wa kikundi,” ikiwa ni mtumishi wa huduma ataitwa “mtumishi wa kikundi.”
11. Kwa nini ni pendeleo kubwa kuhubiria watu wanaozungumza luga ya kigeni katika eneo tulilogawiwa?
11 Kuhubiria watu wanaozungumza luga ya kigeni katika eneo letu ni sehemu ya maana sana ya kampanye ya ulimwenguni pote ya kuhubiri iliyoanzishwa na Yesu Kristo, Mfano wetu. Acheni basi tutimize sehemu yetu na kuona jinsi Yehova ataendelea kutikisa mataifa na kuleta vitu vyenye kutamanika kwake. (Hag. 2:7) Inafurahisha kabisa kuungana mkono katika kazi hiyo! Yehova na atubariki tunapojikaza sisi wote kuhubiria watu wanaozungumza luga ya kigeni katika maeneo yetu kwa kuwa tunakumbuka sikuzote kwamba Mungu anaweza kukuza, hata ikiwa kuna vizuizi vinavyotokana na luga za wanadamu!—1 Kor. 3:6-9.