Barua Kutoka Baraza Linaloongoza
Mashahidi wa Yehova Wenzetu Wapendwa:
Mtume Paulo alitumia kila nafasi ili kuonyesha upendo wake na shukrani kwa waamini wenzake. Aliwaandikia Wakristo wa Roma hivi: “Namshukuru Mungu wangu kupitia Yesu Kristo kuhusu ninyi nyote, kwa sababu imani yenu inazungumzwa kotekote ulimwenguni.” (Rom. 1:8) Ndiyo, katika Milki yote ya Roma, Wakristo hao wa karne ya kwanza walijulikana kwa sababu ya imani yao yenye nguvu na kwa sababu ya kazi yao ya kuhubiri kwa bidii. (1 The. 1:8) Haishangazi kwamba Paulo aliwapenda sana hivyo ndugu zake!
Kama Paulo, tunamshukuru Yehova kila mara tunapowafikiria ninyi. Tunawapenda sana ninyi wote! Na muwe na uhakika kwamba Yehova anapenda kila mmoja wenu. Wengine kati yenu wanashindana na upinzani mkali, lakini munaendelea kuhubiri. Bila shaka, roho ya ujasiri na ya bila woga munayoonyesha inafurahisha sana moyo wa Yehova!—Met. 27:11.
Munaposoma na kufikiri kwa uangalifu kuhusu habari yenye kichwa: “Utendaji wa Mashahidi wa Yehova Katika Nyakati za Sasa” yenye kuonyeshwa katika Kitabu cha Mwaka hiki chenye kusisimua na kutia nguvu imani, mutaona mambo mengi yenye kuhakikisha kwamba Bwana Yesu anaendelea mbele “akishinda na kukamilisha ushindi wake” na kwamba silaha yoyote itakayofanywa juu ya wafuasi wa Kristo haitakuwa na matokeo yoyote.—Ufu. 6:2; Isa. 54:17.
Paulo aliandikia Wakristo wa Filipi hivi: “Namshukuru Mungu wangu . . . kwa sababu ya mchango ambao mmeutoa kwa ajili ya habari njema.” (Flp. 1:3-5) Sisi washiriki wa Baraza Linaloongoza tuna mawazo yaleyale kuwahusu ninyi. Katika mwaka wa utumishi wa 2007, wahubiri 6,691,790 walitumia kwa ujumla saa 1,431,761,554 wakihubiri habari njema katika inchi 236 ulimwenguni pote. Munachangia sana ili kuendeleza kazi ya kuhubiri habari njema! Mufikiri kuhusu mamia ya maelfu ya watu ambao tumesaidia kwa kuwa tunatumika pamoja kwa bidii, yote hayo kwa kumsifu Yehova!
Pindi nyingine, Paulo alionyesha kwamba aliwasikilia ndugu zake huruma nyingi. Aliandikia ndugu wa Thesalonike hivi: “Daima sisi hukumbuka akilini . . . uvumilivu wenu kwa sababu ya tumaini lenu katika Bwana wetu Yesu Kristo mbele za Mungu wetu na Baba.” (1 The. 1:2, 3) Kwa kweli, maisha yana matatizo mengi. Magumu yanatokea, lakini ni lazima tuvumilie. Wewe unapambana na matatizo gani? Je, unavunjika moyo kwa sababu ugonjwa mkali unakuzuia sana kufanya yale ambayo unaweza kufanya katika utumishi wa Yehova? Je, mwenzi wako wa ndoa mpendwa aliyeishi pamoja nawe kwa miaka mingi, amemezwa na Sheoli, adui mkubwa asiyeshiba? (Met. 30:15, 16) Je, unajikaza bila matokeo kutafuta mtu wa kuunga naye ndoa anayempenda Yehova kama wewe, na ijapokuwa hivyo, unashikamana kwa uaminifu na shauri la Maandiko la kuoa ao kuolewa katika Bwana tu? (1 Kor. 7:39) Je, unajikaza sana kulea watoto wako katika maisha ya taabu ya kukosewa na feza? Hata hali yenu iwe gani, mukiendelea kutia faida za Ufalme pa nafasi ya kwanza, munaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova ‘hatasahau kazi yenu na upendo mulioonyesha kwa ajili ya jina lake.’ Tafazali, ndugu na dada, ‘musife moyo katika kufanya yaliyo mema’!—Ebr. 6:10; Gal. 6:9.
Ni nini kitawawezesha kuvumilia? Kama vile Wathesalonike, ni “tumaini katika Bwana wetu Yesu Kristo.” Kwa kufaa, Paulo alilinganisha baadaye “tumaini la wokovu” na kofia ya chuma iliyo nguvu inayoweza kumlinda Mkristo kutokana na mawazo yenye kuvunja moyo na mashaka yasiyokwisha.—1 The. 5:8.
Kwa kweli, munapovumilia kwa furaha, munajibia mashtaka ambayo Shetani alitokeza kuhusu enzi kuu ya ulimwengu wote. Shetani alisema kwamba watumishi wa Mungu wana hali ya kizalikio ya kuhangaikia tu faida zao wenyewe, na kwamba hata ikiwa wanaweza kumtumikia Mungu kwa muda fulani, watapunguza bidii yao katika ibada ya Mungu ikiwa majaribu yanaongezeka ao ikiwa ulimwengu huu unakawia kuliko walivyotazamia. Muna pendeleo la pekee la kumtoa waziwazi Ibilisi kuwa mwongo aliye mwovu kabisa! Kila siku inayopita ya maisha yenu inawafanya mukaribie zaidi utimizo wa tumaini lenu.
Kama vile Paulo alivyofurahia nafasi za kuwashukuru ndugu zake kwa sababu ya imani yao yenye nguvu, kujitoa kwao kwa moyo wote katika kazi ya kuhubiri, na uvumilivu wao, tunafurahia pia nafasi hii ili kuwashukuru na kuwahakikishia kwamba tunawapenda. Endeleeni kufanya kazi hiyo njema!
Mwaka ujao na ujazwe baraka nyingi kutoka kwa Mungu. Tunawatakia mema,
Ndugu zenu,
Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova