Je, Umekwisha Kumwonyesha Mutu Namna Tunavyojifunza na Watu Biblia Unapomhubiria kwa Mara ya Kwanza?
Tunapowaelezea jinsi tunavyojifunza na watu Biblia, wasikilizaji fulani wanasema kwamba hawapendezwi ao kwamba wanajifunza Biblia katika kanisa lao. Kwa kuwa labda hawajui kwamba namna yetu ya kujifunza Biblia ni tofauti na ya dini zingine, hawaelewi kwamba funzo la Biblia linaweza kuwa lenye kuelimisha na lenye kufurahisha. Kwa hiyo, kuliko kumuelezea tu mutu jinsi tunavyojifunza Biblia na watu, kwa nini usitumie dakika chache unapomhubiria kwa mara ya kwanza ili kumwonyesha jinsi funzo la Biblia linavyofanywa? Kwa mfano: usimwambie tu mutu kwamba wewe ni mpishi mzuri na kwamba utamletea chakula utakaporudi; mwonjeshe papohapo! Ona jinsi unavyoweza kufanya hivyo kwa dakika chache tu, kwa kutumia mapendekezo yaliyo katika Huduma Yetu ya Ufalme ya mwezi wa 1, 2006 kuanzia kwenye ukurasa wa 6:
“Je, unafikiri kwamba maneno haya yatatimizwa siku fulani? [Soma Isaya 33:24, na acha mutu ajibu.] Acha nikuonyeshe jambo fulani lenye kupendeza kuhusu habari hiyo.” Umtolee kitabu Biblia Inafundisha, na umwombe afungue kwenye ukurasa wa 36 fungu 22. Soma ulizo chini ya ukurasa, na umwombe msikilizaji atafute jibu unaposoma fungu. Kisha uliza tena ulizo, na usikilize maelezo yake. Soma pamoja naye andiko lingine kati ya maandiko yaliyo katika fungu. Utokeze ulizo litakalojibiwa munapokutana tena, na ufanye mpango wa kumrudilia. Umekwisha kuanzisha funzo la Biblia!