Uwasaidie Watu ili Wamusikilize Mungu
1. Broshua gani zilitangazwa kwenye Mukusanyiko wa wilaya wenye kichwa “Ufalme wa Mungu na Uje!”, na sababu gani broshua hizo zinasaidia sana?
1 Kwenye Mukusanyiko wa wilaya wenye kichwa “Ufalme wa Mungu na Uje!” broshua mbili zilitangazwa: Umusikilize Mungu ili Uishi Milele na broshua ya pili iliyorahisishwa Umusikilize Mungu. Kwa kuwa broshua hizo hazina maandishi mengi, zinaweza kutafsiriwa haraka na kwa urahisi. Kwa hiyo, mara tu broshua Umusikilize Mungu ili Uishi Milele ilipotokea katika Kiingereza, ilikuwa imekwisha kukubaliwa kutafsiriwa katika luga 431.
2. Ni nani hasa watakaofaidika na broshua hizi?
2 Ni nani hasa watakaofaidika na broshua hizi? Fikiria hali zifuatazo zinazotokea mara nyingi duniani pote:
• Muhubiri anapozungumuza na mutu kwa mara ya kwanza ao anapomurudilia, anatambua kama mutu huyo hajui kusoma ao hasome vizuri.
• Muhubiri anahubiria watu wanaozungumuza luga ambayo tumetafsiri vitabu vichache ao hakuna kitabu ambacho kimetafsiriwa katika luga hiyo. Ao watu wengi katika eneo hawana uwezo wa kusoma luga wanayoongea vizuri.
• Muhubiri anapotumia luga ya ishara ili kuhubiri viziwi katika eneo lake.
• Muzazi anatamani kumufundisha mutoto wake mudogo kweli ambaye hajajua bado kusoma.
3. Namna gani habari zimepangwa katika broshua Umusikilize Mungu?
3 Namna Habari Zimepangwa Katika Broshua Hizo: Broshua Umusikilize Mungu ina maandishi machache tu—kwa kawaida ni musemwa wenye maneno machache chini ya ukurasa na pia andiko ambalo linakazia mambo makuu. Sababu gani habari imepangwa hivyo? Kwa mufano, wazia mutu fulani anakupatia broshua inayoandikwa katika luga ambayo labda haujue kusoma, je, utapendezwa na broshua hiyo hata ikiwa ina picha nzuri? Labda hapana. Vilevile, watu ambao hawajue kusoma wanaogopeshwa na vitabu vilivyo na maandishi mengi. Kwa hiyo, kila ukurasa wa Broshua hiyo una picha ambazo zimetayarishwa vizuri, na kuna alama inayoonyesha kama ukiisha kuzungumuzia picha fulani unaweza kuzungumuzia picha inayofuata.
4. Namna gani habari zimepangwa katika broshua Umusikilize Mungu ili Uishi Milele?
4 Broshua Umusikilize Mungu ili Uishi Milele ina picha zilezile zinazopatikana katika broshua Umusikilize Mungu. Broshua hiyo imetayarishwa ili kujifunza na wale wasiojua kusoma vizuri na wale wanaojifunza kusoma. Pia, muhubiri anaweza kutumia broshua hiyo anapojifunza pamoja na mutu aliye na broshua Umusikilize Mungu. Kwenye upande wa kushoto juu, mwanzoni mwa kila somo lililo kwenye kurasa mbili, kuna ulizo linalojibiwa kwenye kurasa hizo mbili. Karibu na picha kuna pia maelezo na maandiko ya Biblia. Kwenye kurasa zingine upande wa kuume chini, kuna kisanduku kilicho na maelezo ya zaidi na maandiko ya Biblia ambayo muhubiri anaweza kuzungumuzia pamoja na mwanafunzi, kwa kutegemea uwezo wake.
5. Wakati gani na namna gani tunaweza kuwatolea watu broshua hizo?
5 Namna ya Kutumia Broshua Hizo: Kila wakati unapohubiri nyumba kwa nyumba na unaona kuwa inafaa, unaweza kuwatolea watu broshua moja kati ya broshua hizo mbili, hata ikiwa broshua hizo hazikupangwa kutolewa watu mwezi huo. (Ona kisanduku “Namna Broshua Hizo Zinavyoweza Kutolewa.”) Unaweza kuionyesha mutu mwenye kupendezwa unapomurudilia kwa kumuambia tu kama ungependa kumuonyesha kitu fulani, na kisha umupatie broshua.
