-
Mathayo 22:15-22Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
-
-
15 Ndipo Mafarisayo wakaenda kupanga njama pamoja ili wamtege Yesu kwa maneno yake.+ 16 Basi wakawatuma wanafunzi wao kwake, pamoja na wafuasi wa chama cha Herode.+ Wakamwambia: “Mwalimu, tunajua wewe husema ukweli nawe hufundisha njia ya Mungu katika kweli, na hutafuti kibali cha yeyote, kwa maana huangalii sura ya nje ya mtu. 17 Basi tuambie, unaonaje? Je, ni halali* au si halali kumlipa Kaisari kodi?”* 18 Lakini Yesu akijua uovu wao, akasema: “Kwa nini mnanijaribu, ninyi wanafiki? 19 Nionyesheni sarafu ya kodi.” Wakamletea dinari.* 20 Akawauliza: “Sura hii na maandishi haya ni ya nani?” 21 Wakajibu: “Ni ya Kaisari.” Ndipo akawaambia: “Basi, mlipeni Kaisari vitu vya Kaisari, na Mungu vitu vya Mungu.”+ 22 Waliposikia hilo, wakashangaa, wakamwacha na kwenda zao.
-
-
Luka 20:20-26Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
-
-
20 Baada ya kumtazama kwa makini, wakatuma watu waliowakodi kisiri wajifanye kuwa waadilifu ili wamnase Yesu kwa maneno yake+ na kumkabidhi kwa serikali na kwa mamlaka ya gavana. 21 Nao wakamuuliza: “Mwalimu, tunajua wewe husema na kufundisha kwa usahihi na huna ubaguzi, bali unafundisha njia ya Mungu kupatana na kweli: 22 Je, ni halali* au si halali kwetu kumlipa Kaisari kodi?”* 23 Lakini alitambua ujanja wao na kuwaambia: 24 “Nionyesheni dinari.* Ina sura na maandishi ya nani?” Wakajibu: “Kaisari.” 25 Akawaambia: “Basi mlipeni Kaisari+ vitu vya Kaisari, na Mungu vitu vya Mungu.”+ 26 Kwa hiyo, wakashindwa kumnasa kwa maneno yake mbele ya watu, nao wakanyamaza wakiwa wameshangazwa na jibu lake.
-