‘Uwakusanye Watu Pamoja’
1. Mikusanyiko ya wilaya na ya kimataifa inafanana namna gani na kukusanywa kwa Waisraeli chini ya mulima Sinai?
1 Muda kidogo kisha Waisraeli kutoka Misri, Yehova alimuagiza Musa ‘awakusanye watu pamoja’ chini ya Mulima Sinai wasikilize maneno Yake ili waweze kumuogopa na kuwafundisha watoto wao njia Zake. (Kum. 4:10-13) Bila shaka imani ya Waisraeli ilitiwa nguvu na kwa hiyo waliendelea kukumbuka tukio hilo. Kisha miezi michache, Mashahidi wa Yehova watakuwa na mikusanyiko ya wilaya na ya kimataifa ili wafundishwe na Yehova. Tunapashwa kufanya nini ili tufaidike kabisa na mikusanyiko hiyo?
2. Tunapashwa kufanya nini ili ‘tuwe tayari’ kwa ajili ya mukusanyiko wa wilaya?
2 ‘Uwe Tayari’: Yehova aliwaamuru Waisraeli ‘wawe tayari’ kwa ajili ya mukusanyiko huo wa maana chini ya Mulima Sinai. (Kut. 19:10, 11) Vilevile, ni lazima wote watakaohuzuria mikusanyiko ya wilaya na ya kimataifa wajitayarishe vizuri, si wale tu watakaokuwa na sehemu kwenye mukusanyiko huo. Kwa mufano, wengi watahitaji kuomba mapumuziko kwenye kazi. Pengine hali yako inafanana na ile ya Nehemia. Nehemia alikuwa munyweshaji wa Mufalme Artashasta, kwa hiyo aliitika kuacha kazi hiyo ili kwenda kusaidia kujenga upya ukuta wa Yerusalemu. Lakini alijua kwamba mufalme anaweza kukataa kumuruhusu aende. Nehemia alisali, na kisha bila woga lakini kwa heshima, akamuambia mufalme ombi lake. Mufalme akamuruhusu aende na akamupatia hata wasaidizi! (Neh. 2:1-9) Zaidi ya kuomba mapumuziko kwenye kazi, hakikisha kwamba una feza za kukusaidia kusafiri na kupata mahali pa kupanga. Wazee watafanya mipango ili wale wasio na uwezo wasaidiwe. Panga kufika mbele ya wakati kwa kila kipindi cha mukusanyiko ili ‘ukazie uangalifu zaidi kuliko ilivyokawaida’ mambo yatakayofundishwa.—Ebr. 2:1.
3. Tutafanya nini ili kutayarisha moyo wetu kwa ajili ya mukusanyiko?
3 Njia ingine ya kuwa tayari kwa ajili ya mukusanyiko wa wilaya, ni kutayarisha moyo wetu ili tusikilize na kujifunza. (Ezra 7:10) Programu ya mukusanyiko itawekwa kwenye adresi yetu ya Internete jw.org mbele ya wakati na itakuwa na vichwa vya hotuba zote, na kila kichwa cha hotuba kitakuwa na andiko moja ao maandiko mawili ya maana. Munaweza kuzungumuzia habari hizo wakati wa Ibada yenu ya Familia katika majuma yanayotangulia mukusanyiko wenu. Wahubiri fulani wanachapisha programu ya mukusanyiko, kwa hiyo, wakati wa mukusanyiko wanaitumia ili kuandika mambo ya maana.
4. Namna gani mukusanyiko unaweza kuwasaidia wazazi wawafundishe watoto wao?
4 ‘Fundisha Watoto Wako’: Moja kati ya makusudi ya kuwakusanya Waisraeli kwenye Mulima Sinai ilikuwa kuwasaidia wazazi ‘wawafundishe watoto wao.’ (Kum. 4:10) Mukusanyiko unatolea wazazi nafasi nzuri ya kufanya hivyo pia. Wazazi wanapashwa kukaa na watoto wao wakati wa mukusanyiko na kuwasaidia wafuate kwa uangalifu. Mwishoni mwa kila siku ya mukusanyiko, na baada ya hapo wakati wa ibada ya familia, ni muzuri familia zizungumuzie programu ya mukusanyiko.
5. Tutafaidika namna gani kwa kuhuzuria mukusanyiko unaokuja?
5 Mukusanyiko wa Waisraeli kwenye Mulima Sinai uliwasaidia wafurahie pendeleo lao la pekee la kuwa taifa la Mungu. (Kum. 4:7, 8) Mukusanyiko wetu unaokuja utatusaidia kwa njia hiyohiyo. Kwa muda wa siku tatu tutaacha ulimwengu huu muovu wa Shetani, tutafaidika na chakula cha kiroho na kutiana moyo wakati tutakuwa katika paradiso yetu ya Kiroho. (Isa. 35:7-9) Kwa kuwa siku ya Yehova inakaribia, basi, tusikose nafasi hiyo ya kukusanyika pamoja ili kutiana moyo!—Ebr. 10:24, 25.