6. Namna gani tutaongoza funzo la Biblia kwa kutumia broshua hizo?
6 Broshua Umusikilize Mungu haina maulizo, kwa hiyo, mazungumuzo hayatakuwa ya maulizo na majibu, kama tunavyofanya tunapojifunza pamoja na watu kitabu Biblia Inafundisha. Mahali pote duniani, watu wanafurahia kusikiliza hadisi. Kwa hiyo, eleza hadisi zilizoandikwa katika Biblia ukitumia picha zilizo katika broshua. Toa maelezo kuhusu picha. Sema kwa uchangamfu. Umuombe musikilizaji akuambie anaona nini na anafikiri nini juu ya mambo hayo. Umusomee maandiko yaliyo chini ya ukurasa, na ufikiri na musikilizaji juu ya yale ambayo maandiko hayo yanasema. Umuulize mwanafunzi maulizo ili aseme yale anayowaza na uhakikishe kwamba anaelewa. Ikiwa mwanafunzi anatumia broshua Umusikilize Mungu ili Uishi Milele, musome pamoja maneno na maandiko munapozungumuzia kila picha.
7. Namna gani tunaweza kuwasaidia wanafunzi wetu wafanye maendeleo?
7 Saidia Mwanafunzi Afanye Maendeleo: Tunatumaini kama mazungumuzo yenu yatamuchochea mwanafunzi atamani kujifunza kusoma ili yeye mwenyewe ajisomee na kujifunza hivyo mambo yanayomuhusu Yehova. (Mt. 5:3; Yoh. 17:3) Kwa hiyo, ikiwa mazungumuzo yenu yanategemea broshua Umusikilize Mungu, labda kisha wakati fulani, unaweza kumuuliza ikiwa unaweza kumufundisha kusoma na munaweza sasa kuanza kujifunza broshua Umusikilize Mungu ili Uishi Milele. Hata ikiwa munamaliza broshua gani kati ya broshua hizo, jua kama mwanafunzi huyo hajastahili kubatizwa. Kwa hiyo, unapaswa kuendelea kujifunza pamoja naye kitabu Biblia Inafundisha ao kitabu kingine kinachofaa ambacho kitamusaidia aelewe Biblia vizuri.
8. Je, wewe ni mwenye shukrani kwa sababu ya broshua hizo; sababu gani?
8 Ikiwa watu wanataka kuishi milele, ni lazima wamusikilize Mungu, Mutawala wa ulimwengu wote. (Isa. 55:3) Na Mungu anataka “watu wa namna zote,” kutia ndani wale wasiojua kusoma, wajifunze kumusikiliza. (1 Tim. 2:3, 4) Sisi ni wenye shukrani sana kwa Yehova kwa sababu ametupatia broshua hizi ambazo tunaweza kutumia ili kuwafundisha watu wamusikilize Mungu!
[Sanduku katika ukurasa wa 3]
Namna Broshua Hizo Zinavyoweza Kutolewa
Umuonyeshe musikilizaji ukurasa wa 2 na wa 3, na umuambie hivi: “Je, ungefurahia kuishi katika dunia kama hii? [Acha ajibu.] Maandiko yanaahidi [ao, kitabu hiki kitakatifu kinaahidi] kama karibuni Mungu atafanya dunia hii iwe mahali pazuri na penye amani ambapo hakutakuwa maskini ao wagonjwa. Ona mambo tunayopaswa kufanya ili kuishi katika dunia hiyo. [Soma andiko la Isaya 55:3, ambalo limetajwa kwenye sehemu ya juu ya ukurasa wa 3.] Katika andiko hilo Mungu anasema ‘muje kwangu’ na ‘munisikilize.’ Lakini, namna gani tunaweza kumusikiliza Mungu?” Fungua ukurasa wa 4 na wa 5 na muzungumuzie jibu pamoja. Ikiwa hana wakati, umuachie broshua na ufanye mipango ya kumurudilia ili kuzungumuzia jibu.